Wanawake, watoto hatarini mgodini Geita maisha wawatesa waishio

Geita. Baadhi ya wanawake katika machimbo ya Nyarugusu wilayani Geita wakiwa wabeba watoto wao mgongoni wameendelea kufanya kazi ya kuponda mawe bila kujali maradhi yanayoweza kuwapata watoto wao.
Inaelezwa kuwa hali hiyo inatokana na kupanda kwa gharama za maisha pamoja na umaskini uliokitihiri kwa baadhi ya familia zinazoishi jirani na machimbo ya wachimbaji wadogo wa dhahabu wilayani Geita.
Hatua hiyo inadaiwa kukiuka agizo la Serikali la kuzuia watoto kuonekana kwenye machimbo au kutumikishwa kwenye shughuli hizo.
Watoto wanaodaiwa kuathirika zaidi na shughuli hizo ni watoto wadogo wanaonyonyeshwa, ambao huambatana na wazazi wao wanaotegemea kipato cha familia kwa kuponda mawe katika machimbo hayo.
Mwananchi limeshuhudia baadhi ya wanawake katika machimbo ya Nyarugusu wilayani Geita wakifanya kazi hizo, huku wakiwa na watoto wao mgongoni bila kujali maradhi yanayoweza kuwapata watoto wao.
Wachimbaji wadogo hutumia zaidi maji yaliyochanganywa na kemikali ya zebaki kuosha mchanga wenye madini ya dhahabu ambayo hata hivyo hutiririka kwenda kwenye vyanzo vya maji.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Geita, Dk Adamu Sijaona alisema kwamba maradhi yanayoweza kutokea kutokana na kemikali hizo ni magonjwa ya ini.
‘’Kemikali hizi ni hatari sana kwa afya za watu, kwani kama mtu akivuta hewa inayotokana na kemikali hizi anaweza kupata ugonjwa wa ini ambalo linaweza kuharibika,’’ alisema Dk Sijaona.
Baadhi ya wanawake waliozungumza na gazeti hili kuhusu kujishughulisha na ujira huo na wakiwa na watoto wao mgongoni walisema wanafanya hivyo kutokana na kukosa wasaidizi wa kukaa na watoto nyumbani.
Pia, walisema umaskini unaozikabili familia zao unasababisha wao kwenda kutafuta kazi katika machimbo hayo ili kulisha familia zao na kujipatia fedha za kuwasomesha watoto wao.
‘’Sina mtu wa kumwachia mtoto...Watoto wangu wakubwa wameenda shule...kwa hiyo nitamuacha na nani sasa...Nikisema nikae nyumbani wanangu watakula nini, shughuli hizi zinatusaidia kusomesha watoto, tunakula kutokana na kazi hizi,’’ alisema Sophgia Thomas.
Walisema hulipwa Sh5,000 kwa mfuko mmoja na kwa siku mtu mmoja ana uwezo wa kuponda mifuko mitatu hadi mine ya mawe.
- Mwananchi

Post a Comment

Previous Post Next Post