Kutokana na wakimbizi hao kuzoea utamaduni wa Serikali wa kutosimamia
utekelezaji wa uamuzi wake, wahamiaji wengi walikaidi agizo hilo la
Serikali kwa kudhani mamlaka husika zisingekuwa na uthubutu na dhamira
ya kuwarudisha makwao.PICHA|MAKTABA
Operesheni ya kuwakamata wahamiaji haramu
iliyofanyika nchi nzima mwishoni mwa mwaka jana ilionyesha mafanikio
makubwa. Baada ya miaka mingi ya wahamiaji kuishi nchini kinyume cha
sheria na kuifanya nchi yetu kuwa kama haina wenyewe, sasa raia wa nchi
mbalimbali waliokuwa wakidhani Tanzania haina wenyewe wamesoma maandishi
kwenye ukuta na kutambua kuwa, hakika Tanzania ina wenyewe, hivyo siyo
rahisi tena kuingia nchini kiholela.
Ukweli ni kwamba nchi yetu ililea tatizo hilo la
wahamiaji haramu. Ni siri iliyo wazi kwamba tatizo hilo halikuanza leo
wala jana, bali lilianza mara baada ya nchi yetu kupata uhuru mwaka 1961
ambapo sera ya nchi yetu ya kuwaona Waafrika wote kama ndugu,
ilipotoshwa ama ilitafsiriwa vibaya na baadhi ya Waafrika wenzetu, hivyo
kuingia nchini kutoka kila pembe ya Afrika pasipo kufuata taratibu.
Matokeo yake ni usalama wa taifa kuwekwa rehani kwa kuachia mipaka yetu
kuingiwa kirahisi kwa namna ambayo ni vigumu kuielezea.
Matokeo yake ni Watanzania wenzetu katika mikoa ya
mipakani kulazimishwa kuishi kama mateka au wakimbizi katika nchi yao.
Wahamiaji haramu pamoja na wengine wengi walioitwa wakimbizi kutokana na
vita ya wenyewe kwa wenyewe katika nchi zao, waliifanya Tanzania kama
kimbilio pekee katika pembe hii ya dunia. Muda si mrefu tulianza
kushuhudia kuzorota kwa hali ya usalama kutokana na kushamiri kwa
vitendo vya uhalifu kama mauaji, utekaji wa magari na kuzagaa kwa silaha
za kila aina. Uharibifu wa mazingira na vyanzo vya maji uliongezeka kwa
kasi ya kutisha na kuleta njaa na hata kusababisha baadhi ya watu
kupoteza maisha.
Wakati huo, tulimpongeza Rais Jakaya Kikwete
alipoamuru wahamiaji wote haramu warudi makwao kwa hiari, vinginevyo
ingeendeshwa operesheni maalumu ya kuwarudisha makwao kwa nguvu.
Wakimbizi wapatao 14,000 walirudi makwao kwa hiari, lakini wenzao wengi
walikaidi agizo hilo na kujibana kwa wenyeji na sehemu nyingine,
yakiwamo mapori.
Kutokana na wakimbizi hao kuzoea utamaduni wa
Serikali wa kutosimamia utekelezaji wa uamuzi wake, wahamiaji wengi
walikaidi agizo hilo la Serikali kwa kudhani mamlaka husika zisingekuwa
na uthubutu na dhamira ya kuwarudisha makwao. Hivyo, operesheni hiyo
ilipoanza walitaharuki na kukumbwa na mfadhaiko mkubwa. Ndiyo maana
operesheni hiyo iliwanasa wahamiaji wengi na wa kila aina, wakiwamo
wachungaji, walimu, wafanyabiashara na wafanyakazi kutoka nchi
mbalimbali barani Afrika waliokuwa katika ajira mbalimbali kinyume cha
sheria, ikiwa ni pamoja na walioajiriwa katika sehemu nyeti kama viwanja
vya ndege, ofisini na viwandani. Operesheni hiyo pia iliwatia mbaroni
Watanzania waliokamatwa wakiwa wamewaficha majumbani mwao wahamiaji hao
haramu.
Pamoja na kuipongeza Serikali kwa kuendesha
operesheni hiyo kwa ufanisi, tunasikitishwa na kushindwa kwake
kuhakikisha operesheni hiyo inakuwa endelevu. Kila kukicha tumeendelea
kushuhudia makundi ya wahamiaji haramu kutoka nchi za Ethiopia, Eritrea
na Somalia yakiingia nchini na pindi yanapokamatwa yanadai yalikuwa
yakielekea Afrika Kusini. Hii ina maana kwamba mipaka ya nchi yetu bado
inavuja kwa kiwango kikubwa, hasa kutokana na vitendo vya rushwa
miongoni mwa watumishi wa vikosi vya ulinzi na usalama. Ushauri wetu kwa
Serikali ni kwamba iendeleze operesheni hiyo na ishirikiane na serikali
za nchi hizo tulizozitaja hapo juu ili kwa pamoja zipate suluhisho la
kudumu.
- Mwananchi-
- Mwananchi-
Post a Comment