Siku tatu za kishindo; watano kutangaza nia CCM.


mshindo 
Ni siku tatu za hekaheka na kujenga hoja za kujinadi kuanzia kesho wakati makada wa CCM watakapotangaza kwenye mikutano ya hadhara sababu zilizowasukumu kuomba kuteuliwa na chama hicho kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
CCM ipo kwenye wakati mgumu wa kutafuta mrithi wa Jakaya Kikwete katika nafasi ya urais na mwenyekiti wa chama hicho kikongwe nchini baada ya Rais huyo wa sasa kuongoza nchi kwa vipindi viwili vya miaka mitano kila kimoja na hivyo kulazimika kuondoka Ikulu kutokana na utashi wa kikatiba.
Kutokana na hilo, zaidi ya makada 20 wanatajwa kuwa na nia ya kuomba ridhaa ya CCM kugombea urais ili kuongoza Serikali ya Awamu ya Tano na watatakiwa kutangaza, kuchukua fomu na kuzirudisha ndani ya takribani siku 32 kabla ya Julai 2 ambayo ni siku ya mwisho iliyowekwa na chama hicho.
Wakati makada hao wa CCM wakijipanga kufanya shughuli kubwa za kutangaza nia ya kuomba wanachama wao wawape ridhaa ya kugombea urais, baadhi ya vyama vya upinzani vimeshatangaza ratiba zao lakini kinyang’anyiro kikubwa kitakuwa wakati vyama vilivyo chini ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) vitakapofanya mchujo wa kumpata mgombea atakayewakilisha umoja huo.
Kwa mujibu wa ratiba za makada wa CCM, kesho Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa atafanya mkutano wa hadhara kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha kutangaza rasmi nia ya kuomba kuteuliwa na CCM kugombea nafasi hiyo ya juu nchini.
Timu ya Lowassa, ambaye aliwaambia wahariri wa vyombo vya habari mwanzoni mwa wiki kuwa atatangaza nia Mei 30, imekuwa ikitoa matangazo mbalimbali kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii kutaarifu tukio hilo la kuanza rasmi kwa safari aliyoiita “ya matumaini”.
Katika mkutano wake na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari mapema wiki hii, Lowassa alihifadhi majibu ya baadhi ya maswali, akisema ni sehemu ya masuala atakayozungumzia kwenye hotuba yake ya kutangaza dhamira yake ya kuomba urais.
Tukio hilo litakalofanyika kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha litarushwa moja kwa moja na vyombo vinane vya habari kwa muda wa saa nne kuanzia saa 8:00 mchana hadi saa 11:00 jioni.
Habari ambazo Mwananchi imezipata kutoka vyanzo mbalimbali zinaeleza kuwa kumekuwa na maandalizi ya hali ya juu jijini Arusha kuelekea siku ya tukio hilo ikiwa ni pamoja na kuwasili kwa watu mbalimbali wanaomuunga mkono wakiwamo wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM.
Lowassa, ambaye ni mbunge wa Monduli, alikuwa waziri mkuu wa kwanza wa Serikali ya Awamu ya Nne, lakini akalazimika kujiuzulu mwaka 2008 baada ya Kamati ya Bunge kuibua kashfa ya kuingia mkataba wa ufuaji umeme wa dharura na kampuni iliyokuwa haina sifa ya Richmond RDC, uamuzi ambao anasema aliufanya ili kuiokoa nchi.
Lowassa pia aliwahi kuwania urais mwaka 1995, lakini CCM ikampa nafasi Benjamin Mkapa kuongoza Serikali ya Awamu ya Tatu.
Wakati Lowassa na timu yake wakiwa katika mikakati hiyo, makada wengine wa CCM ambao nao wanawania nafasi ya kuteuliwa na chama hicho, pia wamejipanga kutangaza nia zao kila mmoja kwa wakati wake huku wanne kati ya hao wakitoa taarifa kutangaza nia katika siku mbili tofauti Jumapili na Jumatatu katika maeneo tofauti.Kusoma zaidi bofya
Makada hao ni mbunge wa Afrika Mashariki, Makongoro Nyerere na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya watakaotangaza Juni Mosi (Jumatatu) kila mmoja katika eneo lake.
Taarifa iliyotolea na Makongoro inaeleza kuwa mtoto huyo wa Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Nyerere, atatangaza nia yake akiwa kijijini kwao Butiama mkoani Mara.
Makongoro, mbunge wa Afrika Mashariki na ambaye aliwahi kuongoza Jimbo la Arusha Mjini kwa tiketi ya NCCR-Mageuzi wakati wa uchaguzi mkuu wa kwanza tangu siasa za vyama vingi zirejeshwe, alidokeza nia yake mapema juma hili baada ya siku kadhaa za ubashiri kuwa anaandaliwa na CCM kumrithi JK kutokana na hali ya kambi za urais kutishia mustakabali wa chama hicho.
Kada mwingine ni Profesa Mwandosya, mbunge wa Rungwe Mashariki (CCM) ambaye ameeleza kuwa atatangaza nia yake Juni Mosi akiwa mkoani Mbeya na siku mbili baadaye atachukua fomu.
Mwandosya, ambaye amekuwa mbunge wa Rungwe kwa vipindi vitatu, aligombea nafasi hiyo mwaka 2005 na kushika nafasi ya tatu akiwa nyuma ya Kikwete na Dk Salim Ahmed Salim.
Wengine wawili ambao nao watatangaza nia siku moja katika maeneo tofauti ni Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira na Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba.
Wasira, ambaye ni mbunge wa Bunda, ameeleza katika ukurasa wake wa Facebook kuwa atatangaza nia yake akiwa mkoani Mwanza keshokutwa (Mei 31) huku Mwigulu akitangazia nia yake mkoani Dodoma siku hiyohiyo.
Wasira, mbunge wa Bunda na mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, amekuwa mbunge na waziri kuanzia mwaka 1970 na ndiye mwanasiasa mkongwe kuliko wote wanaotajwa kuwania urais kwa tiketi ya chama hicho.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, Nchemba, ambaye ni mbunge wa Iramba Mashariki, alitangaza kujivua nafasi yake ya naibu katibu mkuu wa CCM-Bara ili ajikite zaidi kwenye harakati za kuwania urais.
Naibu waziri huyo wa fedha anatumikia kipindi chake cha kwanza bungeni.
Wakati makada hao wakijipanga kuwaeleza wananchi sababu zilizowasukuma kuomba kushika nafasi hiyo ya juu kisiasa nchini, makada wengine wa CCM bado hawajatangaza ratiba zao, huku baadhi wakiwa wameshatangaza nia na kwa sasa wanasubiri kuchukua fomu na baadaye kuzunguka mikoani kutafuta wadhamini.
Waziri Mkuu Mizengo Pinda, pamoja na waziri mkuu wa zamani, Frederick Sumaye, na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ni miongoni mwa makada ambao hawajaweka bayana ratiba zao, ingawa Membe ameweka bayana kuwa atafanya hivyo kijijini kwake Rondo mkoani Lindi.
Wengine ni mbunge wa Sengerema (CCM), William Ngeleja, Mbunge wa Songea(CCM), Dk Emannuel Nchimbi, Waziri Mkuu wa zamani, Frederick Sumaye na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli.
Ambao tayari walishatangaza nia zao za kuomba kuteuliwa na CCM ni Pinda, Lazaro Nyalandu, ambaye ni Waziri wa Maliasili na Utalii, Januari Makamba (Sayansi na Teknolojia), na Dk Hamisi Kingwangalla (mbunge wa Nzega).
Chanzo:Mwananchi

Post a Comment

Previous Post Next Post