Wahandisi, Tanroads waanza kulifanyia tathmini jiji la Dar

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki ameteua timu ya wahandisi kutoka Wilaya za Temeke, Ilala na Kinondoni kwa kushirikiana na Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), kufanya tathmini ya uharibifu wa miundombinu kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha pamoja na kujua gharama stahiki kulirudisha jiji katika hali yake.
Akizungumza jijini jana, Sadiki alisema kuwa baada ya kufanya tathmini hiyo, itatoa mwanga ni kiasi gani kinahitajika ili kurudisha miundombinu iliyoharibika katika hali yake ya kawaida.
“Siwezi nikasema leo (jana) kuwa miundombinu iliyoharibikia itafanyiwa matengenezo kwa kiasi hiki au kile, subirini. Nimeitisha wahandisi na wanaendelea na kazi,” alisema Sadiki na kuongeza kuwa;
“ Hiki kitu siyo cha kukurupuka kina taratibu na sheria zake inabidi zifuatwe, hayo yote yakishakamilika wananchi wa mkoa huu watafahamishwa lini ukarabati unaanza na kwa kiasi gani, kwani hapa hakuna siri,”.
Akizungumza na gazeti hili juzi ofisini kwake, mkuu huyo wa mkoa alisema mvua zimelivuruga jiji na kusababisha uharibifu mkubwa wa miundombinu.
Sadiki aliyasema hayo baada ya kumalizika kikao cha kutathmini mafuriko hayo kilichohusisha wakuu wa wilaya za mkoa huo, Ilala, Kinondoni na Temeke, Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa na Kitengo cha Maafa Mkoa.
Sadiki aliliambia gazeti hili kuwa, jiji haliko kwenye hali nzuri kwani barabara zaidi ya 20 zimeharibiwa, madaraja kadhaa, makaravati yamesombwa na maji na kusababisha kukatika kwa mawasiliano katika baadhi ya maeneo.
Aliyataja maeneo yaliyoathirika zaidi kutokana na mvua hizo ni pamoja na Keko, Chang’ombe Maduka Mawili, Yombo Vituka, Vingunguti, Africana, Msasani Bonde la Mpunga, Jangwani, Manzese, Kigogo, Mburahati, Boko na Basihaya.
Waathirika waweka ngumu
Licha ya kuathirika na mafuriko yaliyotokana na mvua zilizoonyesha mfululizo kwa siku kadhaa, wakazi wa maeneo yaliyopatwa na adha hiyo wamesisitiza kuwa hawatahama katika makazi yao kwa sababu mafuriko yamewafuata.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili walidai kuwa wameishi maeneo hayo kwa miaka mingi, wakipata huduma zote, ikiwamo maji, umeme lakini hakukuwa na adha hiyo, huku wakiitupia lawama Serikali kwa kushindwa kutafuta jinsi ya kuwasaidia.
Wakazi wa Magomeni Madaba ambako nyumba zilijaa maji na kuonekana paa juzi na jana, kwa nyakati tofauti walisema kuwa huu ni mwaka wa nne wanaingiliwa na maji na miaka minne iliyopita, walipewa namba kwa ajili ya kupewa viwanja lakini hadi leo hawajapewa

Post a Comment

Previous Post Next Post