Halmashauri 26 zinazoongozwa na vyama vya upinzani nchini Zatishia Kujiondoa ALAT


Halmashauri zinazoongozwa na vyama vya upinzani nchini vinavyounda umoja wa katiba ya wananchi (UKAWA) zinakusudia kujiondoa kuwa wanachama wa Jumuiya ya Halmashauri Nchini (ALAT), endapo mapendekezo waliyoyatoa yatapuuzwa.

Akiwasilisha maazimio ya kikao chao jana mbele ya waandishi wa habari mjini Dodoma, Makamu Mwenyekiti wa umoja wa wenyeviti na mameya wa halmashauri zinazoongozwa na (UKAWA) ambaye pia ni Meya wa Jiji la Arusha, Bw. Calist Lazaro, alisema wamependekeza kubalishwa kwa sheria na kanuni za katiba ya (ALAT), ili ziweze kuendana na wakati uliopo na kutoa mazingira rafiki kwa vyama vya upinzani, ili viweze kuwa na uwakilishi katika kamati tendaji ya (ALAT) taifa

Ukawa, ambayo inaundwa na vyama vya Chadema, CUF, NLD na NCCRMageuzi, imeshikilia majiji na halmashauri kubwa nchini baada ya kupata ushindi kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2015 uliokuwa na ushindani mkubwa. 
Kati ya majiji, miji na halmashauri 26 zilizo chini ya vyama hivyo, kuna majiji matatu ya Mbeya, Arusha na Dar es Salaam, baadhi ya manispaa muhimu za miji kama Iringa, Moshi na Siha mkoani Kilimanjaro, Tunduma (Songwe), Monduli (Arusha), Kinondoni na, Ilala (Dar es Salaam).

Alisema athari itakazopata kama wakijitoa ni kuyumba kifedha kutokana na ukweli kuwa majiji na halmashauri hizo ndizo zinazotoa michango mikubwa kwenye mfuko wa umoja huo.

“Kama mambo tuliyopendekeza hayatafanyiwa kazi, tutajitoa kwenye umoja huu na kuangalia uwezekano wa kuunda umoja mwingine ambao kweli utakuwa ni kwa maslahi ya taasisi hizi za serikali za mitaa,” alisema.

“Halmashauri zetu hazitachangia, Alat wabaki na chombo chao.”

Mbali na michango, Alat pia hutegemea fedha za wafadhili na wadhamini wa shughuli zao.

Kalist, ambaye ni meya wa Jiji la Arusha, aliiutaka uongozi wa Alat kufanya marekebisho ya katiba na kanuni za Alat ziweze kuendana na wakati kwa kutoa mazingira rafiki kwa vyama vya upinzani.

Alisema mazingira hayo ni kuwa na uwakilishi katika kamati ya utendaji ya Alat Taifa kama ilivyo bungeni na katika kamati za fedha za halmashauri ambapo suala la uwepo wa uwiano wa kivyama miongoni mwa wajumbe ni la kikanuni.

Pia mameya na wenyeviti hao walitangaza kutoutambua uongozi mpya wa Alat kwa madai ulichaguliwa kinyume cha Katiba ya Alat na kanuni za uchaguzi za mwaka 2009.

“Tunaomba Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kukagua mapato na matumizi ya Alat kwa kuwa fedha hizi ni za wananchi zinazochangwa kupitia halmashauri zao,” alisema.

Miongoni mwa mambo wanayodai kukiukwa katika uchaguzi huo ni pamoja na kumruhusu Meya wa Jiji la Tanga kugombea umakamu mwenyekiti, wakidai kuwa si chaguo la wananchi wa jiji la Tanga kupitia madiwani wao

Post a Comment

Previous Post Next Post