HATIMA YA WASANII WA TANZANIA KATIKA KATIBA ILIYOPENDEKEZWA

Ndugu  Waandishi  wa  Habari.
 Yahusu Katiba Inayopendekezwa na Hatima ya Wasanii wa Tanzania
 Utangulizi.
 Fleva Inc Film Academy ni taasisi inayojihusisha na shughuli za ukuzaji wa  sanaa nchini hasa kwa  yale masuala yanayohusu tasnia ya filamu hapa Tanzania, ni taasisi inayofanya kazi na kutoa mafunzo ya uigizaji, uongozaji wa filamu au tamthilia,matangazo ya biashara , uandishi wa michezo  ya kuigiza ya jukwaani,uhariri wa filamu pamoja na utayarisahji wa Filamu kwa ujumla.
Fleva Inc Film Academy ni taasisi inayotambulika na mamlaka inayosimamia shughuli za sanaa na inapatikana  Manispaa ya Temeke hapa  Mjini  Dar es Salaam.
 Malengo ya Fleva Inc Film Academy.
Fleva Inc Film Academy ina malengo na madhumuni yafuatayo;
  • Kutoa Mafunzo yanayohusu tasnia ya filamu yenye ubora unaondana na mabadiliko ya ukuaji teknolojia duniani kote.hasa kwa fani za uigizaji michezo ya kuigiza na filamu, Kutoa mafunzo ya  kuhariri filamu, michezo ya kuigiza pamoja na tamthilia .
  • Kushirikiana na serikali,asasi zisizo za serikali,vikundi vya kijamii katika mambo mbalimbali yatayoweza kuleta mabadiliko ya kimaendeleo kwa Wasanii wa Tanzania na jamii kwa ujumla.
 Ndugu Waandishi kama tunavyofahamu tasnia ya filamu nchini imepitia hatua mbalimbali katika ukuaji wake ili kufikia maendeleo yanayoonekana sasa. Lakini jitihada hizi zimefanywa na kada mbalimbali za kisekta zikijumlisha serikali na taasisi zake pamoja na Wadau na Wabia  mbalimbali pamoja na Wasanii wenyewe wakishirikiana na taasisi zao.
 Lakini pamoja na changamoto nyingi zilizopatikana katika maendeleo ya tasnia ya filamu hapa nchini na sanaa nyinginezo kwa ujumla bado serikali yetu inayoongozwa na  Mheshimiwa  Rais Dkt Jakaya Mrisho Kikwete imejaribu kufanya maboresho na au utungaji wa sheria na kanuni kadhaa zitazowezesha kutoa miongozo iliyo  sahihi  katika kulinda , kutetea, kusimamia na ukuzaji wa tasnia za sanaa za ufundi, sanaa za maonesho, filamu na muziki, baadhi ya sheria hizo ni za hakimiliki na hakishiriki ya 1999 inayosimamia haki bunifu za Wasanii, sheria ya TRA ya mwaka 2014 inayosimamia kodi za mauzo ya kazi za filamu na muziki pamoja na sheria namba ya 4 ya mwaka 1976 inayosimamia michezo ya kuigiza ambazo kanuni zake zilizinduliwa  mwaka 2011 Mjini Musoma.  Pamoja na jitihada hizo kufanyika bado sekta ya sanaa haikupewa uzito unaostahili kwa sababu ilionekana si eneo ambalo linaweza kuwa na mchango katika pato la Taifa letu, yaani sanaa ilionekana ni kiburudisho kwa watu Fulani na umuhimu wake ulikuwa katika matukio na hafla maalumu.
 Ndugu Waandishi, nachukua fursa hii kuipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni Vijana na Michezo, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Fedha  na taasisi zao ambazo zimepewa majukumu ya  kusimamia kazi za Wasanii kwa namna moja au tofauti, zikiwemo,BASATA, COSOTA,TRA na  Bodi ya Filamu Tanzania na matunda ya majukumu yao yanaonekana.   
Pamoja na jitihada hizo za awali Naipongeza Serikali ya Mh Rais Dkt Mrisho Jakaya Kikwete kuanzisha mchakato wa kuandikwa kwa katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambapo katika mchakato huo makundi mbali mbali ya kijamii yalishirikishwa kuanzia hatua ya Mwanzo mpaka katika uundwaji wa Bunge Maalum la Katiba, Kutokana na hilo sisi tunaofanya kazi katika sekta ya Sanaa tuliwakilishwa na Ndg Paul Mtenda ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha Waongozaji wa Filamu na Michezo ya kuigiza Tanzania(TAFIDA).
