KOCHA mkuu wa timu ya Taifa ya Soka Tanzania, ‘Kilimanjaro Taifa
Stars’ Mdenish Kim Poulsen, amesema licha ya kuwa ni mara yake ya
kwanza kukinoa kikosi hicho ugonjwa unaokisumbua ni umaliziaji.
Akizungumza mara baada ya pambano la kirafiki kati ya Stars na Malawi
‘The Flames’ juzi Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam lililomalizika
kwa sare ya bila kufungana, Poulsen alisema, umaliziaji ndilo tatizo
linalowakabili vijana wake.
Poulsen alisema endapo tatizo hilo litakwisha, ana imani kikosi chake
kitafanya vema licha ya kuwa ni mara ya kwanza kukabidhiwa mzigo mkubwa
kama huo na kuwa kwa sasa analifanyia kazi tatizo hilo kubwa.
“Nimetazama na nilikuwa makini sana, lakini tatizo ni umaliziaji,
ukiangalia utafutaji kwa maana ya kiungo walijitahidi kufanya kazi yao
kwa umakini zaidi, tatizo lilikuwa katika kumalizia na hasa hapo
wapinzani wetu ndipo walipokuwa wakichukulia mpira,” alisema Poulsen.
Aidha Poulsen aliwapongeza vijana wake kwa jinsi ambavyo walijituma na
kusema kuwa mapungufu ni sehemu ya mchezo na ndio sababu ya kuwa na
mchezo wa kujipima nguvu kabla ya kuvaana na Ivory Coast kwenye mechi ya
mchujo ya Kombe la Dunia itakayofanyika ugenini Juni 2 mwaka huu.
Naye Kocha wa The Flames, Kinnah Phiri, amelipongeza Shirikisho la
Soka Tanzania (TFF), kwa kuona umuhimu na kuwaomba kuja hapa nchini
kucheza mchezo huo wa kirafiki na kuwa ni kipimo kizuri kwa timu yake.
Aliongeza kwa kuwapongeza wachezaji wa Stars, kwa uwezo wao na kusema
kuwa hata kama kuna upungufu ni kidogo, kwa kuwa ni moja ya makosa
katika soka kwani hata timu yake ina upungufu iliyouonyesha.
Katika hatua nyingine, pambano hilo kati ya Stars na The Flames,
limeingiza sh 40,980,000, kutokana na mashabiki 10,767 waliokata tiketi
kushuhudia.
Kili Taifa Stars imedhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania kupitia bia yake ya Kilimanjaro kwa kiasi cha sh bil. 23.
إرسال تعليق