Vijana wataka kura ya maoni juu ya Muungano




Rashid Salum Adiy akizungumza na vijana wake nje ya viwanja vya baraza la wawakilishi Zanzibar akiwataka warudi nyumbani
KUNDI la Vijana zaidi ya 30 jana wamekusanyika katika viwanja vya Baraza la Wawakilishi Zanzibar wakitaka kuitishwa kwa kura ya maoni ya kuamua khatma ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao umefikisha miaka 48 sasa tokea kuunganishwa kwa nchi hizo mbili. Akiongoza vijana hao kiongozi wao, Rashid Salum Adiy alisema lengo la kukusanyika hapo ni kufikisha ujumbe kwa wawakilishi ambao pamoja na mambo mengine wanahitaji kuitishwa kura ya maoni itakayoamua mutastakbali wa nchi yao ambayo imevamiwa na Tanganyika kimabavu kwa miaka kadhaa tokea walipoungana kwa khiyari kati ya viongozi walioasisi Muungano huo Mwalimu Nyerere na Mzee Karume ambao wote ni marehemu kwa sasa.
Mara baada ya kuwasilia katika viwanja hivyo majira ya saa moja kamili asubuhi vijana hao walionekana wakiwa na mabango kadhaa yakiwa na maandishi ya kutaka kura ya maoni kwa kuwa Zanzibar ina sheria ya kuitisha kura ya maoni iwapo kutatokea jambo linalotaka kuamuliwa na wananchi wenyewe.
Kabla ya kuingia ndani ya viwanja hivyo askari dhamana waliokuwepo katika viwanja vya baraza hilo waliwazuwia vijana hao na kuwaambia wasiingie ndani na ndipo taarifa zikasambazwa kwa kuitwa jeshi la polisi kutoka makao makuu ya jeshi hilo wakitakiwa kuleta ulinzi mkali kudhibiti hali hiyo.
Sio muda mrefu vikosi vya ulinzi na usalama vilifika eneo la tukio vikiwa vimejitayarisha kimapambano lakini hali ghalfa ilibadilika baada ya uongozi wa jeshi hilo kutaka mazungumzo ya vijana hao na kuingia ndani kwa pamoja huku gari za polisi wa kuzuwia fujo FFU zikiwa zimekaa kusubiri amri ya mkuu wao wa jeshi hilo.
Hata hivyo hali haikuwa mbaya kama vile kama ilivyosambazwa ambapo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Azizi Juma Mohammed alipata wasaa wa kuongea na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kutoa katika kikao cha pamoja ambacho kiliwajumuisha viongozi wa vijana hao, jeshi la polisi pamoja na uongozi wa baraza la wawakilishi.
Kamanda Azizi alisema wamepokea taarifa kutoka vyanzo mbali mbali za tukio hilo na kwa mujibu wa umuhimu wa chombo hicho cha kutunga sheria kuhitaji utulivu waliona ni muhimu kufika uongozi wa jeshi hilo na kutaka kujua zaidi juu ya kadhia hiyo ambapo baada ya kukaa na uongozi waliona mambo ni tofauti na taarifa za awali.
“Mimi kama Kamanda mwenye dhamana ya mkoa huu kuhakikisha usalama unakuwepo muda wote nilipigiwa simu nikaambiwa kuna vijana wapatao 30 wamevamia katika viwanja vya baraza la wawkailishi wakilazimisha kuingia ndani lakini baada ya kufika hapa nikauta mambo ni tofauti na tumepata wasaa wa kuongea nao lakini kumbe walikuwa wanataka kuonana na mwakilishi wao wa jimbo la Kikwajuni ili kufikisha ujumbe wao kwa ambao wanasema muda mrefu wamewasiliana nao lakini amekuwa akiwazungusha” alisema Kamanda Azizi.
Naye kiongozi wa kundi hilo Rashid alisema awali walimuandikia barua Mwakilishi wao lakini kwa kuwa amekuwa akiwazungusha na hatoa majibu wameamua kumfuata katika kikao hicho cha baraza la wawakilishi lakini kwa kufuata taratibu zote zinzostahiki kwa kuwa lengo lao sio kufanya fujo bali ni kutekeleza kwa vitendo azma ya demokrasia na utawala wa sheria.
