Wasomi: Mapinduzi Z’bar yawe mapinduzi ya fikra

Dar es Salaam. Wakati Wazanzibari leo wakiadhimisha miaka 51 ya Mapinduzi, wanasiasa na wasomi wametaka wananchi hao kufanya mikakati muhimu ya maendeleo na kuacha fikra mgando zinazoathiri maendeleo yao na nchi yao.
Wasomi na wanasiasa hao amesema Zanzibar imepiga hatua kubwa za maendeleo kiuchumi, kijamii na kisiasa lakini zinaweza kuendelezwa au kuharibiwa na Wazanzibari wenyewe iwapo wataendekeza tofauti zao za kihistoria zinazohusiana na mapinduzi.
Zanzibar inaadhimisha sherehe hizo huku kukiwa na matukio mawili makubwa ya kitaifa yanayoisubiri ikiwamo Kura ya Maoni ya Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, ambayo kwa namna moja au nyingine yanatajwa kuwa kipimo kikuu cha mwelekeo wa visiwa hivyo kisiasa.
Maadhimisho hayo yatakayoongozwa na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein kwenye Uwanja wa Amaan, yatahudhuriwa pia na Rais Jakaya Kikwete na viongozi wengine waandamizi wa Serikali ya Mapinduzi na ile ya Muungano.
Mhadhiri wa Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Zanzibar, Ali Uki alisema pamoja na kwamba Zanzibar imepiga hatua katika ujenzi wa miundombinu, huduma za kijamii, sheria, kilimo na maendeleo ya kisiasa kudumisha amani ndilo jambo la msingi.
“Suala la maendeleo hayo yamefikiwa kwa kiwango gani? Kila mtu anatazama kwa jicho na mtazamo wake,” alisema Uki na kuongeza kuwa kisiasa kuna mafanikio makubwa.
Alisema tangu kuanza mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, Zanzibar imekuwa ikijitahidi kuhimili misukosuko mbalimbali ya kisiasa ukiwamo upinzani mkali baina ya CCM na CUF uliosababisha kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK).
Alisema mbali na mafanikio hayo, kuna haja ya kufanya mkutano wa kitaifa wa kukubaliana kiwango cha sera za kufuatwa kutoka katika kila chama kwani licha ya kuwa na SUK hivi sasa, sera za CCM ndizo zinazofuatwa.
Iwapo itaonekana hili ni tatizo katika mwaka huu wenye changamoto za Kura ya Maoni na Uchaguzi Mkuu, Uki alisema kila chama kinaweza kukaa katika kamati zake na wataalamu na kuamua kuhusu kujumuisha sera zao ili kujenga mustakabali bora wa kisiasa Zanzibar.
“Watu waache fikra mgando kwamba hili ni suala langu na lile ni la yule, wafanye maendeleo kwa ushirikiano kwa kuwa mustakabali wa Zanzibar utatengenezwa na wao wenyewe,” alisema.
Mhadhiri katika Idara ya Sayansi ya Siasa ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Richard Mbunda alisema Mapinduzi ya Zanzibar yana mafanikio makubwa na yameendelea kuwapo bila mapinduzi mengine, jambo linaloonyesha yalikubalika vizuri.
Alisema mapinduzi yalifanikiwa kuendana na misukosuko ya kisiasa ukiwamo mfumo wa vyama vingi vya kisiasa ulioleta uga wa kisiasa usiotabirika wa nani atakuwa mshindi katika uchaguzi mkuu wowote.

Post a Comment

Previous Post Next Post