AU yakaribisha mazungumzo ya Khartoum na Juba

Umoja wa Afrika umeyapokea vizuri matokeo ya mazungumzo kati ya Marais wa Sudan na Sudan Kusini na makubaliano yaliyofikiwa kati ya pande mbili hizo kwa ajili ya kutekeleza maafikiano ya mafuta kati ya Sudan mbili. 

Bi. Nkosazana Dlamin Zuma, Mkuu wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika amepongeza maamuzi na hatua zilizochukuliwa na Marais Omar al Bashir na Salva Kiir wa Sudan na Sudan Kusini katika mazungumzo waliyofanya huko Khartoum pamoja na matokeo ya kuridhisha ya mazungumzo hayo hasa uamuzi uliochukuliwa na serikali ya Sudan wa kuakhirisha kutekeleza uamuzi wake wa kuzuia usafirishaji mafuta ya Sudan Kusini kupitia mabomba ya nchini kwake. 

 Suala la kuendeleza mazungumzo kati ya Juba na Khartoum ili kutatua hitilafu zilizosalia kati ya pande mbili hizo khususan mivutano iliyopo katika kadhia ya eneo la Abyei, ni moja ya masuala yaliyopokewa vizuri na Umoja wa Afrika. 

Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini Jumanne iliyopita alifanya safari nchini Sudan lengo likiwa ni kufanya mazungumzo na mwenzake wa Sudan, Omar al Bashir, ili kutatua hitilafu zilizopo kati ya nchi mbili hizo. Safari hiyo ilijiri ikiwa zimesalia siku kadhaa tu hadi kumalizika muhula uliokuwa umeainishwa na Sudan wa kufunga mabomba yake ya kusafirishia mafuta ya Sudan Kusini.

Post a Comment

Previous Post Next Post