Mombasa iko katika hali ya wasi wasi, uchunguzi unaendelea baada ya kuvamiwa kwa misikiti

Na Bosire Boniface, Garissa

Uvamizi wa hivi karibuni wa misikiti minne uliofanywa na vikosi vya usalama vya Kenya mjini Mombasa ikituhumiwa kuwa na uhusiano na al-Shabaab umeibua mchanganyiko wa majibu za umma juu ya kama operesheni hizo ni mkakati madhubuti wa kupambana na itikadi kali na vurugu.

Maafisa wa polisi wa Kenya wakilinda nje ya msikiti Swafaa katika wilaya ya Kisauni ya Mombasa kufuatia uvamizi wa msikiti huo tarehe 19 Novemba, 2014. [PICHA YA AFP / STRINGER]

Siku ya Jumatano (tarehe 19 Novemba), polisi walivamia misikiti ya Swafaa na Minaa, na kuwatia mbaroni watu 10 na kukamata maguruneti, risasi na mabomu ya petroli.

Siku mbili kabla, polisi walifanya uvamizi wa asubuhi mapema katika Masjid Shuhada (uliokuwa ukiitwa Masjid Musa) na Masjid Mujahideen (uliokuwa ukiitwa Masjid Sakina), wakaua mtu mmoja aliyekuwa akichomea maguruneti na kuwatia mbaroni zaidi ya watu 250.

Pia walikamata silaha - mabomu sita, bastola kadhaa, risasi, baruti, mapanga na visu - rekodi za kusikiliza na video juu ya mauaji ya mwanazuoni mwenye siasa kali Aboud Rogo Mohammed, beji za polisi wa Kenya, na bendera nyeusi inayohusishwa na al-Shabaab, alisema kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Mombasa Robert Kitur.

Afisa polisi wa Kenya akiteremsha bendera inayohusishwa na magaidi wa Kiislamu baada ya uvamizi wa misikiti miwili mjini Mombasa tarehe 17 Novemba. [PICHA YA AFP / STR]

"Operesheni sawia ya usalama ilidumu muda wa saa sita," alisema Kitur kuhusu uvamizi wa Jumatatu. "Ilikusudiwa kuepusha vitendo vya vurugu ambavyo vilikuwa vimepangwa kutoka misikiti hiyo miwili na mengine."


Polisi ilikuwa na intelijensia imara kuwa misikiti iliyovamiwa ilitumika kama maghala ya silaha na kama vituo vya mafunzo kwa shughuli za siasa kali na vurugu, alisema.

"Operesheni ilikuwa imepangwa kwa mikakati ya hali ya juu kwa karibu wiki moja ili kuhakikisha kwamba itawanasa wahalifu tuliokuwa tunawataka zaidi na kuzuia majeruhi kutoka pande zote mbili," aliiambia Sabahi.

Uchunguzi unaendelea
Polisi bado wanachunguza wafungwa na watatolewa wale ambao hawana hatia, Kitur alisema, akiongeza kuwa watu angalau 40 watafikishwa mahakamani hivi karibuni, ikiwa ni pamoja na 24 waliokamatwa katika Masjid Mujahideen na 16 walikamatwa katika Masjid Shuhada.

Ili kutetea operesheni hiyo, alisema kwamba wahalifu watasakwa popote pale watakapojificha.

"Kujificha katika maeneo matakatifu ni mbinu zinazotumiwa na wahalifu kuficha shughuli zao na kuanzisha migogoro kutoka kwa waumini dhidi ya polisi wakati wanapojaribu kuwatoa nje wahalifu," alisema. "Lakini sisi hatutaruhusu hilo na tutawafuata wahalifu popote."

Polisi pia wanachunguza nia na utambulisho wa kundi la vijana wenye silaha ambao walifanya ghasia siku ya Jumatatu usiku, na kuua watu wanne na kujeruhi wengine nane katika kitongoji cha Kisauni.

"Bado hatujui kama tukio hili linahusiana na kukamatwa kwa watu katika misikiti," alisema Kitur. "Waathirika waliochomwa visu ni Waislamu vile vile Wakristo na sisi bado tunafanya uchunguzi."

