Wanakijiji wamsimamisha Mkuu wa Mkoa wa Singida kwa kumtaka awaondolee kero ya Zahanati


Jengo la zahanati ya kijiji cha Lamba kata ya Mgori jimbo la Singida kaskazini ambalo inadaiwa limekamilika kujengwa zaidi ya miaka mitatu lakini hadi sasa halijaanza kutumika. Kitendo cha kushindwa kuanza kutumika kwa zahanati hiyo, inadaiwa kusababisha usumbufu wakazi wa kijiji cha Lamba kufuata huduma za afya kwenye kijiji cha Ngimu kilometa 15 au kijiji cha Mgori kilometa nane.(Picha na Nathaniel Limu).
Na Nathaniel Limu, Singida
WAKAZI wa kijiji cha Lamba kata ya Mgori jimbo la Singida kaskazini,juzi walizuia/walisimamisha msafara wa mkuu wa mkoa wa Singida,Dk.Parseko Kone kuendelea na safari ya kikazi, kama njia ya kumshinikiza ili aweze kusikiliza kilio chao juu ya huduma ya afya.
Wakazi hao wanaokadiriwa kuwa zaidi ya 30,walisimamisha msafara huo uliokuwa ukielekea katika hifadhi ya msitu wa Mgori kwa ajili ya kuadhimisha siku ya kitaifa ya utundikaji wa mizinga ngazi ya mkoa.
Baada ya msafara huo kusimama,wakazi hao walimweleza Dk.Kone kuwa toka zahanati ya kijiji chao imalizike kujengwa miaka mitatu iliyopita,hadi sasa haijaanza kutoa huduma za afya.
Walidai kitendo hicho kinaendelea kuchangia waendelee kupata usumbufu mkubwa wa kufuata huduma umbali wa kilometa nane katika kijiji cha Mgori au kilometa 15 hadi kijiji cha Ngimu.
“Mkuu wetu wa mkoa, hatujakusimamisha ili tukupotezee muda wa kuendelea na kazi zako za kuwahudumia wananchi, lengo letu ni kutaka utumie uwezo na nguvu zako kututafutia ufumbuzi wa kudumu kuhusu tatizo la kushindikana utoaji wa hudumu za afya kwa kipindi chote hichi cha miaka mitatu toka kumalizika kwa ujenzi wa zahanati.
Akadai waathirika wakubwa na kasoro hii,ni akina mama wajawazito”,alisema mkazi mmoja ambaye hakutaka jina lake litajwe humu.
Baada ya kumaliza kukagua jengo la zahanati na jengo linaloendelea la nyumba ya mtumishi wa zahanati hiyo ambalo lina miaka miwili toka lifikie hatua ya lenta,Dk.Kone aliwapongeza wakazi hao kwa ujasiri wao wa kusimamisha msafara na kuda kwamba wana haki ya msingi kusimamisha msafara wake.
Kwa kifupi mkuu huyo wa mkoa,alisema kwamba zahanati hiyo kushindwa kuanza kutoa huduma,ni udhaifu tu wa watendaji na kwamba kuanzia sasa atashughulikia mapema iwezekanavyo kilio chao.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Singida,bwana Mtefu,alijitetea kuwa muda mrefu halmashauri hiyo ina upungufu mkubwa wa rasilimali fedha kitendo ambcho kimekuwa kikwazo kikubwa kwa ustawi wa maendeleo ya halmashauri hiyo.
Habari nyingine kutoka kwa kiongozi mwingine wa ngazi ya juu katika halmahauri hiyo ambaye ametaka jina lake lisitajwe kwa madai kuwa sio msemaji wa halmashauri hiyo, amedai kuwa zahanati hiyo haijakamilika kwa aslimia mia moja kutokana na fedha karibu zote kuhamishiwa katika ujenzi wa maabara.

Post a Comment

Previous Post Next Post