Stamina ni tatizo Taifa Stars - Poulsen
WAKATI kikosi cha timu ya soka ya Tanzania, Taifa Stars,
kikitarajia kuondoka alfajiri ya kesho kwenda Ivory Coast kwa mechi ya
kimataifa, Kocha Mkuu wa timu hiyo, Kim Poulsen, amesema stamina ni
tatizo kubwa kwa nyota wengi.
Poulsen aliyetwaa jukumu hilo hivi karibuni kutoka kwa Jan Poulsen,
aliyasema hayo jana wakati akitoa tathmini fupi juu ya mazingira ya
kikosi chake tangu akabidhiwe jukumu hilo wiki mbili zilizopita.
Alisema, pamoja na wachezaji wengi kuwa na uwezo mkubwa kiuchezaji,
suala la stamina limekuwa tatizo kwa wachezaji wengi, hivyo kushindwa
kucheza kwa kasi na ufanisi kwa dakika zote 90.
Alisema kutokana na dosari hiyo, tayari ameanza kuchukua hatua kwa
kufanya mazungumza na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuangalia njia
bora ya kuondoa tatizo hilo kwa kushirikiana na makocha wa timu
nyingine.
“Kwa upande wa Stars, nimeshaanza nalo kwa kuwapa mazoezi ya ziada
baada ya mazoezi ya kawaida. Kwa kweli, wachezaji wameonekana
kuyakubali, wameridhishwa nayo na kuyafurahia, binafsi inanitia moyo,”
alisema.
Kim alisema mbali ya stamina, pia amekuwa akiwasihi wachezaji wake
kuwa na moyo wa kujituma, akisema hicho ni kitu muhimu kwa timu katika
kupigania ushindi na mafanikio ya timu.
Aidha, Poulsen alisema ndani ya kipindi cha wiki mbili alizodumu na
timu hiyo, wachezaji wameanza kuelewa falsafa yake, hivyo kumpa
matumaini ya kuwa na kikosi bora zaidi katika siku za usoni.
Hata hivyo, ameishauri TFF kuwa, wachezaji wote ambao watakuwepo
kambini kipindi cha maandalizi ya mechi, wote wawe wanasafiri na timu
(hata kama hawatacheza), kwa lengo la kuwapa nafasi ya kujifunza zaidi.
Kim alisema, kitendo cha mchezaji kusafiri humwongezea hamasa ya
kuitumikia timu na nchi yake sambamba na kuendeleza umoja na mshikamano
miongoni mwao.
Kuhusu mechi dhidi ya Ivory Coast itakayopigwa Juni 2, mjini Abidjan,
alisema kikosi chake kinawaheshimu wapinzani wao kutokana na kusheheni
nyota wengi wanaowika Ulaya wakiongozwa na Didier Drogba, lakini
watapambana.
Alisema licha ya umahiri wa Drogba, Yaya Toure na Solomon Kalou na
wengineo wengi, wachezaji wa Stars watapaswa kupambana kwani
hiyo ndio siri ya ushindi na mafanikio ya timu yoyote.
Mechi hiyo ni ya kuwania nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia
nchini Brazil mwaka 2014.
Katika hatua nyingine, Kim amekana kufanya upendeleo katika uteuzi wa
kikosi cha kwanza, hasa katika mechi ya kirafiki dhidi ya Malawi,
akisema alichagua kutokana na uwezo na sifa zao.
Aliongeza kuwa, nyota wake Nurdin Bakari na Thomas Ulimwengu watabaki
kutokana na kuwa majeruhi waliyopata wakati wa mazoezi yao, hivyo
watabaki kujinoa kabla ya kuungana na wenzao watakaporudi kujiandaa
dhidi ya Gambia.
Nyota wa Stars ni makipa: Juma Kaseja (Simba), Mwadini Ally (Azam) na
Deogratius Munishi (Mtibwa Sugar). Mabeki: Nassor Masoud Cholo (Simba),
Aggrey Morris (Azam), Amir Maftah (Simba), Erasto Nyoni (Azam), Kelvin
Yondani (Simba), Waziri Salum (Azam), Shomari Kapombe (Simba) na Juma
Nyoso (Simba).
Viungo ni Mwinyi Kazimoto (Simba), Salum Abubakar (Azam), Jonas Mkude
(Simba), Shabani Nditi (Mtibwa Sugar), Edward Christopher (Simba - U20),
Mrisho Ngasa (Azam) na Frank Domayo (JKT Ruvu- U20).
Washambuliaji ni Mbwana Samata (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya
Congo), Ramadhan Singano (Simba -U20), Simon Msuva (Moro United - U20),
Haruna Moshi (Simba) na John Bocco (Azam).
إرسال تعليق