Kamishna wa Kaunti ya Mombasa Nelson Marwa alisema kuwa watu 110 walikamatwa wakati wa operesheni ya usalama ya Jumatano usiku katika misikiti Swafaa na Minaa, 36 wameshtakiwa mahakamani.

Aidha, ni mtu mmoja tu aliyekamatwa ndani ya msikiti, alisema.

"Wale waliokuwemo ndani ya misikiti waliparamia kuta na kukimbia wakati walipopata fununu ya vikosi vya usalama vinakaribia," Marwa aliiambia Sabahi. "Lakini tumeweza kukamata mabomu ya petroli, maguruneti na bendera nyeusi inayohusishwa na al-Shabaab."

Mtuhumiwa aliyekamatwa ndani ya msikiti Minaa alishtakiwa katika Mahakama ya Sheria ya Shanzu akiwa anamiliki panga kwa nia ya kutenda kosa na alipelekwa rumande chini ya ulinzi na dhamana ya shilingi 300,000 (dola 3,330), Marwa alisema.

Alisema kuwa 33 wengine walishtakiwa kwa uhalifu kuanzia uzururaji na kukosa vitambulisho, na wote walikuwa huru baada ya kulipa faini za fedha.

"Mtanzania na Mganda pia walishitakiwa mahakamani kwa kuwemo Kenya kinyume cha sheria," alisema. "Walitozwa faini ya shilingi 50,000 (dola 555) kila mmoja na watafukuzwa kurejeshwa nchini zao."

Misikiti bado imefungwa
Marwa alisema misikiti minne itabaki imefungwa hadi uchunguzi utakapokamilika, lakini kwamba vikosi vya usalama vitakuwa katika hali ya tahadhari kwa uwezekano wa matatizo mjini baada ya sala ya Ijumaa.

"Tupo na tahadhari kwa ukweli kwamba siku ya Ijumaa watu wachache huweza kuchochea wengine kushambulia maafisa wa usalama wanaolinda misikiti iliyofungwa," alisema. "Baada ya kusali katika misikiti mengine sala yao ya Ijumaa, waumini wanashauriwa kutokukaa karibu na misikiti iliyofungwa kwa sababu hatutavumilia vitendo yoyote vya vurugu."

Msemaji wa polisi wa Kenya Sipora Mboroki alisema polisi mjini Mombasa wamepewa maelekezo ya kutumia njia zote ziwezekanavyo ili kuhakikisha amani katika kutakuwa na maandamano ya vurugu baada ya operesheni za usalama.

"Tumekuwa wapole na kutumia diplomasia wakati tulipotembea katika operesheni," alisema juu ya uvamizi wa Jumatatu. "Tuliwapa wahalifu njia rahisi ya kufanya kwa kuacha vurugu zao na kusalimisha silaha walizokuwa nazo kwetu, lakini wao walikataa masharti yetu. Kwa faida ya umma mkubwa tulilazimika kuingia ndani."

Mboroki hakutaja idadi ya maafisa wa usalama walioshiriki katika operesheni, lakini alisema polisi watabaki macho na wataendelea kufuatilia misikiti. Wakati huo huo, wahalifu lazima wakatishwe tamaa ya kujificha au kuficha silaha ndani ya misikiti, alisema.

Mboroki aliita operesheni ya Jumatatu kuwa ya mafanikio na kuongeza, "Wajibu ni juu yetu sasa ili kuhakikisha mafanikio ya kuwashtaki wale tunaoamini kuwa walihusika katika uhalifu."

Nyumba za Ibada zinastahiki kuheshimiwa
Uvamizi wa misikiti umeibua hisia mchanganyiko kutoka kwa viongozi na wakazi wa eneo hilo.

Gavana wa Kaunti ya Mombasa Hassan Ali Joho alisema kuwa anaunga mkono vikosi vya usalama katika kupambana kwao dhidi ya vitendo vya uhalifu na ugaidi, ambavyo vinachafua sura na uchumi wa Kenya.

