CHADEMA yazidi kumkaba Mkuchika
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimemtaka Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika kuhakikisha sh
bilioni 40 zilizochotwa kwa ufisadi na Kampuni ya Kagoda zirudishwa na
kuwanufaisha wakulima, wakiwamo wa k
orosho katika mikoa ya Lindi na Mtwara.
orosho katika mikoa ya Lindi na Mtwara.
Pamoja na hilo, chama hicho kimemtaka Mkuchika kumwajibisha Diwani wa
Mkwedu, Juma Dadi, anayedaiwa na wanakijiji wa Tengulengu wilayani
Newala, mkoani Mtwara kutofika katika ofisi yake kwa zaidi ya mwaka
mmoja sasa na kuwafanya wananchi washindwe kujua sehemu ya kupeleka kero
zao.
Kauli hiyo ilitolewa mjini hapa juzi na Mkurugenzi wa Habari na Uenezi
wa CHADEMA, John Mnyika alipokuwa akifanya mikutano katika Kata ya
Makukwe na Mkwedu wilayani hapa na wananchi kumueleza kero mbalimbali,
ikiwamo kupeleka barua ya kumlalamikia diwani huyo kwa Mkurugenzi wa mji
wa Newala na mbunge wa jimbo hilo, Mkuchika na kwamba hakuna hatua
yoyote iliyochukuliwa hadi sasa.
Alisema udhaifu wa Mkuchika kusimamia majukumu yake haukuishia katika
jimbo analoliongoza, kwani alipokuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri
Mkuu (TAMISEMI), ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za
Serikali (CAG) zilionyesha ufisadi alioshindwa kuusimamia na
kusababaisha nchi kuingia katika hasara.
“Hivi kuna nini baina yao (Mkuchika na Rais Jakaya Kikwete)? Ripoti
zinaonyesha udhaifu mkubwa alionao juu ya usimamizi wa mali ya umma,
lakini rais anamsogeza karibu yake, tena kwenye wizara nyeti ambayo
TAKUKURU inakuwa chini yake. Mnadhani mali zetu zitaendelea kuwa
salama?” alihoji Mnyika.
Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo, alisema Rais Kikwete aliahidi
bungeni kuwa fedha hizo zitarudi na kuingizwa katika Benki ya Rasilimali
(TIB), hivyo ni wakati muafaka kwa Mkuchika kuhakikisha fedha hizo zipo
na kwamba kinyume cha hapo itaaminika kuwa amekwenda kuwalinda
mafisadi.
Aliongeza kuwa, ni wakati wa Mkuchika kuhakikisha ufisadi wa Newala na
maeneo mengine ambayo ripoti ya CAG imeainisha, unashughulikiwa na
kuwahakikishia wananchi kuwa uwepo wake hauhusiani na mafisadi.
Kuhusu diwani wa Mkwedu kutohudhuria katika mipango ya maendeleo ya
kata, Mnyika alisema ni aibu kwa Mkuchika kuzunguka maeneo mengine na
kuwakemea madiwani wasiofanya mikutano na wannchi huku akiwa na barua ya
wananchi wa Newala wanaomlalamikia kuhusu jambo hilo hilo.
Alisema ni wakati wa kuacha kulindana kwa maslahi ya kisiasa na badala
yake aonyeshe mfano kwa kumwajibisha Mkurugenzi wa Mji wa Newala pamoja
na diwani huyo anayelalamikiwa kwa kushindwa kusimamia majukumu yao.
Aidha, Mnyika alilisisitiza kuwa, Mkuchika anapaswa kujipima katika
nafasi yake hiyo kama inamfaa kwa kuwa wananchi wake wanamlalamikia kwa
kuonyesha mfano mbaya wa uongozi, kwa kuamua kuhamisha kituo cha afya na
makao ya tarafa kwenda kwenye maeneo yasiyopimwa bila kuwashirikisha
wananchi.
Chanzo:- Tanzania daima

Post a Comment