GPA
DISTINCTION MERIT CREDIT PASS FAIL
3.6 - 5.0 2.6 - 3.5 1.6 - 2.5 0.3 - 1.5 0.0 - 0.2
1. Mfumo wa Wastani wa Pointi (Grade Point Average - GPA)
Huonesha wastani wa pointi alizopata mtahiniwa katika masomo aliyofaulu katika mtihani wake.
GPA hutokana na masomo saba (07) aliyofaulu vizuri zaidi mtahiniwa katika Mtihani wa Kidato cha Nne na masomo matatu (3) ya tahasusi katika Mtihani wa Kidato cha Sita. Mtahiniwa aliyefanya masomo pungufu ya 07 kwa CSEE au pungufu ya 03 kwa ACSEE, atafaulu katika kiwango cha “Pass” endapo atapata angalau Gredi D katika masomo mawili au gredi C, B, B+ au A katika somo moja.
Uzito wa Gredi A= 5, B+ = 4, B = 3, C = 2, D = 1, E = 0.5 na F = 0.
Utaanza kutumika kupanga madaraja ya ufaulu katika Mtihani wa Kidato cha Nne (CSEE) 2014 na Kidato cha Sita (ACSEE) 2015.
2. Ukokotoaji wa GPA ya Mtahiniwa
Hufanyika kwa kuchukua jumla ya uzito wa gredi katika masomo saba (07) aliofanya vizuri kwa Mtihani wa Kidato cha Nne na matatu (3) ya tahasusi kwa Mtihani wa Kidato cha Sita na kugawanya kwa idadi ya masomo. Ukokotoaji huo huzingatia kanuni ifuatayo:
GPA =
Jumla ya Uzito wa gredi za masomo
------------------------------------------------
Idadi ya Masomo
Masomo yatakayotumika katika ukokotoaji wa GPA ya mtahiniwa ni yale ambayo amefaulu; yaani amepata Gredi A, B+, B, C au D.
3. Muundo wa Madaraja Kwa Kutumia Mfumo wa GPA
Katika mfumo wa Wastani wa Pointi (GPA) kutakuwa na madaraja manne ambayo ni Distinction, Merit, Credit na Pass.
Daraja la juu la ufaulu ni Distinction na la chini ni Pass kama ilivyoainishwa katika Jedwali lifuatalo:
Mfano; Mtihani wa Kidato cha Nne, mtahiniwa aliyepata ufaulu wa Civics (A), History (B+), Geography (B+), Kiswahili (B), English (C), Physics (C), Chemistry (C), Biology (C) na Mathematics (E) atakuwa na jumla ya pointi 22 kwenye masomo saba aliyofanya vizuri.
Idadi hiyo ya pointi ikigawanywa kwa idadi ya masomo saba (07), Mtahiniwa huyu atakuwa na Wastani wa Pointi (GPA) 3.1 na atatunukiwa daraja la Merit. Katika Mtihani wa Kidato cha Sita mtahiniwa aliyepata ufaulu wa Physics (A), Chemistry (B+), Biology (A), Basic Applied Mathematics (D) na General Study (A) atakuwa na jumla ya pointi 14 kwenye masomo ya tahasusi (PCB). Idadi hiyo ya pointi ikigawanywa kwa idadi ya masomo matatu (03), mtahiniwa atakuwa na Wastani wa Pointi (GPA) 4.7 na atatunukiwa daraja la Distinction.
4. Manufaa ya kutumia Mfumo wa Wastani wa Pointi (GPA);
Kuwa na mfumo wa kutunuku matokeo wa aina moja katika ngazi zote za mafunzo kuanzia Elimu ya Msingi hadi Elimu ya Juu;
Matokeo yaliyo katika mfumo wa wastani wa pointi kwenye cheti yatarahisisha kazi ya udahili wa watahiniwa unaofanywa na Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) katika ngazi za juu za mafunzo na Mfumo wa wastani wa pointi (GPA) ni rahisi kueleweka kwa wadau wa kada mbalimbali kwa sababu hutoa tafsiri yenye kuonesha mtahiniwa aliye na GPA kubwa ndiye aliye na matokeo mazuri kuliko aliye na GPA ndogo.
Maelezo zaidi kuhusu GPA yanapatikana katika tovuti ya Baraza la Mitihani (www.necta.go.tz).
Post a Comment