Mwisho wa uhasama


Marekani na Cuba zimekuwa na uhasama wa zaidi ya miaka 50 sasa na kusababisha Taifa hilo kuwekewa vikwazo vya kiuchumi kwa miaka mitano. Rais Raul Castro amemwomba Rais Obama kuiondolea nchi yake vikwazo hivyo alivyosema vimeiletea nchi yake madhara makubwa.
Baada ya miongo ya miaka ya kutokuwepo uhusiano wa kibalozi, Marekani sasa imetangaza kuwa inataka irejeshe uhusiano wake na Cuba uwe wa kawaida.
Katika hotuba yake kupitia televisheni, Rais Barack Obama alisema alifikia uamuzi huo baada ya kuzungumza na mwenzake wa Cuba, Raul Castro.
Naye Castro aliwaambia wananchi wake kwamba anaikaribisha hatua hiyo ya Washington, lakini akataja kwamba bado ziko tofauti ambazo hazijatatuliwa kisawasawa baina ya nchi mbili hizo.
Barack Obama anasema siasa iliyokuwa inafuatwa na nchi yake kabla ya hapo ilikuwa haiambatani na wakati wa sasa na haijasaidia kupeleka mbele masilahi ya Marekani.
Kuitenga Cuba hakujafanya kazi, ni wakati sasa wa kuwa na siasa mpya, alisema Obama huku akiongeza kwamba, badala yake Marekani sasa inataka kuwasaidia raia wa Cuba na kuboresha uhusiano baina ya nchi hizo mbili.
Haya ni mabadiliko muhimu sana katika siasa ya Marekani kuelekea Cuba tangu kupita zaidi ya miaka 50.
Uhusiano baina ya nchi mbili hizo ulivunjika mwaka 1961.
Sasa imetajwa kwamba ubalozi wa Marekani utafunguliwa tena mjini Havana na waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani, John Kerry, bila ya kuchelewa, ataanza kufanya mazungumzo na Serikali ya Cuba. Mazungumzo ya wiki iliyopita baina ya Obama na Castro yalikuwa ya mwanzo ya moja kwa moja kuwahi kufanyika baina ya marais wa Marekani na Cuba tangu kuvunjika uhusiano wa kibalozi.
Yalitokana na mazungumzo ya siri yaliyodumu miezi 18 huko Canada. Pope Francis, Mkuu wa Kanisa Katholiki duniani, alichangia katika kufaulu kwa mazungumzo hayo.
Kurudisha uhusiano baina ya nchi hizo mbili kumesabaisha kubadilishana wafungwa. Cuba imemuachia huru jasusi wa Kimarekani mwenye cheo cha juu ambaye kwa zaidi ya miaka kumi amekuwa gerezani.
Pia, raia wa Marekani, Alan Gross mwenye umri wa miaka 65, ameachwa huru kwa sababu za kibinadamu. Alipewa kifungo cha miaka 15 jela kutokana na tuhuma za ujasusi.

Post a Comment

Previous Post Next Post