![]() |
| Chuo kikuu cha Gollis kimefungua maktaba ya kieletroniki yenye vituo 30 vya kompyuta tarehe 12 Februari. [Barkhad Dahir/Sabahi] |
Na Barkhad Dahir, Hargeisa
Fatima Mohamed, mwenye umri wa miaka 24 mwanafunzi wa tiba katika chuo
kikuu cha Gollis huko Hargeisa, hana haja ya kuendelea kuwa na wasiwasi
tena kuhusu namna ya kupata nakala za vitabu vya kiada katika uga wake.
Vitabu vya kiada vimekuwa vikipatika kwa uchache nchini Somalia kutoka
vita vya wenyewe kwa wenyewe, lakini sasa Mohamed ana nafasi nzuri ya
kufikia vitabu kwa kupitia njia ya maktaba ya kieletroniki ambayo
ilifunguliwa mwezi uliopita katika kampasi inayoendeshwa kibinafsi.
"Nina furaha kuhusu huduma hii kwa sababu itasaidia kuinua na kuimarisha
maarifa ya wanafunzi ... imefanya kujifunza kuwa rahisi kwangu mimi,"
aliiambia Sabahi.
Maktaba ya vitabu vya kielektroniki ilikuwa ya kwanza ya aina yake
kufunguliwa Somalia wakati wakuu wa Chuo Kikuu cha Gollis kilipoitangaza
rasmi katika kampasi ya Hargeisa tarehe 12 Februari. Sasa wanafunzi
wanaweza kukaa kwenye sehemu ya kufanyia kazi ya kompyuta na kupata
vitabu kwenye skrini mbele yao.

Wanafunzi wa chuo kikuu cha Gollis waksoma
kwenye maktaba ya kieletroniki iliyofunguliwa hivi karibuni, maktaba ya
aina hiyo ni ya kwanza nchini Somalia. [Barkhad Dahir/Sabahi]
Aidaros Mohamed Abib, mkuu wa taaluma wa chuo kikuu, alisema maktaba ya kielekroniki ni bure kwa wanafunzi wa chuo kikuu 3,500.
"Kwa wakati mmoja, wanafunzi 30 wanaweza kukaa pale, kuwa na uwezo wa
kutumia vitabu vinavyotumiwa na idara tofauti za chuo -- vilivyo vingi
ni vitabu vya uhandisi, sayansi, udaktari, utawala na uongozi," Abib
alisema.
Abib alisema anatumaini chuo kikuu kitaweza kuongeza idadi ya kompyuta
katika maktaba ili kutosheleza wanafunzi wengi zaidi kwa wakati mmoja.
Zaidi ya hayo, mwezi ujao Chuo Kikuu cha Gollis kinapanga kuzindua
sehemu ya mtandao, ambapo wanafunzi na wasio wanafunzi kwa pamoja
wanaweza kulipa ada ndogo ili kupata vitabu kutoka katika eneo lolote
kupitia intaneti.
"Tutaanzisha utaratibu [katika mtandao] utakaoweza kupatikana kutoka
kokote, na kutoa uanachama kwa yeyote ambaye anavutiwa," alisema Walid
Mohamed Ali, mkurugenzi wa idara ya teknolojia ya habari katika chuo
kikuu.
Mara utaratibu huo utakapokuwa tayari kufanya kazi, utawawezesha watu
kuvipata vitabu 50,000 vya ngazi ya chuo pamoja na mihadhara 10,000 ya
video na ya sauti kwa njia ya mtandao, aliiambia Sabahi. Vitabu vingi
vimechapishwa kwa Kiingereza, lakini baadhi vitapatikana kwa Kiarabu.
Kuanzisha maktaba ya kielektroniki kutasaidia kutatua tatizo la ukosefu
wa vitabu vya kiada na vya ziada huko Somaliland, lakini mkoa bado una
maktaba chache sana za umma na vitabu vingi vya kiada vinachapishwa kwa
lugha nyingine ambazo si Kisomali, alisema Khadar Abayare, profesa wa
Chuo Kikuu cha Hargeisa.
Hargeisa ina maktaba mbili pekee ambazo zinatumiwa na umma: Maktaba ya
Umma ya Gandhi inayoendeshwa kibinafsi na kituo kinachoendeshwa na Mfuko
wa Asasi ya Kiingereza kwa ajili ya Elimu ya Afrika, alisema Hodo
Sultan Aden, mkuu wa Shirika la Mohamed Mogeh kwa ajili ya Kusoma,
Kuandika, Mila na Utamaduni.
"Kusoma ni kipengele muhimu ambacho kinakosekana sasa, na wanafunzi
wanazuiliwa katika ufafanuzi wanaopewa na walimu," Aden aliiambia
Sabahi. "Hii ni changamoto ambayo inazuia ubora wa ukuaji wa kujifunza
wa wanafunzi wa Chuo Kikuu huko Somaliland."
Chanzo: sabahionline.com

إرسال تعليق