Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu
ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Wajumbe wa
Halmashauri ya CCM Mkoa wa Kusini Pemba hawapo Pichani kwenye Ukumbi wa
Kiwanda cha Makonyo Wawi Chake chake Pemba akiwa katika ziara ya siku
mbili Kisiwani humo.
Kulia
yake ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kusini Pemba Nd. Abdulla Mohammed
Mshindo na Kushoto yake ni Katibu wa CCM Mkoa huo Shija Othman Shija.
Balozi Seif akizungumza na Wajumbe wa
Halmashauri ya CCM Mkoa Kaskzini Pemba kwenye ukumbi wa Vijana Mjini
Wete alipokuwa katika ziara ya siku mbili Kisiwani Pemba.
Kulia
ya Balozi ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa huo Nd. Mberwa Hamad Mberwa na
Kushoto yake ni Katibu wa CCM wa Mkoa huo Kassim Mabrouk.
Baadhi ya Wajumbe wa Halmashauri ya CCM
Mkoa wa Kaskazini Pemba wakifuatilia Hotuba ya Mjumbe wa Kamati Kuu ya
Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Iddi hayupo pichani
iliyokuwa ikifafanua mchakato wa katiba Mpya ya Tanzania unaopingwa na
upande wa upinzani.
Picha na Hassan Issa wa – OMPR – ZNZ
Na Othman Khamis Ame, Pemba
Mjumbe wa Kamati Kuu
ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi Balozi Seif Ali Iddi
alisema kauli aliyoitoa katika kikao cha Bunge kilichopita alipotakiwa
kuthibitisha ushirikishwaji wa Zanzibar katika mchakato juu ya
marekebisho ya sheria ya katiba mpya ya Jamuhuri ya mungano wa Tanzania
ilikuwa sahihi.
Balozi Seif alitoa
Kauli hiyo wakati alipokuwa akizungumza na wajumbe wa Halmashauri Kuu za
Chama cha Mapinduzi za Mikoa ya Kusini na Kaskazini Pemba kwa nyakati
tofauti wakati akiwa katika ziara ya siku mbili Kisiwani humo.
Kufuatia shutuma za
upande wa kampi ya upinzani dhidi yake za kudai kwamba amekuruputa
katika kutoa kauli hiyo Bungeni Balozi Seif akitoa ufafanuzi kwa mara ya
kwanza kufuatia tukio hilo ili kuwatanabahisha wanachama wa CCM na
wananchi kwa ujumla kuufahamu ukweli.
Balozi Seif alisema
inashangaza kuona kambi ya upinzani imeibua hoja ya kumtuhumu yeye
katika mabadiliko yaliyofanywa na Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria
wakisahau kwamba vipengele wanavyovilalamikia vilikuwemo ndani ya
rasimu ya awali ya mswaada huo ambao ulichanw a wakati ulipopelekwa kwa
wadau kujadiliwa.
Balozi Seif ambae pia
ni makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alifahamisha kwamba mamlaka ya
kutunga mswaada wa sheria inakuwa kazi ya Serikali ambayo hushirikisha
wataalamu na wadau wa sekta zote kazi ambayo inaishia wakati
unapowasilishwa katika Kamati ya Bunge.
Alifafanua kwamba
Sheria ya Bunge la Katiba ilifikishwa Zanzibar na kujadiliwa na kufanywa
uchambuzi kupitia wadau wa Sekta hiyo waliotoa nyongeza ya baadhi ya
vipengele ambavyo vyote vilikubaliwa na Kamati iliyosimamia mswaada huo.
“ Sheria ya mabadiliko
ya katiba imehusisha mambo manne makubwa nayo ni kuundwa kwa Kamati ya
kukusanya maoni, kutungwa kwa mabaraza ya Katiba ya Wilaya, Bunge la
Katiba na Kura ya maoni mambo ambayo yaliyokubalika na kuridhiwa na
pande zote mbili za Muungano. Sasa ugomvi uko wapi ?“. Aliuliza Balozi
Seif.
Akizungumzia
uimarishaji wa CCM Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmshauri Kuu ya Taifa
ya CCM Balozi Seif aliwakumbusha Viongozi na wanachama wa chama hicho
kisiwa Pemba kuhakikisha kwamba wanajenga chama ndani ya kipindi hichi
kinachoelekea kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Balozi Seif alisema
kazi ya Viongozi wa Chama hicho katika Mikoa na Wilaya ni kuhakikisha
kwamba program za ziara za mara kwa mara kuanzia shina, matawi na
majimbo zinatekelezwa ipasavyo ili kuamsha ari za wanachama hao.
