Al-Shabaab yawateka wakaazi, yawakata kichwa wanawake 2 huko Kudha

Al-Shabaab yawateka wakaazi, yawakata kichwa wanawake 2 huko Kudha

Na Fuad Ahmed, Mogadishu

Al-Shabaab waliwakata vichwa wanawake wawili na kuwateka zaidi ya raia 20 iliowatuhumu kwa kufanya ujasusi na kupinga mitazamo yao baada ya kukimata kwa muda kisiwa cha Kudha tarehe 8 Novemba.

Wanamgambo wa al-Shabaab walifanya msako nyumba hadi nyumba kisiwani Kudha, wakawakusanya wasichana na wavulana iliowatuhumu kuifanyia ujasusi Serikali ya Mpito ya Jubbaland. Pichani juu, wakaazi waliokimbia majumba yao Bulomarer wanaweza kurudi tarehe 31 Agosti baada ya wanajeshi wa Kikosi cha Umoja wa Afrika nchini Somalia kuukomboa mji huo kutoka kwa al-Shabaab. [Picha ya AMISOM / Tobin Jones]

"Ninaweza kuhakikisha kwamba wanawake hao wawili waliokatwa vichwa na al-Shabaab na zaidi ya raia 20 waliowateka hawakuhusika hata kidogo na tuhuma walizowatwisha za kuifanyia ujasusi Serikali ya Mpito ya Jubba (IJA)," alisema Kanali Urdan Kilas Gurase wa vikosi vya usalama vya IJA.

"Wanawake hao walikuwa na umri wa chini ya miaka 20 na kile kinachofanywa na hawa jamaa ni ushenzi," aliiambia Sabahi.

Al-Shabaab iliikimbia Kudha siku ya Jumatatu (tarehe 10 Novemba), siku tatu baada ya kukishambulia kisiwa hicho na kuwauwa kiasi cha wanajeshi 15 wa IJA.

Vikosi vya IJA sasa vimerudi kuchukua udhibiti wa kisiwa hicho, alisema Gurase.

Wanamgambo wa al-Shabaab walikuwa wamefanya msako wa nyumba kwa nyumba kwenye kisiwa hicho na kuwasafirisha raia iliowateka hadi kwenye maeneo yasiyojuilikana, kwa mujibu wa ripoti za vyombo vya habari vya Somalia.

Wakaazi wengi wa Kudha waliyakimbia maeneo ya mbali wakihofia ukatili wa al-Shabaab, alisema Gurase.


"[Wanamgambo hao] wanawadhuru wananchi kwa sababu wamekasirishwa na namna raia walivyofurahia hasara yao. Kile raia hawa wanachokitaka ni kuwa huru dhidi ya magaidi ya al-Shabaab," alisema.

Akizungumza kutoka Kismayu, kiongozi wa wazee wa Kudha, Omer Jeylani mwenye umri wa miaka 50 aliiambia Sabahi kwamba watu wanahofia hali zinazowakabili marafiki na familia zao walioko nyumbani.

"Kitu kinachotuhofisha sana ni pale tuliposikia wanawake wawili wasio hatia wamekatwa vichwa katikati ya Kudha na taarifa za zaidi ya watu 20 hazifahamiki baada ya al-Shabaab kuwachukua," alisema Jeylani. "Tunadhani nao pia wamewachinja."

Imekuwa ni shida kuwasiliana na watu wa Kudha kwani al-Shabaab imekata mitandao ya mawasiliano, alisema Jeylani.

"Ni vigumu kwetu kuwasiliana na jamaa zetu huko, na watu hawatwambia mengi tunapowapata (kwa simu)," alisema. "Wanahofia kwa sababu al-Shabaab wameingia kwa nguvu kwenye nyumba nyingi na kuwachukuwa watu ambao taarifa zao bado hazijuilikani."

Mkaazi wa Kismayu, Maryam Mumin, mwenye umri wa miaka 61, alisema binti yake na watoto sita wa binti huyo bado wako Kudha na kwamba anahofia ni vipi wataweza kuvuuka.

"Tunaishi kwenye siku za giza la kutokujua kama wazazi juu ya waliokwama kisiwani Kudha kwa sababu al-Shabaab wanalipiza kisasi kwa yeyote aliyevipokea vikosi vya serikali ya Jubba wakati wao (al-Shabaab) walipofukuzwa kutoka kisiwa hicho," aliiambia Sabahi.

"Mungu atulinde na al-Shabaab. Ni watu waovu," alisema.

Mumin alivitolea wito vikosi vya Umoja wa Afrika na IJA kuhakikisha kundi hilo "haliwezi tena kuyakamata maeneo waliyoyachukuwa kutoka kwa magaidi hao."

Wakati vikosi vya Somalia vikichukuwa udhibiti wa ngome za zamani za al-Shabaab, serikali ya shirikisho inawahimiza wananchi kuripoti shughuli zozote zinazotilika mashaka na wapiganaji wa al-Shabaab waliosalia kujisalimisha wenyewe na kutumia fursa ya programu ya msamaha iliyoongezwa muda hadi mwishoni mwa mwaka huu.

"Kuna njia ambazo kila mwanamme, mwanamke na mtoto anaweza kupambana na magaidi hawa pia; na hakuna hata moja kati ya njia hizo inayojumuisha kukamata bunduki," alisema Rais Hassan Sheikh Mohamud mwezi uliopita.

"Badala yake, tunaweza kushika simu na kuripoti vitendo vya kutilika mashaka na vya kihalifu serikalini," alisema. "Hilo linaweza kumaanisha kuwa tunamripoti jirani au binami yetu, kaka au dada yetu, hata mtoto wetu wa kiume au wa kike - lakini tutakuwa tunawaokoa, na pia kuokoa maisha ya Wasomali wasio hatia."

Post a Comment

Previous Post Next Post