TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
RIADHA TANZANIA (RT)
Juni 21, 2012
Ndugu Wanahabri,
Riadha Tanzania inapenda kuwakaribisha na kushukuru kwa kufika kwenu.
Madhumuni ya kuwa hapa
leo ni kushirikiana nannyi ili Watanzania wote ambao ni wadau wa mchezo
wa Riadha, wajue baadhi ya yale tunayoyafanya sasa hivi na yale
tunayokusudia kuyafanya:
1: Mashindano ya
Taifa, ambayo kalenda ilikuwa ikionesha yafanyike Julai 7 na 8 jijini
Dar es Salaam na kuahirishwa hadi Julai 20-23, lakini kutokana na mikoa
mingi kutumia wanafunzi wa shule za Msingi na Sekondari, tumeyapeleka
wikendi ya mwisho wa Agosti, tarehe 31-Septemba 2. Ili kutoa nafasi kwa
wachezaji hao ambao wanamaliza mashindano yao ya UMITASHUMTA NA UMISSETA
yanayomalizika Julai 15.
2: Mchakato wa Katiba
ya RT, katika kikao cha Kamati ya Utendaji kilichokaa Juni 10 mjini
Morogoro, kiliridhia kukabidhi kazi hiyo kwa wataalamu na wanasheria na
baada ya wiki moja kuanzia sasa, tutakuwa tumepata rasimu ya katiba
mpya, ambayo katika itaipitia na kuitawanya ikiwamo kuwekwa katika
tovuti ya RT, ili wanachama na wadau kuipitia na kutoa maoni yao.
3: Ushiriki Mashindano ya Afrika-Benin Juni 26-Julai 2.
i. Timu teule ya riadha ya Jeshi, (JWTZ), iliyokuwa kwenye mazoezi huko Mbulu, Manyara, ndio itakayoliwakilisha Taifa.
ii. Uongozi wa juu
wa RT, Rais na Makamu wa Kwanza, wanategemea kuondoka Juni 24 kwenda
katika mkutano wa mwaka wa Shirikisho la Riadha la Afrika, (CAA), na
wakati huo huo watakutana na Rais wa Afrika na Shirikisho la Riadha la
Kimataifa (IAAF), na viongozi wa mashirikisho mbalimbali ya Riadha ya
nchi za Afrika.
4: RT inatoa wito kwa
wadau na wapenda michezo kote nchini, kuanzisha klabu mbalimbali za
riadha ili kuibua na kuendeleza vipaji vya watoto kuanzia miaka 12 na
kuendelea katika michezo ya ndani (field events), na mbio za uwanjani
(Truck events). Lazima klabu hizo zizingatie hili.
5: RT itahakikisha
inatoa mafunzo ya ukocha wa awali, katika vyuo vya ualimu
vinavyofundisha mchepuo wa ulimu kwa michezo, ili wanapomaliza waweze
kufundisha riadha kwa ufasaha katika shule zao. Mfano hivi karibuni,
tumetoa mafunzo katika Chuo cha Ualimu Korogwe.
6: RT itakuwa na utaratibu maalumu ambao utakuwa na muongozo kwa wale wote wanaondaa mbio za aina zote.
Utaratibu huo utakuwa
na lengo la kulinda maslahi ya pande zote, kuanzia Riadha Tanzania,
Chama cha Mkoa husika, wachezaji na waandaji, kwa manufaa ya maendeleo
ya mchezo wa riadha Tanzania.
RT itakuwa makini na wakali kwa wale ambao watakwenda kinyume na taratibu za mchezo wa riadha hapa nchini.
7: Katika mpango
mkakati mmojawapo, ambao tumejipanga ni kuwa na kitalu cha wachezaji,
(Sports Centre), mkoani Singida, ambako tayari kuna heka takribani 50,
ambako kitajengwa kituo hicho kwa ajili ya kulea na kuendeleza watoto
wenye uwezo na vipaji. (High Performance Training Centre).
Asanteni kwa kunisikiliza, tushirikiane kujenga riadha yetu.
William Kallaghe
Makamu wa Kwanza wa Rais (RT).
KNY ya Rais RT.
Mwisho
Post a Comment