TUME ya mabadiliko ya Katiba imesema suala la Muungano litaguswa na
iko tayari kupokea maoni yoyote kuhusu aina ya serikali ambayo wananchi
wanaitaka.
Hayo yalisemwa jana na Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Joseph Warioba,
ambaye alikuwa ameongozana na timu nzima inayounda tume hiyo wakati
akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Karimjee jijini Dar
es Salaam.
Jaji Warioba ambaye alikuwa akizungumzia juu ya tume hiyo kuanza
mchakato wa awamu ya kwanza ya kukusanya na kuratibu maoni ya wananchi,
alitoa kauli hiyo wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari juu ya
suala la Muungano kuguswa.
Katika hilo, Jaji Warioba alisema tume yake ipo tayari kupokea maoni
ya kila aina juu ya serikali ambayo wananchi wanaitaka kisha watafanya
uchambuzi.
Kauli hiyo ya Jaji Warioba imekuja wakati ambapo kundi la Kiislamu la
Wanauamsho likipinga Muungano na kutaka Zanzibar ijitenge.
Katika hali inayoonyesha kufahamu juu ya hilo, Jaji Warioba
alisisitiza kuwa jazba zisitawale katika kukusanya maoni na kwamba
wanajua matakwa ya wananchi, hawatayapindisha na watayatendea haki maoni
yao.
Kuhusu uhalali wa tume hiyo visiwani Zanzibar, Jaji Warioba alisema
kuwa chombo hicho kipo kwa mujibu wa sheria na kwamba kwa utaratibu
uliopo sheria ambazo zinapitishwa zinawekwa mezani na Baraza la
Wawakilishi linapatiwa taarifa.
“Sheria ya mabadiliko ya Katiba ilipitishwa na Bunge la Jamhuri ya
Muungano Novemba, na Januari Baraza la Wawakilishi likakutana na
likapewa taarifa, hivyo tuna uhalali wote Zanzibar na maoni
yanayokusanywa yatahusu pande zote,” alisema Jaji Warioba ambaye pia
tume yake inakutana na waandishi wa habari leo visiwani Zanzibar.
Aidha, Tume ya Jaji Warioba ambayo imesema imeanza kuratibu maoni ya
wananchi yanayotolewa kwa njia mbalimbali imeainisha maeneo makuu manne
ambayo wameyataja kuwa ni moyo wa katiba, hivyo wangependa kupata maoni
ya wananchi.
Eneo la kwanza ni misingi ya taifa, ambayo ndiyo nguzo ya utamaduni,
nidhamu, maadili ya nchi na wananchi wake, na kwamba katiba ya sasa
imetaja msingi kuwa ni uhuru, haki, udugu, amani, demokrasia na serikali
kutofungamana na dini yoyote ingawa wananchi wana uhuru wa kuabudu,
misingi hiyo ni amani na utulivu.
Kwa mujibu wa Jaji Warioba, baadhi ya watu wanasema misingi hii
haitoshi au imetelekezwa, wengine wanasema inatosha hivyo tume ingependa
kupata maoni yake.
Katika eneo la pili ni kuhusu mamlaka ya wananchi. Jaji Warioba
alisema kuwa katiba ya sasa inaeleza kwamba msingi wa mamlaka yote ni
msukumo mkubwa wa mchakato huu wa kupata katiba mpya na matakwa ya
kuwawezesha wananchi kutunga katiba yao, lakini kuna watu wanasema
mamlaka ya wananchi hayakufafanuliwa kama ilivyo kwa Serikali, Bunge,
Mahakama, Tume mbalimbali za kikatiba na vyama vya siasa.
“Mamlaka ya wananchi hayakufafanuliwa wala hakuna utaratibu wa
kuyatumia madaraka hayo wanasema wananchi wanatumiwa tu kisiasa wakati
mamlaka yao yote yameporwa, wengine wanasema mamlaka hayo yapo isipokuwa
wananchi wameyakasimu kwa taasisi mbalimbali. Tume ingependa kupata
maoni ya wananchi kuhusu eneo hilo,” alisema.
Aidha, eneo la tatu ni malengo muhimu na misingi ya mwelekeo wa
shughuli za serikali ambayo yameelezwa vizuri katika Ibara ya 9 ya
katiba, baadhi yake ni kwamba utu na haki nyinginezo zote za binadamu
zinaheshimiwa na kuthaminiwa.
“Kwamba shughuli za serikali zinatekelezwa kwa njia ambazo
zitahakikisha kwamba utajiri wa taifa unaendelezwa, unahifadhiwa na
unatumiwa kwa manufaa ya wananchi wote kwa jumla pia kuzuia mtu
kumnyonya mwingine. Kwamba aina zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi,
rushwa, uonevu au upendeleo zinaondolewa nchini.
“Kwamba matumizi ya utajiri wa taifa yanatilia mkazo maendeleo ya
wananchi, hasa zaidi yanaelekezwa kwenye jitihada za kuondosha umaskini,
ujinga na maradhi, kwamba shughuli za uchumi haziendeshwi kwa njia
zinazoweza kusababisha ulimbikizaji wa mali au njia kuu za uchumi katika
mamlaka ya watu wachache binafsi,” alisema.
Alisema malengo hayo ndiyo ndoto ya wananchi, kwa sababu yanajumuisha
matumaini ya Watanzania kuhusu aina ya Tanzania wanayoitaka, mgawanyo wa
madaraka kwa mamlaka mbalimbali za dola, unakusudiwa kuhakikisha kwamba
malengo haya yanafikiwa.
Na kwamba baadhi ya watu wanasema malengo hayo yanatosha ila
hayatekelezwi kwa ukamilifu na wengine wanasema hayatoshi katika zama
hizi, hivyo wangependa kupata maoni ya wananchi kuhusu malengo hayo
muhimu kwa taifa.
Eneo la nne, ambalo tume ingependa kupata maoni ya wananchi ni haki za
binadamu na wajibu wa jamii ambapo wengine wanasema haki hizi hazitoshi
huku wengine wakisema haki za mtu binafsi zinadhulumu haki za jamii na
wengine wanasema haki za binadamu zinaminywa au hazitekelezwi kwa
ukamilifu na zinavunjwa.
Mbali na hilo, Jaji Warioba alisema baada ya kuchukua muda kidogo kwa
ajili ya maandalizi, tume itaanza mchakato wa kushauriana na wananchi
ikiwa ni pamoja na kufanya safari za mikoani ambapo tume imejigawa
katika makundi saba na kila kundi litafanya safari nne mikoani kati ya
sasa na mwisho wa mwaka.
Alisema kila kundi litafanya kazi kwa wastani wa mwezi mmoja kila mkoa
isipokuwa kwenye mikoa midogo kwa eneo ambapo tume itatumia muda mfupi.
Aliitaja mikoa minane ambayo wataanza nayo kuwa ni Dodoma, Kagera,
Kusini Pemba, Kusini Unguja, Manyara, Pwani, Shinyanga na Tanga.
Jaji Warioba pia alisema kuwa watakuwa na mfumo wa kupokea maoni ya
Watanzania kutoka pande zote za nchi na nje ya nchi kupitia simu, barua
pepe, mitandao ya kijamii kama facebook, twitter, blogu na kwa njia ya
posta.
Aidha, ametaka tume yao isiingiliwe kwa maana ya kufanya kazi kwa uhuru bila ya kuwapo kwa makundi yanayoishinikiza
Post a Comment