Dk. Ulimboka Mahututi

Hali ya afya ya Dk. Steven Ulimboka ambaye anatibiwa Afrika Kusini, imebadilika ghafla na kuna habari kuwa yuko mahututi.
Habari zilizoifikia Tanzania Daima kutoka vyanzo mbalimbali vya habari ndani na nje ya nchi, zimesema kuwa Dk. Ulimboka alikuwa amepoteza fahamu, na juhudi za kuokoa maisha yake zilikuwa zikiendelea chini ya jopo la madaktari bingwa wa nchi hiyo na wale wa Tanzania.
Inadaiwa kwamba hali ya kiongozi huyo wa jumuiya ya madaktari nchini ambaye alikimbizwa nchini humo wiki iliyopita, awali ilielezwa kuwa inaendelea vema, lakini ghafla ikabadilika na kufikia kiwango cha kupoteza fahamu.
Mwandishi wa habari wa Shirika la Habari la Uingereza (BBC) alikaririwa akisema kuwa hali ya Ulimboka ilikuwa mbaya, na kwamba kulikuwa na ulinzi na usiri mkubwa kuhusiana na hali hiyo.
Jijini Dar es Salaam, mmoja wa madaktari aliyezungumza na gazeti hili kwa sharti la kutotajwa jina, alisema kuwa walipata taarifa za kuzidiwa kwa Dk. Ulimboka kutoka kwa ndugu yake aliyeko Afrika Kusini kwamba alikuwa yuko kwenye hali mbaya, hali iliyowachanganya mno.
Mmoja wa madaktari alikiri kupokea taarifa za kuzidiwa kwa mwenyekiti wao kutoka kwa kaka wa Dk. Ulimboka.
“Leo asubuhi baada ya kupokea taarifa za kuzidiwa kwa Dk. Ulimboka kikaitishwa kikao cha dharura cha madaktari wote tunaelekea huko,” alisema.
Hata hivyo, majira ya mchana habari zilivuma kwamba Dk. Ulimboka alikuwa amefariki, hali iliyozidi kuzusha wasiwasi mwingi miongoni mwa madaktari, viongozi wa vyama vya kijamii na wananchi wa kawaida waliokuwa wakihaha kupata ukweli wake.
Uvumi huo hata hivyo, ulikanushwa baadaye na msemaji wa Hospitali ya Muhimbili Kitengo cha Mifupa MOI Almasi Jumaa lakini akakiri kupata taarifa za kubadilika kwa hali ya mgonjwa huyo.
Chanzo:- Tanzania Daima

Post a Comment

Previous Post Next Post