Alisema ziara hizo ni
vyema zikaenda sambamba na uhamasishaji wa ulipaji wa ada za chama
utakosaidia kuwepuka ule mwanya unaoutumiwa na baadhi ya Wanachama
kutaka kuwalipia ada wanachama hasa katika kipindi cha uchaguzi kwa
lengo la kushawishi kuungwa mkono.
Alisisitiza kwamba
mwanachama anapoamua kuilipia ada kadi yake anajijengea nguvu za uwezo
wa kuwa huru unaompelekea kuepuka kuburuzwa na wanachama wengine wenye
tamaa ya uongozi.
“ Kazi iliyopo hivi
sasa ni kwa kila mwanachama kujipanga vyema katika kutafuta wanachama
ili kupata turufu na nguvu za kukipatia ushindi chama chetu wakati
utapowadia wa uchaguzi mkuu “. Aliongeza Balozi Seif.
Akizungumzia kuhusu
daftari la kudumu la wapiga kura Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya CCM
aliwataka Viongozi wa Mikoa hiyo kujipanga katika kushajiisha Vijana
kujiandikisha katika daftari hilo kwa vile muda wa kufanya hivyo bado
upo.
Balozi Seif
alitahadharisha kwamba bila ya kujiandikisha hakutakua na fursa ya
kupiga kura jambo ambalo linaweza kuisababishia mazingira magumu CCM
Katika uchaguzi mkuu huo ujao.
“ Bila ya
kujiandikisha hakuna fursa ya kupiga kura na bila ya kupiga kura maana
yake hakuna ushindi. Sasa siri ya yote hayo ni kwa wale vijana wapya
kujitokeza kwa wingi katika kujiandikisha kwenye daftari hilo la kudumu
la wapiga kura “. Alizidi kufafanua Balozi Seif.
Akiupongeza Uongozi wa
CCM wa Mikoa yote miwili ya Kusini na Kaskazini Pemba kwa utekelezaji
mzuri wa ilani ya CCM ya mwaka 2010 Balozi Seif alisema Viongozi hao
bado wanapaswa kuwaelimisha Vijana mfumo mzima wa kuendeleza maisha yao.
Alieleza kwa vile
mfumo wa ajira kwa vijana umo ndani ya ilani ya chama hicho Viongozi hao
wajitahidi katika kuwaandalia mazingira vijana hao katika kuanzisha
vikundi vya uzalishaji mali vitakavyosukuma mbele harakati zao za
kiuchumi na kupunguza ukali wa maisha.
Balozi Seif aliwataka
Viongozi na wanachama hao kuamini kwamba Serikali zote mbili zitaendela
kujitahidi katika kuona zinatoa msukumo wa uwezeshaji kwa vikundi
vitakavyoanzishwa ili viweze kujiendesha kiuchumi.
Naye Mke wa Mjumbe
huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi
Mama Asha Suleiman Iddi aliwatahadharisha Viongozi na wanachama hao
kuwepuka tabia ya kuendeleza makundi ndani ya chama hicho.
Mama Asha alisema
kwamba tabia hiyo ikiachiwa kuendelea inaweza kudhoofisha nguvu za
chama na hatimae kuleta athari katika harakati zake za kujipanga
kuelekea kwenye ushindi wa uchaguzi mwaka 2015.
Aliwakata kutembea
kufua mbele kuyatangaza maendeleo yaliyofikiwa katika utekelezaji wa
ilani ya chama hicho kupitia ndani ya Serikali zote mbili ile ya
Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Ile ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Mapema akitoa Taarifa
fupi ya utekelezaji wa kazi za chama ndani ya Mkoa wa Kusini Pemba
Katibu msaidizi wa CCM Mkoa huo Abdulla Yussuf Ali alisema yapo
mafanikio makubwa ndani ya mkoa huo yanayofanywa na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya CCM
Nd. Yussuf alisema
maeneo mengi ndani ya mkoa huo hivi sasa yanaendelea kupata huduma
muhimu za lazima kama afya, maji safi, Kilimo pamoja na Mawasiliano ya
usafiri wa Bara bara.
Alieleza kwamba shehia
nyingi ndani ya mkoa wa kusini Pemba zimebahatika kuwemo ndani ya mradi
mkubwa wa maji safi na salama ambao kumalizika kwake utasaidia
kuondosha tatizo kubwa la usumbufu wa huduma ya maji iliyokuwa
ikivikabili baadhi ya vijiji Mkoani humo.
Akizungumzia Siasa
Katibu Msaidizi huyo wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Kusini Pemba Nd. Ali
Yussuf alisema hali ya kisiasa hivi sasa imekuwa shuwari mkoani humo
tokea kuanza kwa mfumo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa ulioshirikisha
Vyama Vikuu viwili vilivyokuwa vikipingana vya CCM na CUF.
Post a Comment