CHADEMA yamkaba CAG

 Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa CHADEMA, Anthony Komu
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimembana Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kikimtaka aweke bayana vyama vya siasa ambavyo havijakaguliwa hesabu zake na aeleze lini vitakaguliwa.
Shinikizo la CHADEMA linakuja siku chache baada ya Ofisi ya CAG, kushindwa kutaja chama cha siasa mbele ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (PAC), alichodai hakijakamilika kukaguliwa kutokana na kushindwa kufanya nacho vikao.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa CHADEMA, Anthony Komu, alisema CAG alitoa kauli bungeni kwamba si vyama vyote vimekaguliwa, kwamba kama sehemu ya jamii na chama kinachopigania utawala wa sheria, wanamtaka aweke taarifa bayana.
"Hii ni kwa sababu zilizotusukuma kupigania CAG kukagua vyama bado iko pale pale. Mwaka 2005, CCM ilitumia fedha za EPA katika kampeni zake, hatutaki utamaduni kama huo ujirudie tena kinyemela," alisema.
Alisisitiza kuwa ni imani yao kwamba Msajili wa Vyama vya Siasa, atachapisha ripoti za vyama vyote kama sheria inavyomtaka kwa ajili ya rejea ya umma unaolipa fedha hizo.
Akizungumzia ukaguzi wa hesabu za CHADEMA, Komu alisema kuwa CAG ameainisha kasoro kadhaa alizobaini na hivyo kutoa taarifa yake kwamba wanastahili kupewa hati yenye mashaka 'Qualified opinion' ambayo tayari wamepatiwa.(P.T)
Komu, alisema maeneo yote yaliyotajwa na CAG, yana maelezo ya kutosha na kuitaka ofisi hiyo kusimamia sheria na kuweka hadharani mahesabu ya vyama vingine kama ilivyofanya kwao.
Alisema kuwa, Oktoba 5 mwaka huu, CHADEMA kilipokea taarifa rasmi ya ukaguzi wa hesabu zinazoishia Juni 30 mwaka 2012, na ile ya Juni 30 mwaka 2013, iliyoeleza kuwa chama hicho kina akaunti zaidi ya 200 wakihusisha zile zinazoendeshwa na makao makuu, kanda, mikoa, wilaya, majimbo na hata ngazi za chini.
Alisema mashaka ya CAG, pia yamesimama katika salio la kufungia vitabu kutohusisha akaunti zote zenye jina la chama na kwamba, inawezekana akaunti hizo zilikuwa na fedha ambazo kinaweza kubadilisha kiasi kilichotajwa.
Kwa mujibu wa Komu, walimpatia CAG taarifa kuhusu akaunti hizo na ugumu wa kuweza kuzipata kwa kile alichosema masharti ya benki yanaeleza kuwa, wenye jukumu la kuendesha akaunti hizo ni viongozi wa ngazi husika.
Alisema kuwa CHADEMA kimepokea taarifa hiyo ya CAG na kuichukua kama sehemu muhimu ya kuboresha ujenzi wa chama kama taasisi ya kudumu na inayokua, na kwamba changamoto zote alizoziainisha watazifanyia kazi.
Komu, alifafanua kuwa kwa mujibu wa wabunge wao, taarifa zilizopo zinaonyesha mpaka juzi ni CCM pekee ambayo haijakaguliwa.
Jumanne wiki hii, Msaidizi wa CAG, Benja Majura, aliwasilisha taarifa ya ukaguzi wa mahesabu kwa mwaka 2012/13 mbele ya PAC, akisema kuwa kati ya vyama 21 ni 12 tu ndivyo viliweza kupeleka mahesabu yake na kukaguliwa.
Kwamba kati ya hivyo 12, kimoja wameshindwa kufikia hatua ya mwisho ya ukaguzi kutokana na kukosa muda wa kufanya vikao kwa ajili ya shughuli hiyo.
Pamoja na kubanwa akitaje chama hicho, Majura hakufanya hivyo, hatua iliyomfanya Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe, kuingilia kati akiwataka wajumbe wasubiri taarifa rasmi Oktoba 28 watakapokutana na msajili wa vyama.
Chanzo: http://www.freemedia.co.tz/daima/chadema-yamkaba-cag/

Post a Comment

Previous Post Next Post