Tume ya Warioba yatoa msimamo

TUME ya mabadiliko ya Katiba imesema suala la Muungano litaguswa na iko tayari kupokea maoni yoyote kuhusu aina ya serikali ambayo wananchi wanaitaka.
Hayo yalisemwa jana na Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Joseph Warioba, ambaye alikuwa ameongozana na timu nzima inayounda tume hiyo wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam.
Jaji Warioba ambaye alikuwa akizungumzia juu ya tume hiyo kuanza mchakato wa awamu ya kwanza ya kukusanya na kuratibu maoni ya wananchi, alitoa kauli hiyo wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari juu ya suala la Muungano kuguswa.
Katika hilo, Jaji Warioba alisema tume yake ipo tayari kupokea maoni ya kila aina juu ya serikali ambayo wananchi wanaitaka kisha watafanya uchambuzi.
Kauli hiyo ya Jaji Warioba imekuja wakati ambapo kundi la Kiislamu la Wanauamsho likipinga Muungano na kutaka Zanzibar ijitenge.
Katika hali inayoonyesha kufahamu juu ya hilo, Jaji Warioba alisisitiza kuwa jazba zisitawale katika kukusanya maoni na kwamba wanajua matakwa ya wananchi, hawatayapindisha na watayatendea haki maoni yao.
Kuhusu uhalali wa tume hiyo visiwani Zanzibar, Jaji Warioba alisema kuwa chombo hicho kipo kwa mujibu wa sheria na kwamba kwa utaratibu uliopo sheria ambazo zinapitishwa zinawekwa mezani na Baraza la Wawakilishi linapatiwa taarifa.
“Sheria ya mabadiliko ya Katiba ilipitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano Novemba, na Januari Baraza la Wawakilishi likakutana na likapewa taarifa, hivyo tuna uhalali wote Zanzibar na maoni yanayokusanywa yatahusu pande zote,” alisema Jaji Warioba ambaye pia tume yake inakutana na waandishi wa habari leo visiwani Zanzibar.
Aidha, Tume ya Jaji Warioba ambayo imesema imeanza kuratibu maoni ya wananchi yanayotolewa kwa njia mbalimbali imeainisha maeneo makuu manne ambayo wameyataja kuwa ni moyo wa katiba, hivyo wangependa kupata maoni ya wananchi.
Eneo la kwanza ni misingi ya taifa, ambayo ndiyo nguzo ya utamaduni, nidhamu, maadili ya nchi na wananchi wake, na kwamba katiba ya sasa imetaja msingi kuwa ni uhuru, haki, udugu, amani, demokrasia na serikali kutofungamana na dini yoyote ingawa wananchi wana uhuru wa kuabudu, misingi hiyo ni amani na utulivu.
Kwa mujibu wa Jaji Warioba, baadhi ya watu wanasema misingi hii haitoshi au imetelekezwa, wengine wanasema inatosha hivyo tume ingependa kupata maoni yake.
Katika eneo la pili ni kuhusu mamlaka ya wananchi. Jaji Warioba alisema kuwa katiba ya sasa inaeleza kwamba msingi wa mamlaka yote ni msukumo mkubwa wa mchakato huu wa kupata katiba mpya na matakwa ya kuwawezesha wananchi kutunga katiba yao, lakini kuna watu wanasema mamlaka ya wananchi hayakufafanuliwa kama ilivyo kwa Serikali, Bunge, Mahakama, Tume mbalimbali za kikatiba na vyama vya siasa.
“Mamlaka ya wananchi hayakufafanuliwa wala hakuna utaratibu wa kuyatumia madaraka hayo wanasema wananchi wanatumiwa tu kisiasa wakati mamlaka yao yote yameporwa, wengine wanasema mamlaka hayo yapo isipokuwa wananchi wameyakasimu kwa taasisi mbalimbali. Tume ingependa kupata maoni ya wananchi kuhusu eneo hilo,” alisema.
Aidha, eneo la tatu ni malengo muhimu na misingi ya mwelekeo wa shughuli za serikali ambayo yameelezwa vizuri katika Ibara ya 9 ya katiba, baadhi yake ni kwamba utu na haki nyinginezo zote za binadamu zinaheshimiwa na kuthaminiwa.
“Kwamba shughuli za serikali zinatekelezwa kwa njia ambazo zitahakikisha kwamba utajiri wa taifa unaendelezwa, unahifadhiwa na unatumiwa kwa manufaa ya wananchi wote kwa jumla pia kuzuia mtu kumnyonya mwingine. Kwamba aina zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi, rushwa, uonevu au upendeleo zinaondolewa nchini.
“Kwamba matumizi ya utajiri wa taifa yanatilia mkazo maendeleo ya wananchi, hasa zaidi yanaelekezwa kwenye jitihada za kuondosha umaskini, ujinga na maradhi, kwamba shughuli za uchumi haziendeshwi kwa njia zinazoweza kusababisha ulimbikizaji wa mali au njia kuu za uchumi katika mamlaka ya watu wachache binafsi,” alisema.
Alisema malengo hayo ndiyo ndoto ya wananchi, kwa sababu yanajumuisha matumaini ya Watanzania kuhusu aina ya Tanzania wanayoitaka, mgawanyo wa madaraka kwa mamlaka mbalimbali za dola, unakusudiwa kuhakikisha kwamba malengo haya yanafikiwa.
Na kwamba baadhi ya watu wanasema malengo hayo yanatosha ila hayatekelezwi kwa ukamilifu na wengine wanasema hayatoshi katika zama hizi, hivyo wangependa kupata maoni ya wananchi kuhusu malengo hayo muhimu kwa taifa.
Eneo la nne, ambalo tume ingependa kupata maoni ya wananchi ni haki za binadamu na wajibu wa jamii ambapo wengine wanasema haki hizi hazitoshi huku wengine wakisema haki za mtu binafsi zinadhulumu haki za jamii na wengine wanasema haki za binadamu zinaminywa au hazitekelezwi kwa ukamilifu na zinavunjwa.
Mbali na hilo, Jaji Warioba alisema baada ya kuchukua muda kidogo kwa ajili ya maandalizi, tume itaanza mchakato wa kushauriana na wananchi ikiwa ni pamoja na kufanya safari za mikoani ambapo tume imejigawa katika makundi saba na kila kundi litafanya safari nne mikoani kati ya sasa na mwisho wa mwaka.
Alisema kila kundi litafanya kazi kwa wastani wa mwezi mmoja kila mkoa isipokuwa kwenye mikoa midogo kwa eneo ambapo tume itatumia muda mfupi.
Aliitaja mikoa minane ambayo wataanza nayo kuwa ni Dodoma, Kagera, Kusini Pemba, Kusini Unguja, Manyara, Pwani, Shinyanga na Tanga.
Jaji Warioba pia alisema kuwa watakuwa na mfumo wa kupokea maoni ya Watanzania kutoka pande zote za nchi na nje ya nchi kupitia simu, barua pepe, mitandao ya kijamii kama facebook, twitter, blogu na kwa njia ya posta.
Aidha, ametaka tume yao isiingiliwe kwa maana ya kufanya kazi kwa uhuru bila ya kuwapo kwa makundi yanayoishinikiza

Post a Comment

Previous Post Next Post