Dar es Salaam. Licha ya Wizara ya Habari,
Vijana, Utamaduni na Michezo kuahidi kuwasaidia wasani katika kudhibiti
wizi wa kazi zao, wadau wa sanaa nchini wamesema kuwa hawaridhishwi na
adhabu zinazochukuliwa na vyombo vyenye mamlaka ya kulinda na kutetea
haki za wasanii nchini.
Kutokana na kukithiri kwa wizi na uchakachuaji wa
kazi za wasanii, wadau hao wameitaka Serikali kuingilia kati kwa
kuwachukulia hatua zinazostahili kisheria wale wote watakaobainika
kuhujumu wasanii.
Mbali na kutoridhishwa na hatua zinazochukuliwa
pia wamewataka wasanii kufanya kazi zao kwa weledi na ubunifu kwa
kuingia darasani na kuacha tabia ya kulipua kwa lengo la kufanya
biashara.
“Sanaa ni kazi kama kazi nyingine, kazi ya msanii
inahitajika kuheshimiwa na kulindwa kwa mujibu wa sheria, kanuni na
taratibu zake na kwa wale wote watakaobainika kuwa wanaihujumu
wadhibitiwe na kuwajibishwa,” anasema Edwin Semzaba.
Semzaba ni Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam (UDSM), alieleza hayo wakati alipokuwa akitoa mafunzo kwa vijana
toka vikundi vitatu vya sanaa ya maigizo vya Malezi Youth Theatre,
Lumumba na Parapanda.
Anasema kwa hapa nchini bado mchango wa taaluma
katika sanaa ya maonyesho siyo nzuri, hasa ikizingatiwa kuwa watu wengi
wanaamini kuwa ni kipaji hata bila ya kuwa na elimu kitu ambacho siyo
kweli.
“Kuna tofauti kubwa kati ya mtu mwenye kipaji na
mtu aliyepata mafunzo, kwa kuwa aliyepata mafunzo ana wigo mpana wa
kufanya shughuli zake tena kwa ubora kuliko yule mwenye kipaji lakini
hana mafunzo,” alibainisha Semzaba.
Semzaba ambaye ni mwandishi wa vitabu, mwigizaji
wa Sanaa za Maigizo na Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi Vitabu nchini
(Uwavita) anasema sanaa ya maigizo ni ngumu na yenye gharama,
ikilinganishwa na sanaa za filamu licha ya kuwa inafanya vizuri.
Alisisitiza kuwa iwapo Serikali ingeweka sera
madhubuti ambayo itasaidia kulinda na kudhibiti wizi na uchakachuaji wa
kazi za wasanii nchini ingeweza kuwainua wao kiuchumi pamoja na pato la
taifa kama ilivyo kwenye nchi za wenzetu.
Lakini kutokana na kuwapo kwa ukosefu wa sera hiyo
madhubuti wasanii wamekuwa wakilia na kuingia hasara kutokana na kazi
zao kuibwa na kuchakachuliwa kila kukicha.
Semzaba ambaye ni mtunzi wa kitabu cha Ngoswe
Penzi Kitovu cha Uzembe, anasema ili mtu awe msanii mzuri katika tasnia
ya Sanaa ambayo inakuwa kwa kasi ni lazima apitie mafunzo ili aweze
kufanya kazi zake kwa ufanisi na weledi.
Anasema moja kati ya vitu vinavyosababisha kazi
nyingi za wasanii kushindwa kufanya vizuri katika soko la kimataifa, ni
kutokana na kufanya kazi zao chini ya kiwango kwa kujikita zaidi kwenye
biashara (masilahi zaidi) bila ya kuzingatia maudhui ili kazi iwe na
ubora unaohitajika.
Post a Comment