Haya ndio Mambo 6 watayarishaji wa muziki TZ wanapaswa kufanya kutunza heshima na haki zao

BeauttyShot-1
Mara kadhaa nimesikia malalamiko fulani kutoka wa watayarishaji wa muziki wa bongo hususani watayarishaji wachanga, uchanga kwa maana kwamba hawana muda mrefu kwenye hii tasnia lakini pia wenye muda mrefu lakini hawajapata fursa ya kuwa miongoni watayarishaji wanaofuatwa sana na superstars na pia majina yao kutotajwa na kuzungumziwa sana katika vyombo vya habari hapa nchini.
Malalamiko ama niyaite manung’uniko yanayotawala zaidi vinywa vyao ni kusahauliwa na wasanii waliofikishwa mbali na nyimbo walizozitayarisha wao, kama ilivyo mara nyingi watayarishaji hawa ndio huwaomba superstars kuingiza maneno yao kwenye beats zao, hili limetawala zaidi mikoani pindi wasanii wafikapo kwa ajili ya matamasha.
“Palipo na ulaji hapakosi maneno”…huu ni msemo wa kale lakini usiozeeka kwakuwa nguvu yake yaonekana katika kila nyanja ihusishayo ‘chochotekitu’, zungumzia siasa, zungumzia biashara, lakini pia zungumzia muziki (nyanja ambayo mimi nimeshawishika kuidadavua hapa).
Muziki kwa kiasi kikubwa hivi leo umekuwa na fursa nyingi sana tofauti na zamani, wapo wanaotumia fursa hizo vizuri lakini pia wapo ambao mpaka leo wako nyuma kimawazo, hii inamaanisha kupoteza nafasi nyingi ambazo laiti kama wangezizingatia mapema basi wangeyaona na kuyatafuna matunda ya kazi zao.
Naamini kinachokuwa kichwani mwa mtayarishaji wakati anafanya beat ya wimbo ni kufanikiwa kwa wimbo huo tunasema ana “visualize” mafanikio. Kubwa ambalo analiweka kichwani kwa wakati ule ni wimbo kupigwa na kupendwa kisha yeye kujulikana zaidi, nimekaa na watayarishaji wengi wa aina hii na kwa kuwasoma mind zao nikaona kabisa kwamba fedha si kitu wanachowaza kwa wakati ule.
Wimbo unatoka na unapendwa (kama mtayarishaji alivyotamani) lakini anakosa kuzungumziwa sana kwenye vyombo vya habari pindi wimbo uzungumziwapo (tofauti na matarajio yake), maneno yanaanza chinichini kuwa kafanya ngoma lakini hasikii kuzungumziwa yeye pindi wimbo na msanii wazungumziwapo, naambiwa kwenye soko kila mtu anatakiwa kufanya lake ili kupata publicity.
Msanii yeye sifa yake inaimarika, anapata shows na matangazo ya kufanya, anaingiza wimbo kwenye makampuni ya simu na hatimaye labda anakuwa awarded kutokana na wimbo huohuo (vitu ambavyo mtayarishaji hakuvifikiria awali), na hapo ndipo manung’uniko yanapoanza kupamba moto, producer anakosa morali ya kufanya kazi na anaishia tu kuingiza mamoshi na vinywaji vikali mwilini mwake.
Pesa haijawahi kutosha hata siku moja ndio maana matajiri wadunia bado wanazisaka, mtayarishaji usitegemee Msanii akupe pesa baada ya mafanikio hayo kwakuwa naye anamatatizo yake kibaaaoo!!! Wachache sana wanaweza kukukumbuka wakati wanazivuna.
Kuanzia leo mtayarishaji nataka nikufungue macho ya upeo wako ili uone ambavyo havionekani kwa macho ya kawaida, ukishaona basi uchukue hatua lakini pia utafute vingine ambavyo mimi sitokuonyesha.
UNGEanza kukithamini kiti unachokalia, kipe heshima kwakuwa ofisi yako ndio kiwanda cha kutengenezea fedha za kuendeshea maisha yako. Ni wazi ukiipa heshima ofisi yako basi kila mtu anayetia mguu atakuheshimu lakini pia ataheshimu kazi ya mikono yako.
UNGEpata ushauri kisheria ya namna gani unaweza kuwa na haki ya kila kazi unayofanya hususani zile unazofanya bure. Bure yako iwe bure kwa muda ule tu nikimaanisha kuwa uwe umewekeza. Tengenezewa mikataba ambayo wewe na msanii unayemfanyia wimbo bure mtasaini, walau kuwe na asilimia fulani ambayo utaipata pindi wimbo huo uingizapo hela kwa namna yoyote (wanasheria watakueleza vizuri).
