Meya CCM Bukoba ampuuza Mangula

MEYA wa Manispaa ya Bukoba, Dk. Anatory Amani (CCM), ameamua kukuza mgogoro ndani ya chama chake mjini Bukoba, na sasa amekiuka maagizo ya Makamu Mwenyekiti wao taifa, Philip Mangula.

Mangula ambaye alilazimika kufika mjini Bukoba mwezi uliopita ili kunusuru mtafaruku huo, aliagiza madiwani nane wa CCM waliokuwa wamesaini hati ya kumtaka Mkurugenzi wa Manispaa kuitisha kikao cha dharura cha kumjadili meya, waondoe tuhuma hizo na kuzipeleka kwenye chama ili zipatiwe ufumbuzi.

Hata hivyo, katika kujihami ili asing’olewe, Meya Amani kwa kushirikiana na Mkurugenzi wake, Hamis Kaputa walilazimika kuahirisha kikao cha Baraza la Madiwani kinyume na kanuni.

Kwa mujibu wa sheria namba 8 ya Serikali za Mitaa ya mwaka 1982 kifungu namba 7 (1), mkurugenzi anapaswa kumwandikia barua kila mjumbe kumweleza mahali na siku vikao vitafanyika na ajenda zitakazojadiliwa siku saba kabla ya kikao.

Madiwani hao hawakuwahi kujulishwa uwepo wa kikao hicho walichotaarifiwa na mkurugenzi kuwa kimesogezwa mbele kama kanuni hizo zinavyosema.

Kikao hicho kilikuwa cha kujadili utekelezaji wa shughuli za robo mwaka za fedha kati ya Oktoba hadi Desemba 30 mwaka jana, na kwa mujibu wa sheria kilipaswa kufanyika si zaidi ya Januari mwaka huu.

Katika barua hiyo yenye kumb. Na BMC/C.50/5/13, inayosomeka ‘Yah: Kusogezwa mbele ratiba ya vikao vya Baraza la Madiwani’, Kaputa hata hivyo haoneshi ni lini kikao hicho kitakaa.

Kaputa, katika barua hiyo anadai kuwa baraza haliwezi kufanyika kutokana na wakuu wa idara wengi kuwa safarini kuelekea jijini Dar es Salaam kwa ajili ya vikao vya bajeti 2013/2014.

Amani ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Kagondo, ameamua kwenda mbali zaidi huku akikiuka kanuni na sheria ambapo sasa amefungua pingamizi mahakamani ili kuzuia mkurugenzi asiitishe kikao chochote cha kujadili tuhuma zake kwa muda wote atakaokuwa katika wadhifa wake.

Bila kujali kuwa hatua hiyo ni kinyume na sheria namba 8 ya Serikali za Mitaa ya mwaka 1982 kifungu namba 5(1)(2)(c) ambacho kinasema kuwa mwamuzi wa mwisho katika migogoro yote ni Waziri wa Tamisemi, Amani aliamua kupiga hodi mahakamani.

Taarifa ambazo gazeti hili limezipata kutoka mjini Bukoba, zilisema kuwa Amani alifungua pingamizi hilo namba 1/2013 Januari 23 mwaka huu mchana, ikiwa ni saa chache baada ya madiwani hao nane kutii agizo la Mangula la kuwasilisha barua za kuondoa tuhuma zao kwa muda.

Kwamba, madiwani hao nane akiwemo mbunge wa Bukoba Mjini, Balozi Khamis Kagesheki, waliwasilisha barua zao kwa mkurugenzi ili kuondoa tuhuma zao kwa muda, asubuhi ya Januari 23 mwaka huu.

Kitendo hicho cha meya kimewaudhi madiwani hao na kutafsiriwa kama dharau kwa chama chake na kiongozi wao wa juu, Mangula, ambaye aliamua mgogoro huo umalizwe ndani ya vikao vya chama.

“Hata kama alikuwa na nia hiyo ya kwenda mahakamani, bado hakukidhi haja ya kanuni za halmashauri, kwani alipaswa kutoa kusudio la shtaka hilo kwa wote ndani ya siku 30, jambo ambalo hakufanya,” alisema mmoja wa madiwani hao.

Kufuatia hatua hiyo ya Amani, madiwani hao nane juzi waliwasilisha pingamizi lao mahakamani hapo kupinga zuio aliloweka meya na kesi hiyo ilihairishwa hadi Machi 21 mwaka huu.

Amani amekuwa kwenye mvutano na madiwani wake ambao tayari walikuwa wametia saini hati ya kumtaka mkurugenzi aitishe kikao cha dharura ili kumjadili na kumng’oa.

Mangula aliwataka madiwani hao kuunda kamati ya kushughulikia mgogoro huo chini ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Fabian Massawe.

Mgogoro huo umekipasua chama hicho mjini Bukona kutokana na Massawe, Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Mwenyekiti na Katibu wa CCM mkoa kudaiwa kumkingia kifua Amani.

Madiwani nane wa CCM akiwemo Mbunge wa Bukoba Mjini, Balozi Kagasheki na wengine wawili wa CUF walitia saini hati ya kumtaka mkurugenzi, aitishe kikao cha dharura ili kumng’oa meya huyo.

Balozi Kagasheki, ambaye pia ni Waziri wa Malialisili na Utalii, anaunga mkono msimamo wa CHADEMA, kupinga miradi ya uuzwaji wa viwanja zaidi ya 5,000 na ujenzi wa soko la kisasa kutokana na mikataba ya siri yenye harufu ya kifisadi aliyoisaini Amani kwa kificho.

Halmashauri hiyo ina madiwani 24, watatu wa CUF, wanne wa CHADEMA na 17 wa CCM. Ili kupitisha uamuzi huo wa kumuondoa meya, ni lazima robo tatu ya madiwani, yaani 16, wapige kura ya kuunga mkono hoja hiyo.

Madiwani waliosaini hati ya kutaka kuitishwa kikao cha kumng’oa meya huyo ni Naibu wake, Alexander Ngalinda (Kata ya Buhende) na Yusuf Ngaiza (Kashai) ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Manispaa ya Bukoba.

Wengine ni Richard Gasper (Miembeni), Dauda Kalumuna (Ijuganyondo), Deusdedit Mutakyahwa (Nyanga), Robert Katunzi (Hamugembe) na Mulubi Kichwabuta (Viti Maalumu)

Chanzo: Tanzania Daima

Post a Comment

Previous Post Next Post