Kiwanda cha kwanza cha karatasi cha Somalia chafunguliwa Hargeisa

Mwajiriwa akifanya kazi katika Kiwanda kipya cha Karatasi AADCO huko Hargeisa. [Na Barkhad Dahir/Sabahi]
Na Barkhad Dahir, Hargeisa

Kiwanda ambacho huzalisha karatasi, maboksi na madaftari ya wanafunzi -- kiwanda cha kwanza kama hicho kufanyakazi nchini Somalia kwa miongo miwili -- kilifunguliwa huko Hargeisa mwishoni mwa wiki iliyopita.


Kuanzisha Kiwanda cha Karatasi cha AADCO kumekuwa kukishughulikiwa tangu mwaka 2009, mmiliki wake Aden Barado alisema katika sherehe za ufunguzi siku ya Jumamosi (tarehe 5 Januari).

"Ilichukua muda mkubwa kwa sababu tulikuwa katika nchi iliyoharibiwa," Barado alisema, na kuongeza kuwa ni shida kuanzisha kiwanda nchini Somalia ambako kuna msaada mdogo wa kurahisisha mchakato.

Kiwanda kilianza kujengwa mwezi Januari 2012 na kumalizika mwezi Disemba.

Kiwanda ina wafanyakazi 50, wakiwemo wanawake, na watu zaidi wataajiriwa hivi karibuni, kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Teknolojia Mohamud Abdullahi Ahmed, aliyesema kuwa baadhi ya wafanyakazi walipewa mafunzo huko China.

Kila saa 16, kiwanda huzalisha vitabu 70,000 ambavyo viko tayari kuuzwa sokoni, aliiambia Sabahi. Kiwanda hakiharibu mazingira kwani kinatumia mfumo unaoweka kikomo cha kelele na moshi ya kupita kiasi, alisema.

Waajiriwa hukusanya vitabu, karatasi za ofisini na maboksi ya ufungaji katika Kiwanda cha Karatasi cha AADCO. [Na Barkhad Dahir/Sabahi]

Hiki ni kiwanda cha kwanza cha aina yake kufunguliwa nchini Somalia tangu kuanguka kwa serikali kuu miongo miwili iliyopitaa, Meneja Mkuu Hassan Nur alisema. Gharama kamili za mradi zilikuwa dola milioni 5.

Katika awamu ya kwanza, kiwanda kinapangiwa kuchapisha vitabu vya mazoezi kwa wanafunzi, Nur aliiambia Sabahi. Katika miezi michache ya kwanza ya mwaka 2013, pia kitazalisha karatasi za ofisi zenye ukubwa wa A4, madaftari na maboksi ya kufungia vitu, alisema.


Katika juhudi za kuacha uagizaji wa vifaa vya kiwanda kutoka nje, kampuni hiyo mwishoni mwa mwaka huu itazalisha malighafi zake yenyewe za kutengenezea karatasi. "Tunaataka tujitosheleze kwa kuchapisha vifaa ambavyo uzalishaji wetu unahitaji, ambavyo kwa sasa tunanunua kutoka China," Nur alisema.

"Dhamiri yetu ni kuuza bidhaa zetu Somalia yote na nchi za jirani kama vile Djibouti na Ethiopia," alisema.

Kuimarika kwa hali za viwanda vya ndani

Kiwanda hiki kipya cha karatasi kitawasaidia watu katika eneo hili kuokoa pesa nyingi ambazo wanatumia katika kuagiza vitabu na karatasi za ofisini, alisema Mohamed Shukri Jama, mwenyekiti wa Chama cha Biashara, Viwanda na Kilimo.

"Kitaongeza upatikanaji wa kazi, ujuzi na uwekezaji, na hayo tunayakaribisha," alisema.

Kutoka mwaka 2000 hadi 2012, alisema kuwa shirika lake lilisajili viwanda 58 huko Somaliland ambavyo huzalisha vitu kadhaa, lakini ni 18 tu kati yao ambavyo kwa sasa vinafanya kazi. Alisema kuwa viwanda vilivyokufa kila kimoja kilipata baina ya dola milioni 1 na 5 kutoka wawekezaji binafsi, lakini vikashindwa kuwa vya faida na hatimaye kufungwa.

Alisema hali hasi, kama vile ukosefu wa msaada wa serikali, upatikanaji mikopo na msaada wa kiteknolojia, kunaweza kukwamisha uzalishaji wa ndani. Ili kusaidia uzalishaji wa ndani, kodi zinapaswa kuongezwa kwa vitu vinavyoagizwa kutoka nje ili watu wanunue bidhaa zilizozalishwa ndani, alisema.

Waziri wa Biashara, Viwanda na Utalii Abdirizak Khalif Ahmed, ambaye alihutubia sherehe za ufunguzi, alisema kuwa wizara yake inapanga kufanya hivyo. Ahmed alisema kuwa karibuni alipeleka kwa Wizara ya Fedha mpango wa kuongeza kodi kwa bidhaa za kuagizwa ambazo ni sawa na bidhaa zilizotengenezwa ndani ili kusaidia na kulinda utengenezaji.

Rais wa eneo la Somaliland Ahmed Mohamed Silanyo alikata utepe katika sherehe hizo, na kuahidi kuwa utawala wake imejitolea kukuza uwekezaji katika eneo hilo na kuongeza upatikanaji wa kazi kupitia msaada wa sera na ufundi.

Post a Comment

Previous Post Next Post