
Abiria hao walikuwa wanasafiri na 
gari dogo aina ya Toyota Pick Up namba T 170 AKZ kwenda kuhani msiba 
uliotokea katika kijiji cha Kongei kilichoko Hedaru mkoani Kilimanjaro.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa 
Mkoa wa Kilimanjaro , Robert Boaz waliofariki ni Stella John (45), Salma
 Kizoka (33), Marry Senzige (49), Neema Daniel (52), Rehema George, 
(29), Sophia Mbike (51), Ritta Kallani (55) na Kallan Stephano (55), 
Kolina Mmasa (55) na Bahati Daudi (25),
Wengine ni Farida Kiondo (24) na 
Maria John (33) wote wakazi wa Kongei na kwamba miili yao imehifadhiwa 
katika hospitali ya Wilaya ya Same.
Boaz aliwataja majeruhi kuwa ni 
Zubeda Mrindoko (42),Mipa Chediel (29) na Zubeda Mlita (32) ambao 
wamelazwa katika hospitali ya rufaa ya KCMC kutokana na hali zao kuwa 
mbaya zaidi.
Wengine waliolazwa hospitalini Same ni Joyce Kandogwe (29), Subira Juma (22), Ramadhan Msangi (31) na Adinan Rajab (31).
Ajali hiyo ilitokea juzi saa 2:00 
usiku katika barabara kuu ya Tanga-Moshi, nje kidogo ya mji wa Hedaru, 
ikihusisha magari matatu ambayo ni Fuso (T 299 ANM) ikitokea Moshi 
kwenda Dar es Salaam na Scania (T 737 AKW) pamoja na tela lake namba T 
776 CCN ikitokea Dar es Salaam kwenda Moshi, kwa mujibu wa Mkuu wa 
Wilaya ya Same, Herman Kapufi.
Alisema watu hao walikuwa wamepanda 
gari la Diwani wa Kata ya Hedaru (CCM), Gerald Gwena aliyekuwa 
amewapakia waombolezaji hao kwenye pick-up yake ambayo iligongwa kwa 
nyuma na Fuso na baadaye gari hilo kuparamiwa kwa nyuma na Scania na 
kisha kusababisha vifo na majeruhi.
"Waombolezaji hawa walikuwa 
wanakwenda na diwani kuifariji familia ya marehemu mzee Mwanga ambaye 
mtoto wake wa kiume, Dismas Mwanga alifariki baada ya kusombwa na 
mafuriko”, alisema.
Alisema Dismas mwenye miaka tisa 
aliyekuwa anachunga kondoo milimani alifariki dunia juzi mchana baada ya
 kusombwa na mafuriko yaliyotokana na mvua kubwa zilizonyesha mfululizo.
Alisema hata, hivyo mpaka sasa haijafahamika iwapo mvua hizo zimesababisha vifo na hasara nyingine.
Kapufi alisema kamati yake ya ulinzi na usalama imekutana kwa dharura kujadili ajali hiyo na hatua ambazo wilaya hiyo itachukua.
Kamanda Boaz, alisema chanzo cha 
ajali hiyo ni kuzimika ghafla kwa  gari hilo mali ya diwani Gwena ambaye
 alikimbia baada ya ajali hiyo.
"Ajali hiyo ilitokea baada ya gari 
hilo kuzimika na Fuso iliyokuwa karibu kuteleza barabarani baada ya 
kujaribu kusimama ili isigongane na Pick Up iliyokuwa na waombolezaji, 
lakini lilivutwa na tope lililokuwa limejaa barabarani kisha kugonga 
kabla ya kupinduka na kuangukia upande wa kulia wa barabara ambako 
kulikuwa na lori la Scania.
Kamanda alisema watu 10 walikufa papo hapo , wawili walifia hospitalini na saba wamejeruhiwa.
Alisema juhudi za kuwasaka madereva  hao wa Fuso pamoja na diwani huyo zinaendelea.
Post a Comment