Polisi wajipanga kudhibiti dawa za kulevya JNIA


Kutokana na matukio ya upitishwaji wa dawa za kulevya kukithiri katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere (JNIA), Jeshi la Polisi Kikosi cha Viwanja vya ndege limesema kwa sasa linajipanga kukabiliana na matukio hayo kwa kuweka na kufunga vitendea kazi vya kisasa.
Mpango huo umetangazwa na  Kamanda wa kikosi hicho, Deusdedit Kato wakati akizungumza na NIPASHE kuhusu mikakati ya jeshi hilo kupambana na matukio ya upitishwaji kiholela wa dawa za kulevya.
Mpango huo ameutangaza siku chache tangu aueleze umma kwamba Polisi inashindwa kunasa watuhumiwa wanaosafirisha dawa za kulevya wanaopitia JNIA, kutokana na kukosekana kwa vitendea kazi vya kisasa.
Akihojiwa katika kipindi cha Kumepambazuka kinachorushwa na Radio One juu kwanini JNIA umeonekana kuwa kitovu cha kupitisha dawa za kulevya, Kato alisema sababu kubwa ni kwamba kuna tofauti kati ya nchi na nchi katika masuala ya teknolojia katika kubaini dawa za kulevya. 
Alisema nchi nyingine zina vifaa vya kisasa zaidi na kwamba wakati sasa umefika kwa serikali kuwekeza katika kupata vitendea kazi zaidi ili kufanikisha mapambano ya dawa za kulevya.
Alisema katika kipindi cha miezi sita hadi nane, watu 14 wamekamatwa wakituhumiwa kusafirisha dawa za kulevya nchini
Alisema tatizo la upitishwaji wa dawa za kulevya katika viwanja vya ndege ni tatizo la Dunia nzima hivyo linahitaji ushirikiano na kila mtu.
Alisema kwa sasa jeshi lake limejipanga kuhakikisha linapambana na matukio hayo kwa kuweka mikakati mbalimbali ikiwamo la kuweka vitendea kazi vya kisasa.
Kato hakuweza kuelezea mikakati mingine iliyopo kwa kile alichodai ni kuogopa kuwapa mbinu hiyo wahusika wa dawa hizo. 
Alisema suala la ukamatwaji wa dawa za kulevya haliwezi kushughulikiwa na taasisi moja tu, bali linahitaji ushirikiano wa hali ya juu pamoja na kujipanga.
Alisema siyo jeshi la Polisi peke yao ndiyo wanaopaswa kutupiwa lawama huku kukiwa na taasisi mbalimbali zinazofanya kazi ya kukagua mizigo JNIA.
 
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment

أحدث أقدم