Chanzo chaeleza jinsi ndege ya Malaysia ilivyopotea, kikosi cha China chaona 'mabaki'

Bado juhudi zinaendelea katika kuisaka ndege ya Malaysia aina ya Boeing 777 na habari mpya kuhusu kinachoendelea zinazidi kutolewa licha ya ukweli kuwa bado ni mtihani mkubwa kwa nchi zilizoingia kwenye msako huo.
Chanzo cha karibu na vikosi vinavyofanya msako wa ndege hiyo kimeiambia CNN kuwa radar ya kijeshi imeonesha kuwa ndege hiyo ilibadili muelekeo na kukata kona kali katika eneo la kusini mwa bahari ya China wakati ikielekea Malacca.
Chanzo hicho kimeeleza kuwa imeonekana kuwa baada ya kupiga kona hiyo ilishuka chini na  iliruka umbali wa futi 12,000 kabla haijatoweka kabisa kwenye radar.
Inasadikika kuwa ndege hiyo ilipiga kona kwa kukusudia na sio kutokana na tatizo kwa kuwa kulikuwa na kila uwezekano wa marubani wa ndege hiyo kuonesha ishara ya hatari.
Hata hivyo baadhi ya wachunguzi wanasema bado inawezekana marubani walishindwa kabisa kufanya mawasiliano kutokana na hali ilivyokuwa.
Katika hatua nyingine, imeripotiwa kuwa kikosi cha China kimeona vitu vinavyosadikika kuwa mabaki ya ndege hiyo kusini mwa bahari ya Hindi.
Shirika la habari la ABC America, limeripoti kuwa kikosi hicho kimeeleza kuwa kimeona vitu viwili vikubwa vyenye rangi nyeupe vikiwa vinaelea baharini.
Vitu hivyo vimeonekana kuwa kuwa na rangi nyeupe na vilishuhudiwa pia na askari mmoja wa Australia aliyekuwa katika ndege ya kikosi hicho cha China.  
Ni zaidi ya siku 16 sasa tangu ndege hiyo ipotee ikiwa na watu 239 na hadi sasa haijafahamika chanzo cha kupotea kwa ndege hiyo.

Post a Comment

أحدث أقدم