Simba wafuata kifaa Sofapaka

fKLABU ya Simba imeanza harakati za kuimarisha kikosi cha msimu ujao kwa ajili ya mashindano ya kitaifa na kimataifa kwa kusajili nyota ambao watakuwa tishio.
Habari kutoka ndani ya klabu hiyo zimedokeza kuwa, chini ya mkakati huo, Simba imeanza harakati za chinichini za kufuatilia nyendo za wachezaji wa ndani na nje ya nchi.
Chanzo cha uhakika kutoka ndani ya uongozi wa Simba, kilidokeza jana kuwa, kwa sasa klabu hiyo imo kwenye harakati za kumsajili mchezaji kutoka Sofapaka ya Kenya.
Tayari viongozi wawili wa klabu hiyo, wapo nchini Kenya kumfuatilia mchezaji huyo ambaye jina lake kwa sasa, wametaka liwe siri kwani mambo hayajakamilika.
Chanzo hicho kimedokeza kuwa, Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ na Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi, Ibrahim Masoud, jana walikuwa Nairobi, Kenya kuweka mipango sawa.
Chanzo hicho kilisema kuwa, kilichowapeleka si kuchunguza uwezo wa nyota huyo, kwani walishamfuatilia kwa muda mrefu na kujiridhisha kuwa, atakuwa ni nguzo muhimu katika safu ya ulinzi ya timu hiyo kwa mujibu wa matakwa ya Kocha Milovan Cirkovic.
Simba wamekuwa katika juhudi za kusaka wachezaji wa kuimarisha kikosi chao, na tayari ina wageni wawili; Musa Muse (Uganda) na Patric Mbiyavamba (DR Congo) wanaofanyiwa majaribio.
Simba ambao ni mabingwa wapya wa Ligi Kuu ya Tanzania bara, wanakabiliwa na michuano ya Kombe la Kagame itakayofanyika baadaye mwezi huu, Ligi Kuu Bara na Ligi ya Mabingwa Afrika.

Post a Comment

أحدث أقدم