Takukuru, AG Kuchunguza Mauzo ya UDA

Ofisi ya Waziri Mkuu,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) imepeleka suala la mchakato wa uuzaji wa hisa za Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam katika Shirika la Usafiri Dar es Salaam(UDA) kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ili kuangalia mchakato mzima na mkanganyiko katika uuzwaji wa hisa hizo.

Pia wamemtaka mwanasheria mkuu wa serikali kuupitia mchakato  mzima kubaini kama hisa hizo zimeuzwa kwa kampuni ya  Simon Group au hazijauzwa.
 
Akijibu hoja za kamati ya Bunge ya Kudumu ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu mikataba yenye maslahi duni kwa halmashauri, Waziri wa Tamisemi, Hawa Ghasia (pichani hapo chini) alisema kupelekwa kwa suala hilo Takukuru pamoja na kwa mwanasheria mkuu wa serikali, ni kutaka kubaini kama hisa hizo ziliuzwa au la na kama ziliuzwa ilikuwa kihalali?
 
“Suala hili la UDA tumeamua kulipeleka kwa Mwanasheria Mkuu wa serikali na Takukuru kujua uhalali wa mchakato mzima wa uwekezaji na iwapo mauzo ya hisa za jiji yaliuzwa kihalali au la?,” alisema.
 
Awali, Mwenyekiti wa kamati hiyo ya LAAC, Rajab Mbaruk  Mohamed akiwasilisha taarifa yake ya hesabu za serikali za mitaa kwa mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, mwaka 2013,alitaka serikali kueleza ukweli kama hisa za jiji katika UDA zimeuzwa na kuhamishiwa kwa mwekezaji huyo au hazijauzwa.
 
Kamati hiyo ilisema endapo hisa hizo hazijauzwa, mchakato wa uuzaji wa hisa hizo utapaswa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zinazohusika.
 
Lakini wakati mijadala inaanza, Mbunge wa Ilala, Mussa Azzan  Zungu alipotaka kujadili suala hilo la UDA, Spika wa Bunge Anne Makinda alimzuia na kueleza kuwa hairuhusiwi  kulijadili kutokana na kuwa serikali walimpelekea taarifa ya kuwepo kwa kesi mbili zinazohusu UDA, hivyo kujadili watakuwa wameingilia uhuru wa Mahakama.
 
Uamuzi huo uliungwa mkono na Mwanasheria Mkuu wa serikali, George Masaju aliyesema hata yeye anayo mashauri matatu ya UDA mahakamani hivyo kwa utaratibu wa kuheshimu mihimili mingine ni vema suala la UDA lisijadiliwe.
 
Akizungumzia suala la Halmashauri ya Kinondoni kutonufaika na uwekezaji wa kampuni ya Oysterbay Villas, alisema ukwamishaji wa Kinondoni ulitokana na mkataba waliokubaliana lakini baada ya wiki moja Halmashauri ya Kinondoni itaanza kunufaika na uwekezaji huo ulioanza mwaka 2010.
 
Ghasia alisema ili kuondokana na mikataba yenye utata katika Halmashauri, imeamuliwa mikataba yote kupitia kwa Mwanasheria Mkuu wa serikali kujua kama mikataba hiyo ina manufaa hivyo malalamiko hayo hayatarudia.

Post a Comment

Previous Post Next Post