Serikali ya Syria yatangaza utayari wake wa kuketi mezani kwa mazungumzo kumaliza umwagaji wa damu

Waziri Mkuu wa Syria Wael al-Halaqi ambaye ametangaza utayari wa serikali yake kutumia mazungumzo kumaliza umwagaji wa damu
Na Nurdin Selemani Ramadhani

Waziri Mkuu wa Syria Wael al-Halaqi ametangaza utayari wa nchi yake kuketi kwenye meza ya mazungumzo kuangalia njia muafaka ambazo zinaweza zikamaliza miezi ishirini na moja ya umwagikaji wa damu unaoendelea kushuhudiwa katika Taifa hilo.



Waziri Mkuu Halaqi ametoa kauli hiyo wakati anahutubia Bunge na kusema hawapo tayari kuona masuala ya nchi hiyo yanaingiliwa na mataifa mengine ya kimagharibi kama ambavyo imeanza kushuhudiwa sasa.

Tamko la Waziri Mkuu wa Syria linakuja baada ya Mpatanishi wa Mgogoro huo Lakhdar Brahimi kuonesha nia yake ya kutumia mazungumzo katika kufikia suluhu ya machafuko yanayogharimu uhai wa watu wasio na hatia.

Brahimi amenukuliwa akisema iwapo pande zinazokinzana zitashindwa kuketi mezani ni wazi kabisa nchi ya Syria itaelekea kubana na itakuwa moja ya mataifa ambayo yameshindwa kwa sasa.

Halaqi ameeleza utayari wa serikali yake kutumia njia ya mazungumzo ikitafsiriwa kama jibu kwa Mpatanishi Brahimi aliyezuru Syria na kukutana na Rais Bashar Al Assad aliyesema yupo tayari kutumia njia yoyote kuleta suluhu lakini si kwa yeye kuondoka madarakani.

Waziri Mkuu wa Syria ameenda mbali zaidi na kusema wapo tayari wa maridhiano ambayo yanashirikisha nchi za kikanda pamoja na mataifa yanayoguswa na kile kinachoendelea lakini si yale ambayo yamejiegemeza kwa upinzani.

Halaqi akihutubia Bunge la Syria amesema mambo ya nchi hiyo yanastahili kupatiwa suluhu na wananchi wenyewe na si kutegemea mataifa ya nje ndiyo yalete suluhu ndani ya Taifa hilo.

Waziri Mkuu Halaqi ameyataka mataifa yote ambayo yanaingilia mgogoro wa nchi hiyo uliosababisha vifo vya watu wanaokadiriwa kufikia elfu arobaini na tano kuheshimu sheria za kimataifa kwenye hili.

Machafuko nchini Syria yalianza mwezi March mwaka 2011 kwa maandamano ya amani yakishinikiza kuondoka madarakani kwa Rais Assad lakini baadaye ghasia zikatawala na ndipo mapigano baina ya wapinzani na wafuasi wa Kiongozi huyo yakazuka.

Post a Comment

Previous Post Next Post