“Jana tulimletea Katibu wa Baraza la Wawakilishi barua na kumuelezea kwamba tunataka kumuona Mwakilishi wetu na kufikisha ujumbe wetu naye katibu alituruhusu kwamba tunaweza kufanya hivyo kwa hivyo tumefuata taratibu sio kama tumekuja hapa kihuni lakini tumekuja kwa kufuata sheria na haki yetu ya kikatiba inayoturuhusu kutoa maoni” alisema Kiongozi huyo.
Vijana hao ambao walionekana wakiwa watulivu sana walisimama kando ya barabara mbele ya jingo la baraza la wawakilishi wakiwa na mabango yao yanayosomeka kutaka kura ya maoni na kukataa mchakato wa katiba kwa kutoa maoni juu ya katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Akiulizwa maswali na waandishi wa habari waliotaka kujua kwamba kwa nini vijana hao wanaharakisha kutoa maoni yao wakati huu kabla ya kuja kwa tume iliyoteuliwa hivi karibu na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete ambayo itaratibu mchakato wa katiba ambao utaamua mustakabali wa nchi mbili, Rashid alisema.
“Hatutaki kutoa maoni katika tume ya Rais Kikwete tunachotaka kwanza ni kufuata taratibu za kuitisha kura ya maoni kwanza kujua kama tunataka au hatutaki Muungano na ikiwa hili tumeshindwa basi tutatizama suala jengine hilo tunajitokeaza katika kutoa maoni lakini kwanza tunatumia utaratibu wetu” alisema kiongozi huyo.
Wakiwasilisha barua ya hiyo kwa Mwakilishi wa Jimbo la KiKwajuni (CCM) Mahmoud Mohammed Mussa ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi walisema baada ya kumuona Mwakilishi wao hatoa majibu sahihi wameamua kuja katika viwanja hivyo na kuandika barua na kuwapa kila mjumbe wa baraza hilo ili kuona wanachotaka vijana hao.
“Mheshimiwa sisi ni wananchi wa Zanzibar hivi sasa tusiopungua laki tatu (300,000) tunaofikisha barua hii mbele yako kuwa ni sisitizo la tunachokihitaji kikatiba kwa mujibu wa katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 tolea la 201 kifungu Nam. 9 (1) (a) (b) kifungu Nm. 18 (1) (2) kifungu Nm. (23) (1) (2) (3) (4) kifungu Nam. 25 (1) (a) (b) kifungu Nam. 80A (1) (2) (a) (b)” nukuu ya barua hiyo.
Lengo la barua hiyo ni kupatiwa haki ya kikatiba dhidi ya suala la Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ili wananchi watoe ridhaa ya kisheria ikwapo Muungano uendelee kuwepo au kutokuwepo.
Katika barua hiyo vijana hao wamesema wao ndio waathirika wa kadhia hiyo ya Muungano na wanachukua hatua hiyo kueleza kwamba ebndapo mwakilishi huyo hatochukua hatua kuwasilisha hoja binafsi, kisheria ajue kwamba atalazimika kuwakosesha wananchi wake haki ya kikatiba na huenda akasababisha uvunjifu wa amani ndani ya Zanzibar.
“Mheshimiwa sisi ni wananchi tunapenda sana kuwepo kwa amani ndnai ya nchi yetu, leo tupo hapa kulinda demokrasia na utawala bora wa kisheria, sote tunaamini kwmaba utachukua hatua kuzingatia katiba sheria kulinda amani ya Zanzibar isitokee saa yoyote na hapali popote” ilisema barua hiyo yenye tarehe 11/04 2012.
Hatimae vijana hao walitakiwa na kiongozi wao kuondoka katika viwanja hivyo na walikubali kuondoka baada ya kutakiwa wafanye taratibu maalumu za kufikisha ujumbe huo kwa mara nyengine tena kwa wawakilishi wao, akizungumza na kuwapa matumaini vijana hao Rashid alisema ” Msiwe na huzuni ondokeni mwende nyumbani mkiwa na furaha kabisa bila ya matatizo maana tumezungumza na tumekubaliana kwamba mambo haya tuyafanye kwa utaratibu maalumu kwa hivyo msiwe na khofu mambo yote tutayapanga vizuri na yatakwenda kwa utaratibu mzuri hakuna kitakachoharibika” alisema kiongozi huyo.
Kwa habari zaidi ingia:-  
 zanzibaryetu

Post a Comment

Previous Post Next Post