BEKI kiraka wa Yanga, Mbuyu Twite,
ametaja sababu moja ya yeye kusitisha mpango wake wa kusaini Azam FC na
kuongeza mkataba wa mwaka mmoja wa kuichezea Jangwani.
Awali mshambuliaji huyo alitajwa kuwepo katika orodha ya wachezaji ambao wangesaini
kuichezea Azam FC baada ya timu hiyo kumnasa mshambuliaji Mrundi, Didier Kavumbagu na kiungo Frank Domayo, kufuatia mikataba yao kumalizika Aprili 29, mwaka huu.
Akizungumza na Championi Jumatano, Twite alisema wanachama na mashabiki wa
timu hiyo ndiyo waliosababisha kuongeza mkataba kwa hofu ya kuvamiwa na kufanyiwa fujo ambazo zingeweza kuhatarisha maisha yake.
Twite alisema mashabiki wasingekubali yeye kuondoka kutokana na upendo wao
mkubwa walionao kwake, tofauti na Kavumbagu na Domayo.
“Kiukweli mwenyewe nilikaa na kufikiria kuwa ni bora nikabaki kuendelea kuichezea Yanga kutokana na hali ilivyokuwa baada ya kuondoka kwa Kavumbagu na Domayo.
“Kuna kipindi fedha inatakiwa iwekwe pembeni na kuangalia uhai wako,
kitendo cha kubaki Yanga kimeokoa uhai wangu, kwa jinsi ninavyowajua
mashabiki wa Yanga, ningesaini timu nyingine tofauti na timu yangu basi
fujo kubwa ingetokea ikiwezekana hata kuvamiwa nyumbani kwangu.
“Mashabiki wa Yanga siyo wavumilivu kabisa, pia maamuzi yangu hayo ya kubaki
Yanga, yamewawezesha viongozi kukaa kwa amani kwani ningeondoka mashabiki
wangewalaumu viongozi kwa kukubali wachezaji wao watatu kuondoka baada ya
Kavumbagu, Domayo na mimi,” alisema Twite aliyerejea kwao Congo.
CHANZO: CHAMPIONI JUMATANO
Post a Comment