Madaktari watishia kugoma tena

Madaktari watishia kugoma tena 

Waitisha mkutano wao kesho Dar
MADAKTARI nchini wametishia kuitisha tena mgomo nchi nzima kushinikiza utekelezaji wa madai waliyoahidiwa na serikali Machi mwaka huu, Tanzania Daima limebaini.
Ili kutekeleza azma hiyo ambayo inaweza kuleta madhara makubwa kwa jamii kuliko ilivyokuwa wakati wa mgomo wa awali, Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), kimeitisha mkutano wa wanachama wake kesho, pamoja na mambo mengine kutoa taarifa ya utekelezaji ya maazimio ya serikali.
Kwa mujibu wa habari hizo, mkutano huo unatarajiwa kutoa maazimio ya nini kifanyike ambapo baadhi ya madaktari kutoka chama hicho walidokeza kuwa wanatarajia kuitisha mgomo mwingine nchi nzima.
Vyanzo vya habari kutoka Kamati ya Kudumu ya Bunge na Huduma za Jamii ambazo gazeti hili imezipata, zilisema kuwa tayari madaktari hao wamewasilisha dhamira yao ya kutaka kugoma kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii.
Ikumbukwe kwamba kamati hiyo iliacha shughuli zake bungeni kuja kuchunguza chanzo cha mgomo wa awali wa madaktari ambao ulisababisha vifo vya mamia ya Watanzania.
Hadi sasa serikali imeshindwa kutoa idadi kamili ya wananchi waliopoteza maisha kutokana na mgomo huo.
Habari zaidi zilidai kuwa hadi sasa serikali imetekeleza agizo moja tu la madaktari hao nalo ni kumsimamisha kazi Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii Blandina Nyoni na Mkuu Mkuu, Dk. Deo Mtasiwa.
Baadaye Rais Jakaya Kikwete aliamua kumtema Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Haji Mponda, na Naibu wake, Dk. Lucy Nkya, wakati alipofanya madailiko ya Baraza lake la Mawaziri hivi karibuni.
“Hadi leo serikali imeshughulikia madai ya uwajibishwaji na watendaji wa wizara. Waziri Mkuu Mizengo Pinda alimsimamisha kazi Katibu Mkuu na Mganga Mkuu. Baadaye Rais Kikwete alimtema Waziri wa Afya na Naibu wake. Madai mengine hayajatekelezwa hadi sasa,” kilisema chanzo chetu cha habari.
Hata hivyo serikali haikuweka muda wa ukomo wa utekelezaji wa maazimio hayo.
Akizungumza na gazeti hili jana, Rais wa MAT, Dk. Namala Mkopi, alisema chama hicho kinakutana na wanachama wake kesho kueleza utekelezaji wa ahadi za serikali.
“Siwezi kukuambia zaidi ila kweli tuna mkutano Jumamosi kutoa taarifa ya utekelezaji wa madai yetu. Nikikuambia zaidi nitakuwa naingilia kile tunachotaka kwenda kujadili, jambo ambalo sio zuri sana,” alisema Dk. Mkopi.
Februari mwaka huu, Waziri Mkuu, Pinda, alimsimamisha kazi Katibu Mkuu Nyoni na Mganga Mkuu, Dk. Mtasiwa, kutokana na tuhuma za kuingiza nchini robo tatu ya vifaa bandia vya vipimo vya ukimwi kutoka Korea Kusini.
Alitaja sababu zingine kuwa ni tuhuma za kuanzisha kampuni ya kusambaza nguo kwa madaktari na kuiingiza kinyemela kampuni ya kufanya usafi ndani ya Hospitali ya Taifa ya Muhimbil. Pinda alisema tuhuma hizo ni nzito zinazoidhalilisha serikali na kamwe haitakuwa busara kuzifumbia macho huku serikali ikiendelea kudhalilika.
Alisema malalamiko ya madaktari ni makubwa na kwamba yana msingi wa kusikilizwa na kusihi kamati iliyoundwa kuorodhesha kila kitu ili serikali iweze kuyafanyia kazi.
Madaktari hao walirejea kazini Machi 7 mwaka huu baada ya mazungumzo yao na Rais Kikwete Ikulu.
Katika mgomo huo wa siku 20, madaktari walitaka utekelezaji wa maslahi yao mbalimbali ikiwemo kuongezewa mishahara, kupatiwa nyumba, kuongezwa posho na pia kuwajibishwa kwa watendaji wa wizara ambao walikuwa ni Katibu Mkuu, Blandina Nyoni, Mganga Mkuu, Dk. Deo Mtasiwa na mawaziri wao.

Post a Comment

Previous Post Next Post