Maalim Seif: Wanaotaka kuua Ukawa watakwama

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar na Katibu Mkuu wa chama cha Wananchi CUF Maalim Seif Sharif Hamad
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar na Katibu Mkuu wa chama cha Wananchi CUF Maalim Seif Sharif Hamad
Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Shariff Hamad amesema juhudi zinazofanywa kuusambaratisha Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), hazitafanikiwa.
Akihutubia mkutano wa hadhara wa CUF uliofanyika katika Kata ya Makurumla, Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, alisema kumekuwa na juhudi za hapa na pale za kutaka kuusambaratisha umoja huo na kusisitiza kuwa zitakwama.
“Umoja huu umeundwa kwa lengo la kutetea masilahi ya wananchi kupata Katiba wanayoitaka na wala siyo kwa masilahi binafsi… Nimefurahishwa na vyama vya upinzani kuunda umoja huu, kwani vinginevyo CCM ingewaburuza na kufanya uamuzi wanaoutaka kinyume na matakwa ya wananchi walio wengi,” alisema.
Alisema Sheria ya Mabadiliko ya Katiba inalitaka Bunge Maalumu la Katiba kujadili Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume hiyo na siyo kujadili rasimu nyingine yenye matakwa ya kundi maalumu.
Hamad alirejea kauli kwamba Ukawa wanaweza kurudi bungeni endapo tu Rais Jakaya Kikwete atawahakikishia kuwa rasimu itakayojadiliwa ni ile iliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba na iwapo itakwenda kinyume, wanaweza kutoka tena kwenye Bunge hilo.
Akizungumzia kuhusu Muundo wa Muungano, Katibu Mkuu huyo wa CUF alisema hakuna mbadala mwingine wa kumaliza kero za Muungano isipokuwa serikali tatu zitakazotoa mamlaka kwa serikali za nchi washirika.
Alisema hata Katiba ikitoa mamlaka kwa Zanzibar kuhusu kuweza kujiunga na mashirika ya Kimataifa yakiwamo; Afya (Who), Chakula (Fao) na Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), mamlaka hayo hayatokuwa na nguvu kwani mashirika hayo yanahitaji kufanya ushirikiano na nchi zenye mamlaka kamili (sovereign states). Pia mamlaka hayo ya kikatiba bila kuwa kamili yatakuwa ni kiini macho.
Awali, Naibu Katibu Mkuu wa CUF (Bara), Julius Mtatiro, alisema vyama vya upinzani vinavyounda Ukawa, vitaendelea kupigania Katiba inayotokana na maoni ya wananchi.
Chanzo: Mwananchi

Post a Comment

Previous Post Next Post