Ilichosema Yanga kuhusu serikali kuchukua eneo lao na kujenga kituo cha mradi wa mabasi yaendayo kasi

YANGASC1Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi wa Jengo la Yanga, Francis Kifukwe amesema kituo cha mabasi yaendayo kasi (DARTS) kilichojengwa eneo Jangwani kipo ndani ya eneo lao.
Kifukwe aliyasema hayo wakati ya ziara ya Kamati ya Mipango Miji na Mazingira ya Manispaa ya Ilala jana ilifanya ziara ya ukaguzi Jangwani kuangalia eneo linaloombwa na klabu ya Yanga kwa ajili ya ujenzi wa uwanja wake wa kisasa.
Kifukwe alionyesha eneo wanalohitaji kuongezewa mbele ya Kamati ya Mazingira kuwa eneo lao linafika hadi kwenye kituo cha mabasi ya mwendo kasi akidai kuwa waongezewe mpaka kwenye bonde la Mto Msimbazi ambako pia akidai kuna mabomba mawili ya majitaka yanayopeleka maji baharini moja likiwa la Kiwanda cha Bia Tanzania (TBL).
“Kile kituo cha mabasi tumeambiwa kipo pale kwa muda, kwa upande huu tutafika mpaka sehemu ya matairi (karibu na bonde Msimbazi), na upande huu wa Barabara ya Morogoro, mwisho wa mpaka wetu ni hapa kwenye misufi, lakini tunaomba mtuongezee mpaka kule barabarani kabisa.
“Mtuzidishie barabarani kwa vile upande huu wa mbele tayari kuna barabara ya kiwango cha lami imejengwa ambayo inaenda mpaka Kigogo na inatumika na watu wengi hivyo hii barabara hatutaigusa, na upande huu wa Barabara ya Morogoro kuna bomba jingine ambalo litaingia ndani ya uwanja wetu.”alisema.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Mipango Miji na Mazingira ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Upanga Mashariki, Sultan Salum akizungumza mara baada ya ziara hiyo alisema wamepokea maombi ya Yanga na wameona eneo wanalohitaji, hivyo watakaa kikao Jumanne ijayo kujadili suala hilo na kujiridhisha iwapo itafaa kwa Yanga kupatiwa eneo hilo.
“Hili suala lina mlolongo mrefu, kwa sababu sio NEMC tu itabidi liende mpaka kwa watu wa Ardhi, na Serikali Kuu, sio la kumalizika leo hili, sisi Jumanne tutakaa wajumbe watakavyoamua tutawapa majibu.”alisema.
Hata hivyo; tayari ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Manispaa ya Ilala imeshaweka wazi msimamo wake wa kuwataka viongozi wa Yanga kubeba dhamana ya fidia za watakaoathirika na ujenzi wa uwanja huo na kwamba gharama halisi itajulikana itakapofanyika tathmini halisi.
 SOURCE: MWANANCHI

Post a Comment

Previous Post Next Post