Mambo ya msingi kuzingatia katika uchanganuzi wa masoko

Masoko ni kitu muhimu sana katika biashara. Pasipokuwa na masoko ya bidhaa/huduma hakuna biashara. Kwa maneno mengine kukua kwa biashara kunatokana na uwepo wa masoko ya uhakika. Kwa lugha rahisi masoko ni wateja au watumiaji wa huduma au bidhaa husika na ili uweze kuwapata sharti utoe huduma/bidhaa zenye kukidhi mahitaji yao.
Kwa vile ustawi wa biashara hutegemea uhakika wa soko/masoko, ni muhimu kuzingatia masuala ya masoko katika ufanyaji wa biashara. Mjasiriamali anatakiwa kuwa na taarifa anuai juu ya soko la bidhaa/huduma anazozitoa.
Mjasiriamali anatakiwa kujua tabia za wateja wake. Wateja huwa wana tabia tofauti katika vipindi tofauti. Kujua tabia za wateja kutamsaidia mjasiriamali kupanga mipango yake yenye kutekelezeka kiurahisi. Pia, itamsaidia kutoa taarifa sahihi juu ya mchakato mzima wa masoko ya huduma/bidhaa zake.
Mjasiriamali anatakiwa kujua ushindani uliopo katika biashara anayoifanya. Ni nadra sana katika ulimwengu wa leo kukuta mjasiriamali anafanya biashara ambayo haina mshindani kabisa. Kwa maneno mengine, hata kama biashara yako ni ya kipekee lazima kutakuwa na mbadala wake.
Kutokana na hali hii, ni vizuri mjasiriamali akawajua washindani wake ili kuweza kukabiliana nao kwa mafanikio zaidi.
Mjasiriamali anatakiwa kujua jinsi alivyojipanga katika ulimwengu wa biashara. Hii ina maana kuwa mjasiriamali anatakiwa kujua jinsi atavyoingia sokoni kwa kuzingatia ubora alionao katika utoaji hudu. Vilevile anatakiwa kujua namna atakavyokabiliana na udhaifu alionao katika masoko, kwani hakuna biashara isiyokuwa na udhaifu hata kama ni mdogo kiasi gani.
Mjasiriamali anatakiwa ajue mbinu za kutafuta masoko. Mjasiriamali sharti awe na rasilimali watu yenye uwezo mkubwa wa kutafuta masoko. Kama nilivyosema hapo awali biashara ni masoko na masoko ndiyo wateja. Pasipo masoko hakuna biashara.
Kwa maana hiyo mjasiriamali anatakiwa kuwa mjanja wa kupenyeza kwenye masoko ambayo hakuwa nayo hapo awali. Hii itahitaji mbinu mbalimbali ili kuweza kuwashawishi wateja wakubaliane na kile unachokifanya.
Mjasiriamali anatakiwa kujua makadirio ya mauzo ya bidhaa zake. Kwa maneno mengine, mjasiriamali anatakaiwa kujua makadirio ya idadi ya wateja wake anaowahudumia katika vipindi tofauti.
Idadi ya wateja hutegemea dira au dhima ya biashara husika. Kwa mfano, mjasiriamali anaweza kuelekeza nguvu zake katika kuwahudumia watu fulani tu kama vile wanafunzi wa shule za msingi. Pia, anaweza kutengeneza bidhaa/kutoa huduma kwa ajili ya watu wote.
Mjasiriamali anatakiwa kujua ukubwa wa soko la huduma/bidhaa zake. Hili linafanyika kwa kuangalia wateja wa eneo (biashara) husika au kuangalia mauzo yaliyofanyika mwaka ulipita na jinsi soko linavyokua. Kwa maneno mengine, mjasiriamali anatakiwa kuangalia idadi ya wateja wake ili aweze kuzalisha bidhaa au kutoa huduma zinazokidhi mahitaji ya wateja wake.
Vilevile mjasiriamali anatakiwa kuelezea rasilimali alizonazo katika kukidhi mahitaji ya soko, namna ya kuingia sokoni na namna ya kupanua soko la bidhaa zake. Pia, anatakiwa kuelezea namna biashara itakavyoonekana siku za usoni, thamani ya bidhaa na namna biashara inavyoweza kukabiliana na upinzani sokoni.

Post a Comment

Previous Post Next Post