Dar es Salaam. Ikiwa imesalia miezi kumi kabla
ya kufanyika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa, hadi
sasa majimbo sita yako wazi baada ya wabunge wanaoyaongoza kutangaza
kutogombea tena ubunge.
Ni wazi kuwa uamuzi wa wabunge hao, wengi wao
wakiwa wameamua kupumzika baada ya kushikilia viti hivyo kwa vipindi
zaidi ya viwili, utaibua ‘vita kali’, vikianzia ndani ya vyama wakati wa
kura za maoni na baadaye baina ya vyama wakati wa kuomba ridhaa kwa
wananchi.
Mbunge aliyetangaza kuachia jimbo hivi karibuni ni
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye amekuwa mbunge wa Katavi kwa vipindi
vitatu kuanzia mwaka 2000 akisema anakwenda kufanya kitu kingine.
“Wapo ambao hawatagombea sababu wanataka kuwania
urais. Wapo waliotangaza kutogombea sababu tu ya demokrasia na kutaka
kuwapisha wengine. Hilo ni jambo zuri,” alisema Profesa wa Chuo Kikuu
cha Ruaha, Gaudence Mpangala.
Profesa Mpangala alikumbushia pendekezo
lililokuwapo katika Rasimu ya Katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko
ya Katiba ambayo ilipendekeza kuwa mwisho wa kugombea uwe vipindi
vitatu.
“Pendekezo lile lilikuwa zuri ili kuwaondoa
wanaokaa madarakani zaidi ya miaka 50, ila wapo wanaotangaza kutogombea
kwa sababu tu za kisiasa,” alisema.
Vyama vya upinzani pia safari hii vitakuwa na kazi
ngumu ya kuteua wagombea baada ya kufikia makubaliano chini ya Umoja wa
Katiba ya Wananchi (Ukawa) kusimamisha mgombea mmoja kutoka miongoni
mwao katika ngazi zote kuanzia Serikali za Mitaa.
Vyama vilivyo chini ya mwavuli huo ni
NCCR-Mageuzi, Chadema, CUF na NLD, wakati chama kipya cha ACT - Tanzania
kilionyesha nguvu katika uchaguzi wa viongozi wa Serikali za Mitaa na
kama hakitamaliza mgogoro, kinaweza kuwa tishio wakati wa kutafuta kura
za wananchi utakapowadia.
Bernard Membe (Mtama)
“Unajua nimekuwa mbunge wenu kwa vipindi vitatu.
Hivi leo ninawaaga rasmi kuwa sitagombea tena nafasi hii ya ubunge,”
alisema Membe katika hafla ya Mwaka Mpya aliyoandaa nyumbani kwake
Januari, 2013.
Membe ni miongoni mwa makada wa CCM wanaotajwa
kutaka kuwania urais, ingawa amekuwa akieleza kuwa anasubiri
“kuoteshwa”. Iwapo atajitosa kugombea kuwania nafasi hiyo ya juu nchini,
jimbo hilo litabaki wazi na tayari linawaniwa na kiongozi mmoja wa juu
wa CCM.
- Mwananchi
- Mwananchi

Post a Comment