 Ndugu Waandishi wa Habari mchakato wa Bunge Maalum la Katiba na majukumu yake yamekamilisha historia muhimu kwa Taifa la Tanzania ambapo tarehe 8/10/2014  katika Uwanja wa Jamhuri Dodoma  Mwenyekiti wa Bunge hilo maalumu Mh Samuel Sita  na kamati zake walimkabidhi rasmi  KATIBA INAYOPENDEKEZWA kwa Mh Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Jakaya Mrisho Kikwete.   
 Ndugu Waandishi, mimi ni mmoja kati ya Walioalikwa na Bunge kuhudhuria sherehe hizo nikiwa Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Wahariri wa Filamu na Michezo ya Kuigiza Tanzania (TAFEA) na Mkurugenzi Mkuu wa taasisi ya  Fleva Inc Film Academy na nikiwa Katibu Mstaafu wa Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF), nimeipitia Katiba inayopendekezwa na hasa vifungu vinavyohusu maslahi na haki za Wasanii Tanzania.
Kutokana na hilo nalipongeza Bunge Maalumu Katiba kwa kazi nzito walioifanya na hasa kuthamini na kuyapa umuhimu madai ya Wasanii wa Tanzania kwa kuingiza mambo ya msingi yanayohusu sekta ya Sanaa na hasa katika ulinzi wa haki bunifu za kazi za Wasanii, usimamizi na uendelezaji wa sekta ya Sanaa,utafiti  na taaluma kwa ujumla  ambazo zimeorodheswa katika Sura ya tano kifungu namba 59(1 -3) na 3(a) – (f) ukurasa 47 – 48.
 Ndugu Waandishi,Pamoja na mazuri yaliyoorodheshwa katika vifungu hivyo bado kuna changamoto kubwa inayoikabili sekta sanaa hasa muziki na filam, nalo ni tatizo la bei katika soko la filamu limekua si lenye kueleweka, katika hili naweza kusema kuwa thamani ya kazi za msanii wa filamu na muziki bado hazijatazamwa inavyostaahili na hasa tukizingatia kwamba tunafanya kazi kubwa katika mazingira magumu lakini bado tatizo la  bei ya zao letu haijatazamwa kwa kina.
 Kwa sababu kama Wavuvi, Wafugaji, na Wakulima watakua na mizania ya bei ya mazao yao kama ilivyotajwa katika Katiba Inayopendekezwa Sasa Sura 3 (13)(2)d ukurasa 10-11,  kwa nini pia katika zao la filamu pasiwepo na utaratibu wa bei elekezi kama ilivyo katika bidhaa za mafuta na sasa kwa wafugaji,Wakulima na wavuvi?. Lakini jambo hili halijachelewa kwa sababu zipo mamlaka zinazoweza kukaana Wadau wake ili kuliongelea na kulipatia ufumbuzi.
 Hivyo basi naziomba taasisi za BASATA, COSOTA, Bodi ya Filamu na Mashirikisho husika kulitazama kwa kina kama wanataka kuleta mapinduzi ya kiuchumi kwa Wasanii wenyewe ili wawezekulipia kodi kadhaa zinazowakabili.
 Mwisho napenda kuwashawishi Wasanii wa Tanzania kuchukua hatua madhubuti katika kutafuta fursa mbalimbali za kuiendeleza tasnia ya Filamu na Sanaa kwa ujumla lakini pia kuipitia katiba hii inayopendekezwa ili Waielewe na kujua yaliyomo ndani kuliko kupiga kelele ambazo majibu yake tayari yamepatiwa ufumbuzi.  
 Lakini pamoja na hayo ili kuleta tija na matokeo chanya ya Katiba hii INAYOPENDEKEZWA itapokuwa tayari na tunaiomba Serikali na hasa mamlaka zinazosimamia sekta za sanaa kuhakikisha inasimamia taratibu zote zinazoelekeza wajibu wa Wasanii na Watendaji wake ili kufanikisha malengo.
 Hongera Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Hongera Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba
 Nawatakia kazi njema
PAMOJA  TUILINDE  NA  KUIENDELEZA  TASNIA  YA  FIAMU TANZANIA.
WILSON R. MAKUBI
MKURUGENZI  MKUU
FLEVA INC FILM ACADEMY

Post a Comment

Previous Post Next Post