"Wakati majeshi yetu usalama yanapokwenda kusafisha uhalifu nchini mwetu, pia wanapaswa kuwa na ufahamu wa baadhi ya maeneo kama vile misikiti," aliiambia Sabahi, akiongeza kwamba vikosi vya usalama na waumini lazima wayachukulie maeneo ya ibada kwa heshima.

"Kama serikali ingeshauriana na viongozi [wenyeji], pengine tungeweza kupata njia nzuri ya kupata wahalifu bila ya kulazimika kuharamisha sehemu za kuabudia," alisema. "Moja ya njia mabazo [tumetumia huko nyuma] ni kuomba kwa uaminifu sio kuwaruhusu watu kwa kujua kutumia misikiti kuficha silaha."

"Dini yetu hairuhusu hata [kuleta] silaha msikitini," alisema, akiwaomba raia kushirikiana na serikali kuondoa kabisa uhalifu.

"Natumaini polisi watawahoji kwa kina ambao wamekamatwa kwa sababu baadhi yao hawana hatia," aliongeza. "Tunaamini kwamba mazungumzo bado yanaongoza katika [kupambana na] msimamo mkali na serikali inapaswa kutupatia muda wa kutosha."

Hisia mchanganyiko za umma
Vincent Akama, mwenye umri wa miaka 29, mlinzi binafsi wa usalama huko Kisauni, alisema uvamizi wa Jumatatu kwenye msikiti ulikuwa "jambo sahihi kufanyika".

"Ulikuwa ni uamuzi wa kipekee," aliiambia Sabahi. "Unaweza kushughulikiwa vizuri zaidi, lakini kwa sasa hakika ni uamuzi sahihi kwa sababu shughuli za msimamo mkali za misikiti miwili zimeandikwa vizuri na umma unaelewa."

Akama aliwaomba viongozi kufanya uchunguzi wa kina na wale wote waliokamatwa ili kuhakikisha wasio na hatia wanaachiwa haraka iwezekanavyo.

"Ninamfahamu jirani yangu Mkristo ambaye alikamatwa wakati wa operesheni," alisema. "Huuza chai na vitafunwa karibu na msikiti wa Musa. Kunaweza kuwa na waathirika wengi zaidi kama yeye ambao wamekamatwa katika tukio hilo."

Athman Hassan Bakari, mwenye umri wa miaka 34, mwendeshaji wa teksi huko Mombasa, alisema operesheni dhidi ya msikiti imeleta wasiwasi huko Mombasa.

"Kufunga msikiti haimaanishi kwamba kuna sheria inayowabana raia watakaoathirika," aliiambia Sabahi, akionyesha wasiwasi kuhusu uwajibikaji rasmi wa operesheni hiyo.

Lakini Amran Nassir Chiaba, mwenye umri wa miaka 39, mhudumu wa basi katika kituo cha mabasi cha Kongowea huko Mombasa, alisema uvamizi wa ghafla wa misikiti unasababisha itikadi kali kumalizika.

"Kitu ambacho serikali ilifanya ni kitu kizuri kukifanya," aliiambia Sabahi. "Uamuzi wa kuingia msikitini ulipaswa kufanyika mapema kuwaokoa vijana na Waislamu wengine kupewa hotuba zisizo za Kiislamu."

"Nimehudhuria mahubiri katika misikiti ya Musa na Sakina", alisema. "Kilichoropokwa kutoka katika mimbari, ni kama imamu alikuwa akitoa wito wa kutotii sheria za nchi, hakikubaliki."

"Wenye msimamo mkali walikuwa wakipinga serikali kwa muda mrefu na kama vikosi vya usalama havijafanya chochote kuhusiana na hilo, kungekuwa na utawala huru," alisema, akiongeza kwamba serikali inapaswa kutafakari kabla ya kufungua misikiti iliyoifunga.

"Tumekuwa tukikabiliana na vitisho vya ugaidi kwa muda mrefu na lolote linapaswa kufanyika."

Post a Comment

Previous Post Next Post