TEGETE AONGEZA MKATABA YANGA
MSHAMBULIAJI Jerryson John Tegete amesaini jioni hii
mkataba wa miaka miwili wa kuendelea kuichezea Yanga hadi mwaka 2014, hivyo
kuwakata maini Simba waliokuwa wanamnyemelea kupata saini yake.
Jerry (pichani kushoto) amesema usiku huu kwamba amesaini mkataba wa miaka miwili zaidi
kuendelea kuichezea Yanga. “Nimesaini leo, mimi ni mchezaji halali wa Yanga,
kweli kabla ya kusaini na hali ya mambo ilivyokuwa Yanga (migogoro) niliwahi
kufanya mazungumzo na viongozi wa Simba na Azam, ilikuwa kama tunaelekea
kukubaliana, ila sasa nashukuru hali imetulia klabuni, nami nimesaini leo,”alisema
Tegete.
Habari zisizo na shaka kutoka
ndani ya Yanga, zimesema kwamba Tegete ambaye amemaliza mkataba wake mwezi huu,
amesaini kwa watu ambao wamepewa kazi ya kufanya zoezi la usajili, Abdallah
Ahmad Bin Kleb na Seif Ahmad ‘Magari’.
Simba, baada ya kipa wao Ally
Mustafa Mtinge ‘Barthez’ na beki wa kati Kelvin Patrick Yondan ‘Cotton Juice’
kusaini Yanga, ikaamua kutaka kulipa kisasi na baada ya kufanikiwa kumtia
mkononi Kiggi Makassy, ikahamia kwa Tegete.
Hata hivyo, wapinzani wao hao wa
jadi, wameshituka mapema na kumtia pingu mpachika mabao wao huyo, ambaye msimu uliopita
haukuwa mzuri kwake.
Jerry alitua Yanga mwaka 2008,
akitokea sekondari ya Makongo na haikuchukua muda kuwa tegemeo la mabao kwa
timu hiyo, hususan katika mechi za watani wa jadi, ingawa msimu uliopita
majeruhi yalimpunguza kasi.
Post a Comment