UCHAMBUZI WA POLEPOLE: Mambo 70 muhimu ya wananchi yaliyofutwa katika Katiba Inayopendekezwa

1. Kupunguzwa kwa madaraka ya rais

Wananchi walipendekeza madaraka makubwa ya Rais hasa ya uteuzi yapunguzwe na ziundwe taasisi za kikatiba za kumshauri rais kabla hajafanya teuzi. Wananchi walipendekeza pia baada ya rais kumteua kiongozi basi itabidi mteuliwa huyo Bunge limthibitishe.

Katiba Inayopendekezwa imeyafuta haya yote na imemwongezea Rais madaraka.

2. Kutenganisha mamlaka ya mihimili ya dola

Wananchi walipendekeza uhuru zaidi kwa Bunge na mamlaka zaidi kwa Bunge kuisimamia, kuiwajibisha na kuishauri Serikali. Pendekezo hili linaenda sambamba na kutenganisha Serikali na Bunge, hali ambayo iko sasa. Rasimu ya Warioba ililipa Bunge mamlaka zaidi kuisimamia Serikali na hata pale ambapo Bunge lingekataa bajeti au muswada mbaya wa Serikali mara kadhaa, rais asingeliweza kulivunja Bunge. Wananchi walisema sana mawaziri wasitokane na wabunge, ili wabunge wafanye kazi ya uwakilishi pekee na mawaziri watumie weledi wao kumsaidia rais kazi za Serikali.

Katiba Inayopendekezwa imefuta masharti haya.

3. Kumwajibisha mbunge

Rasimu ya Warioba iliwapa wapiga kura uwezo wa kuwawajibisha wabunge kwa  kupiga kura ya kutokuwa na imani nao wakati wowote kama wakienda kinyume na masilahi ya wananchi katika jimbo husika. Wananchi walijiuliza kama mbunge ni mtumishi wao, iweje hayuko katika kituo cha kazi kwa miezi kadhaa na wasiweze kumwajibisha mpaka miaka mitano? Katiba Inayopendekezwa imefuta masharti haya.

4. Vyanzo vya mapato vya kuaminika

Kuwapo kwa vyanzo vya mapato vya Serikali ya Jamhuri ya Muungano vitakavyogharimia mambo ya Muungano ambayo yamepunguzwa kutoka 22 hadi 7 lilikuwa pendekezo ambalo hata taasisi za Serikali zilipendekeza. Katiba Inayopendekezwa imerudisha mapato ya Muungano kama Katiba ya Mwaka 1977 na kwa kufanya hivyo tumerudi kwenye mgogoro wa msingi, kuchukua kodi tatu, ushuru wa forodha, ushuru wa bidhaa na mapato kutoka Zanzibar ni kuiua Zanzibar na kuifanya ishindwe kumudu matumizi yake ya ndani kwa mambo yasiyo ya Muungano na vivyo hivyo kwa Tanganyika.

5.Muundo wa shirikisho lenye mamlaka kamili

Kwa miaka nenda rudi tumekuwa na kitendawili cha ni muundo gani wa Muungano Jamhuri yetu inao. Kitendawili hiki kimeelezwa na wengi akiwamo Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere. Rasimu ya Warioba iliweka kwa mara ya kwanza Muundo Jamhuri ya Muungano kuwa ni wa Shirikisho lenye Mamlaka Kamili, nchi moja na yenye Serikali tatu. Kilichoongezwa ni na Rasimu ya Warioba ilikuwa Bunge na Serikali ya Tanganyika na siyo nchi ya Tanganyika kama ambavyo wengi wameaminishwa hivyo. Katiba Inayopendekezwa imerejesha na kuudhoofisha zaidi muundo wa Serikali mbili, kwa kuifanya Tanganyika au Tanzania Bara kuwa ndiyo Jamhuri ya Muungano na Zanzibar kuwa na mamlaka zaidi kwa mambo yasiyo ya Muungano ikiwamo kujiunga na jumuiya za kimataifa.
- Mwananchi

Post a Comment

Previous Post Next Post