HII NDIO FAINALI YA MASTAA WETU …HALI NGUMU YAMKABILI MZEE SMALL, PESA YA CHAKULA HAIKAMATIKI, WASANII WENGI WASHINDWA KUMJULIA HALI JAPO KWA NJIA YA SIMU

YUMKINI hakuna shabiki hata mmoja wa sanaa ya maigizo, filamu na komedi hapa nchini, asiyelifahamu jina la nguli wa tasnia hiyo, Said Ngamba ‘Mzee Small’.
Hiyo ni kwasababu, Small ni kati ya wakongwe waliotokea kuzizolea sifa kemkemu, kutokana na umahiri alionao katika kukonga nyoyo za watazamaji wa muvi za Kibongo.
Kwa wale waliokwishabahatika kutazama baadhi ya kazi alizowahi kushiriki mkongwe huyo, akiwa katika husika yoyote ile, wanaweza kuwa mashahidi wakubwa juu ya hilo.
Mzee Small akiwa Sebuleni kwake
Hivi karibuni, Small alikubwa na zahama ya ugonjwa wa kupooza mkono pamoja na mguu wake wa kusho, hali iliyosababisha kusimama wa shughuli zake zote hivi sasa.
Ugonjwa huo ulimpata ghafla katikati mwaka jana alipokuwa njiani wakati akirejea kutoka jijini Mwanza katika mradi wa Vicky Mtetema, wa kusaka walemavu wa ngozi (Maalbino), ili kuwapeleka nchini Marekani.
Akizungumza na Saluti5 mapema wiki iliyopita, nyumbani kwake Tabata Mawenzi, Small anasema kuwa, ana zaidi ya mwaka mmoja sasa hajatoka nje, huku familia yake ikimfanyia kila kitu kama mtoto mdogo.
“Kiukweli, nasikitika kuona hakuna msaada wowote ninaoupata kutoka kwa viongozi wa serikali, licha ya kuwa kati ya waigizaji wa mwanzo, niliyechangia mapinduzi makubwa kisanaa,” anasema Small.
Japo kapooza mguu, kusimama mwenyewe si jambo linalomsubua
Anasema kuwa, hivi sasa amekuwa akikosa ushirikiano wa kutosha hata kwa wasanii wenzie waliokataa kumkumbuka hata tu kwa kumsalimu kupitia simu yake ya mkononi.
Hata hivyo, kama ilivyo ada, penye wabaya halisi na wema pia hawakosi, kuna baadhi ya wasanii ambao wamekuwa wakifika nyumbani kwake mara kwa mara na kumjulia hali.
Anawataja baadhi yao kuwa ni pamoja na ‘mke wake wa maigizo’ ‘Bi Chau’, Tupatupa, Seif Mbembe, Kingwendu, Senga, Mhogo Mchungu, Natasha, JB, Dk Cheni na timu ya wachekeshaji wa ‘Mizengwe’.
“Maisha yangu hivi sasa yamekuwa magumu mno, kutokana na kuwa, kama ilivyo kwa walalahoi wengine wengi, riziki yangu iko miguuni, hivyo kukaa kwangu kitako kumefunga mambo mengi,” anasema Small.
Anafafanua kuwa, maisha yake yamekuwa magumu kwasababu, yeye ndio tegemeo kwenye familia, kuanzia katika kulisha hadi kusomesha wanawe ambao wengine wako elimu ya juu.
Small anawaomba wasanii wenzake, mashabiki  pamoja na wadau wa sanaa ya maigizo kujitokeza kwa wingi kumsaidia, kutokana na kuwa, hana akiba inayoweza kumwendeshea maisha yake.
Pamoja na kusumbuliwa na maradhi hayo, bado Small anaamini kuwa iko siku Mungu atamwinua na kuanza kuburudisha tena kwa kufyatua kazi nyingine zaidi na kufanya maonesho.
Shida ni pale anapotaka kutembea, ni lazima asaidiwe
“Nanachosisitiza zaidi ni dua za Watanzania wenzangu, ili nipate nafuu haraka na endapo nitainukiwa, nitafanya onesho kubwa maeneo ya Jangwani, jijini Dar es Salaam,” anasema Small.