Hii itapoteza manung’uniko yako ambayo naweza sema ni makosa yako mwenyewe from the first place. Nina mfano mzuri wa wimbo wa Kala Jeremiah ambao aliutengeneza Deey Classic ambaye kipindi hicho alikuwa studio za rock town Mwanza. Wimbo umemuibua Kala kutoka alipokuwepo na nathubutu kusema ndio wimbo uliompa mafanikio makubwa kwa kipindi kifupi kuliko nyimbo zake zote, lakini vipi kuhusu mtayarishaji??? Malalamiko tu.
Rafiki yangu Sappi ni producer mdogo kiumri lakini ameshafanya makubwa nchini Kenya yeye akiwa ni Mtanzania pekee kwenye studio za HomeBoys. Yeye nilimuuliza mambo yalivyo huko akanijibu “Game ya huku ni professional hakuna mtu anaye record bure unless producer ametaka mwenyewe but mnasign contract before kazi ianze.” Nilimdodosa kidogo kuhusu asilimia ngapi producer ananufaika kwa mikataba ya aina hiyo akaniambia 60%…nikashtuka kidogo.
UNGEweka nguvu katika kutoa kazi nzuri zitakazoiweka cv yako vizuri. UNGE ya hapo juu haitokuwa na nguvu kama wewe ndio unambembeleza msanii. Hakika ni ngumu kumbembeleza ufanye nae kazi kisha kumpa mikataba asaini. Lakini ubora wa kazi zako ndio silaha yako kubwa ya kumshikisha Msanii kalamu na kusaini.
Niliona mkwaruzano wa Lucci na Chidi Benz kwenye swala hilihili katika mitandao, kwa waliousikia wimbo alioufanya chidi kwa lucci wanasema ni boonge la ngoma, lakini inaonekana Lucci akaintroduce swala la kisheria baadae kabisa kitu ambacho Chidi anasema si sahihi kwakuwa Lucci ndiye aliyemuita studio kwake na mpaka anafanya wimbo hakuambiwa kuhusu masuala ya kusaini. Lucci did the right thing ila alikosea procedures.
UNGEhifadhi kazi zako vizuri, sio wimbo haujakamilika ushatoa demo zaidi ya saba. Kwanini usiwe na msimamo hata kama ni msanii ndio anataka. UNGEmwambia utaratibu wa ofisi yako ni kutotoa wimbo kabla haujakamilika, hakika atasikiliza na kuheshimu. Nasema hili kwasababu mara kadhaa imetokea beat uliyofanya wewe msanii anaenda kuirudia kwa mtu mwingine na kufanya sauti upya.
Lakini pia mazingira tofauti kidogo ya hali hii ni kumpa msanii wimbo kabla hamjamalizana, somo hili alilifaulu sana Hermy B wa BHitz, sijui ni wangapi mlifuatilia sakata lake na AY na FA? Mambo hutakiwa kuwa vile, unataka chako basi twende nionavyo ni sahihi kwangu kama mtayarishaji, lakini kama angekuwa ni mtu wa kugawagawa tu nyimbo ni wazi kuwa ingekula kwake.
UNGEtanua wigo wa kazi zako kusikilizwa. Mtandao umerahisisha mambo mengi sana siku hizi, na kama unavyojua ni ngumu sana kuwafikia watu muhimu ili wasikie ufanyacho, ni wakati sasa wa kujihusisha na mitandao kama soundcloud, hulkshare, revernation, myspace na mingine mingi ambayo unaweza ukashare kazi zako na kupata nafasi zaidi.
UNGEhakikisha una identity, sizungumzii sauti unayoweka mwanzo na mwisho wa nyimbo unazofanya lah, nazungumzia utofauti wa midundo yako na ya watayarishaji wengine. Nampenda mtayarishaji huyu wa nje anaitwa Liam Geddes, yeye ni mchanga lakini ana ushauri mzuri kwako, anasema “keeping positive is essential, things take time to be released which can be a pain. Always try to make something original and different to the last track you made. Practice really makes perfect as well!”
Kama nilivyosema awali, nayafungua tu macho yako na kukuonyesha vichache, nakushauri kutazama mengine ya kukunufaisha kutokana na kile ukifanyacho, utalalamika mpaka lini? Kila la kheri na Mungu aendelee kuibariki mikono yako.
Imeandikwa na Kinye: Kinye42@gmail.com
@kinye42

Post a Comment

Previous Post Next Post