TRA yasisitiza usajili wa pikipiki ndani ya muda.....Usajili huo ni wa namba mpya zinazoanza na MC

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imewakumbusha wamiliki wa pikipiki maarufu kama bodaboda kuzifanyia usajili kwani watakaoshindwa kufanya hivyo ndani ya muda uliopangwa watachukuliwa hatua za kisheria.
 
“Tunawaomba na kutoa mwito kwa wamiliki wa pikipiki kutii sheria na kusajili namba mpya kabla Machi 31, 2015,” alisema Mkurugenzi wa Idara ya Huduma kwa Mlipa Kodi wa TRA Richard Kayombo wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana.
 
TRA ilitangaza kipindi cha miezi sita cha usajili wa namba mpya za pikipiki kuanzia Oktoba 1, mwaka jana hadi Machi 31, mwaka huu kama sehemu ya mpango mkakati wa TRA wa kuweka utaratibu mzuri wa kusimamia utoaji wa namba za magari na pikipiki kwa kuzitenganisha.
 
Utaratibu wa namba mpya pia unalenga kuzuia wimbi la uhalifu, unaochangiwa na bodaboda. “Mwisho wa muda wa usajili wa namba mpya ni Machi 31, mwaka huu.
 
TRA inatoa mwito kwa wamiliki wa bodaboda kusajili upya vyombo vyao kwa hiari na kupata namba mpya, ambazo zinaanza na MC 101 AAA. Pikipiki za biashara zinakuwa na pleti namba “nyeupe” wakati zile za kawaida zinakuwa na namba za “njano.”"
 
Akielezea kuhusu masuala mbalimbali yaliyoibuliwa wakati wa mchakato huo wa usajili wa namba mpya za pikipiki, Kayombo alisema gharama ya kubadilisha namba kutoka ya zamani kwenda mpya ni kiasi cha Sh 10,000 tu.
 
“Kwa wale ambao hawajalipia leseni za barabarani watatakiwa kulipia kwanza gharama hizo kabla ya kupata namba mpya. Na wale ambao hawajabadilisha majina ya umiliki wa pikipiki watatakiwa kufanya hivyo kabla ya kupata namba mpya.”
 
Kwa mujibu wa Kayombo, TRA imesambaza maofisa wake nchi nzima kuwahamasisha waendesha na wamiliki wa bodaboda kusajili pikipiki zao na kupata namba mpya. “Elimu hii imeenda hadi chini kwenye vituo vya bodaboda.
 
Tumefanya hivi katika mikoa yote ya Kodi katika jiji la Dar es Salaam (Ilala, Temeke na Kinondoni), Pwani, Morogoro, Ruvuma, Njombe, Iringa na Mbeya. Zoezi kama hili linaendelea Kanda ya Kati, Kanda ya Ziwa na Kanda ya Kaskazini,” alisema.
 
Mfumo mpya wa usajili wa pikipiki umekuja kama njia ya kuweka utaratibu mzuri wa namba za magari na pikipiki kwa kuzitenganisha, alisema Kayombo, na kuongeza kuwa mfumo huu pia utasaidia kupunguza matukio ya uhalifu nchini, yakihusisha unyang’anyaji wa kutumia silaha na wizi unaowahusisha waendesha pikipiki au bodaboda.
 
Pamoja na kuongeza pato la serikali, Kayombo aliuelezea mfumo huo mpya kama “mkakati madhubuti,” utakaolinda maslahi ya wamiliki wa pikipiki na kusaidia Tanzania na watu wake kuondokana na vitendo vya kihalifu vinavyohusisha pikipiki

Post a Comment

Previous Post Next Post