Nyayo Za Chifu Mkwavinyika Mkwawa - 8


Akinamama wakicheza ngoma ya yailya katika jengo lililokuwa la Chifu Merere Mgandilwa wa Usangu kwenye Kijiji cha Mbalino.

Mgogoro wapamba moto katika Himaya ya Uhehe

HUU ni mfululizo wa Makala ya Uchunguzi kuhusiana na historia ya kiongozi mkuu wa Wahehe, Chifu Mkwavinyika Munyigumba Kilonge Mwamuyinga, maarufu kama Mkwawa, kama yanavyoandikwa na Mwandishi Wetu DANIEL MBEGA, ambaye amefanya uchunguzi kwa takriban miezi mitatu sasa katika kuhimiza utalii wa ndani na kuhifadhi historia yetu. Endelea na Sehemu hii ya Nane…

KAMA tulivyoona huko nyuma, Wajerumani walionekana wema kuliko Mkwawa, ambapo makabila mengi yaliyoizunguka Himaya ya Uhehe yaliyokuwa yakinyanyaswa hapo kabla yaliona kwamba Wazungu hao ndiyo kimbilio lao na wangeweza kuwatetea dhidi ya Mkwawa.
Wazungu kwa kiasi kikubwa wanaipotosha historia katika kuhalalisha kile wanachodhani Waafrika watakiona ndicho bora zaidi. Katika historia ya Mkwawa, wanadai kwamba, utajiri ambao Chifu Mkwawa aliurithi kutoka kwa baba yake Munyigumba ulikuwa ni wa dhulma, kwamba waliupata kwa kupora misafara, kama walivyofanya Wangoni na Wasangu.
Na itakumbukwa kwamba, Mkwawa aliendelea kuivamia misafara ya Wajerumani katika Njia ya Kati kadiri alivyoweza, hali ambayo baadaye ikasababisha mapigano mengine katika Kijiji cha Munisagara Desemba 7, 1892 ambapo pamoja na Wahehe kushindwa, lakini walifanikiwa kukiteketeza Kijiji cha Kondoa kwenye Bonde la Mukondoa karibu na ngome ya Wajerumani ya Kisaki.
Lakini siyo siri kwamba, ushindi wa Wahehe dhidi ya Wajerumani Agosti 1891 ulisikika kila pembe ya Afrika Mashariki ambapo Waafrika waliuzungumzia sana. Lakini mwishoni mwa mwaka 1892 na mwanzoni mwa 1893 kulikuwa na kila dalilia kwamba Wajerumani wangeweza kutawala kwa sababu nguvu zao dhidi ya Wahehe zilikuwa zimeimarika na kutanua mpaka wao.
Wasagara, ambao awali walikuwa wameishi kwa hofu ya Mkwawa na kumpelekea zawadi kila wakati ili asiwapige, sasa waliishi jirani na kambi za Wajerumani na wakaanza kuubeza uwezo wa Wahehe waziwazi.

 

Post a Comment

أحدث أقدم