Anasema kuwa, kadhalika, atazunguuka mikoa mingine yote hapa nchini na kutumbuiza akiwa na kundi lake Afro Dance, hiyo ikiwa ni moja ya nadhiri kubwa alizoweka.
Akielezea namna alivyojitumbukiza kwenye uigizaji, Small anasema kuwa, mwaka 1970 alijifunza kuigiza kwa mtu aliyemtaja kwa jina la Said Seif Unono ambaye ni marehemu kwa sasa.
Hiyo ni baada ya mwaka 1965 kutua jijini Dar es Salaam kwa mara ya kwanza na kufikia Mtaa Sukuma na Mafia, Kariakoo, akitokea kijijini kwao ambako muda wote tangu azaliwe alikuwa akilima mazao mbalimbali ya chakula.
“Mwaka 1978 nilijiunga na Chuo cha Sanaa, Bagamoyo nikitokea kikundi cha Reli, ambako nikiwa Bagamoyo nilijifunza kwa miezi mitatu, kabla ya mwaka 1980 kuingia kikundi cha Jeshi la Magereza,” anasema Small.
Anasema, kuingia kwake Magereza alikoajiriwa na kupewa cheo cha Koplo, baada ya kuhudhuria na kufuzu vema mafunzo ya kijeshi, kulkitokana na kuvutwa na askari aitwaye Juma Futo.
Akiwa na Magereza, Small anasema kuwa, aliweza kuonesha cheche zake katika sanaa kiasi cha kutuzwa cheo cha Koplo na rais wa wakati huo, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Miaka miwili baadaye, yaani mwaka 1982 rigwaride lilimshinda Small, akaachana na Magereza na kujiunga na kundi la Agizo Group lililokuwa chini ya mwalimu wake, Unono.
“Baadaye kodogo nikaingia kundi lililokuwa likitikisa vilivyo wakati huo, Muungano Culture Troupe chini ya mkali wa kucheza na nyoka, Norbert Chenga, ambako nilikuwa mwigizaji na mcheza ngoma pia,” anasema Small.
Mwaka 1990 alifungasha virago Muungano na kuamua kuanzisha kundi lake aliloliita Afro Dance akiwa na wasanii kadhaa mahiri kama vile; Tupatupa, Hamis Chau na marehemu Zabibu.
Kutokana na fitna hizi na zile za kisanaa pamoja na kutojipanga kwake kikamilifu, Afro Dance ilikufa muda mfupi baada ya kuliasisi, akaajiriwa Bima Modern Taarab alikokutana na Bi Chau.
Bima Modern iliposambaratika, alimchukua Chau na kufufua Afro Dance linalotamba hadi sasa likiwa na filamu nyingi kali, zikiwamo zile za hivi karibuni; ‘Piga Ua Talaka Utatoa’ na ‘Tanga Waja Leo Waondoka Leo’.
“Nashukuru alhamdullilah sanaa imenijengea nyumba, kunisomeshea watoto, kuniolea mke, kutembea hadi nje ya mipaka ya Afrika na kujuana na wengi npamoja na kupata senti ya kula,” anathibitisha Small.
Hata hivyo, Small bado analia na upendo kiduchu uliopo miongoni mwa wasanii kwa kutothaminiana na kila mmoja hamjali mwingine ipasavyo.
Hii ndiyo nyumba ya Mzee Small
Unapomwulizwa kama ana mpango wa kurithisha kizazi chake sanaa anayoifanya, Small anasema mwanae yeyote anaweza kumrithi kwa mapenzi binafsi tu lakini si kwa kujitolea kumfundisha.
Hivi sasa, Small anapatikana muda wote nyumbani kwake, Tabata Mawenzi anakoishi na mkewe na watoto wake sita, ambao ni Mhiddin, Yunus, Mahmoud, Somoe, Sofia na Said.
Alizaliwa, mwaka 1955, Mingumbi, Kililima na kupata elimu ya msingi katika shule ya Mingumbi, ambako alisoma hadi darasa la tano, kati ya mwaka 1961 na 65.Wameandika jamaa wa www.saluti5.com

Post a Comment

Previous Post Next Post