Serikali yakiri teknolojia ya BVR ‘kuchemsha’

Dar es Salaam. Serikali imekiri kuwapo kwa upungufu katika uandikishaji wa wapigakura kwa kutumia mfumo wa Teknolojia ya (BVR) wakati wa majaribio na kuitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) inayoratibu zoezi hilo kulirudia maeneo yote litakapoanza rasmi mapema mwakani.
Kauli hiyo ya Serikali inakuja siku moja kabla ya zoezi hilo kumalizika katika Jimbo la Kawe jijini Dar es Salaam, Kilombero mkoani Morogoro na Katavi linalotarajiwa kukamilika keshokutwa huku likikumbwa na matatizo ya mashine kushindwa kuhimili mazingira ya joto na changamoto mbalimbali.
Akiwa katika ziara ya kukagua zoezi hilo jana katika kituo cha Bunju A jijini humo, Waziri wa Nchi, Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi alibainisha mambo makuu manne yanayotakiwa kufanyiwa kazi haraka ili kulifanya zoezi hilo kuwa na uhalali. Alitaja mambo hayo kuwa ni pamoja na kuwepo kwa dawati maalumu la kuhakiki taarifa zinazotolewa na mhusika, ili kuepuka kuwaandikisha watu wasio na sifa.
“Kinachofanyika sasa mtu anapofika kujiandikisha, anaulizwa jina, umri na maswali kadhaa,” alisema Lukuvi akifafanua kuwa hata mtu akidanganya hakuna sehemu yoyote ya kubaini uogo huo. “Mtu hata akiwa siyo Mtanzania, hivi mnavyofanya anaweza kujiandikisha…, akiwa mtoto anaweza kujiandikisha hii ni hatari,” alisema akionya.
Aliongeza: “Pili, waandikishaji lazima wawe wengi kwani kama foleni ndiyo hii, hili ni tatizo, mtu anatakiwa kuja hapa mara moja anapata huduma na kuondoka, lakini pia muwe na ukakika wa mashine. Mnahitaji ngapi na katika maeneo yote mtatumia muda gani.”
Lukuvi aliitaka NEC kuwa makini na zoezi hilo akisema kwamba Serikali imewaamini na wakikosea makosa yote yatarudi serikalini na hasa kwa CCM jambo alilosema hawataki litokee.
“Mmesema ni zoezi la majaribio, lazima mtumie changamoto hizi kuboresha uandikishaji la sivyo tutakuja kupata lawama baadaye,” alisema Lukuvi.
Awali akisoma taarifa fupi ya zoezi hilo, Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Julius Malaba alisema katika majimbo hayo uandikishaji unaendelea vizuri na utakamilika kama ilivyopangwa.
Alisema Kawe uandikishaji ulianza Desemba 16 mwaka huu na utamalizika kesho, Kilombero Desemba 15 mwaka huu na unamalizika leo huku Milele mkoani Katavi Desemba 17 mwaka huu na utamalizika keshokutwa.
“Kuna changamoto mbalimbali zimejitokeza lakini zoezi linakwenda vizuri kama tulivyopanga na tunatarajia litakapoanza rasmi Januari mwakani au Februari mwanzo mwakani tutaweza kumaliza kwa wakati.”
“Lakini mashine hizi zimekuwa zinapata joto hivyo kushindwa kufanya kazi ambapo wataalamu wetu wamesema tutazingezea feni ili kuhimili joto...Mwanzo mashine zilikuwa haziwezi kupiga picha watu wenye macho mekundu lakini tumezifanyia marekebisho na tunaendelea vizuri,” alisema Malaba

Post a Comment

Previous Post Next Post