RAGE, SUALA LA OKWI HALIHITAJI UCHUNGUZI NA HAUTALIKWEPA


RAGE


Wiki iliyopita nilipokea makala ya Mwenyekiti wa Simba, Ismail Rage kupitia email, aliomba yachapishwe kwenye Gazeti la Championi ili ajibu Hoja Yangu niliyokuwa nimeandika siku kadhaa nyuma. Nikakubali ombi lake, PIA NINAYATOA KWENYE 
SALEHJEMBE KWA KUWA NILIANZA KUTOA HAPA KUANZIA MAKALA NILIYOMCHAMBUA, ALIYOJIBU NA HII.


Baada ya kusoma vizuri, nikatabasamu na kugundua mambo mawili mapema kabisa. Kwanza, uandishi wa makala hayo, nikagundua ni mmoja wa waandishi chipukizi ndiye alipewa kazi ya kuiandika baada ya kusikiliza maneno ya Rage bila ya kuyapima, nikashangazwa, lakini ni suala la ajira, siwezi kumlaumu ingawa iko siku nitamfikia.

Pili, hoja laini za Rage ambaye hata alichokisema, kilinithibitishia kwamba kila ninachoandika kuhusu yeye, kamwe sijawahi kukosea. Waswahili wanasema hivi, “ukimya ni jibu la mjinga”.

Lakini inapofikia wakati unalazimika kusema kwa maslahi ya michezo ya taifa letu, basi hakuna haja ya kunyamaza. Safari hii umemuona Rage ameamua ‘kuandika’ makala na hii ni baada ya kuona sibabaiki na lawama na vitisho vyake, kupitia watu mbalimbali ambavyo amekuwa akivitoa kujaribu kuninyamazisha, kitu ambacho naona anapoteza muda wake.

Naweza kumpongeza kwa kuona umuhimu wa kuzungumza, wenye uwezo wa kuchambua mambo huyachambua na wasioweza hutumia vitisho kwa kuwa hawawezi kujibu hoja za msingi, hata hivyo Rage amejaribu kujibu hoja ya msingi bila tafakuri, akionyesha wazi ni mtu mroho wa madaraka, asiye na huruma hata kidogo na maendeleo ya Simba na badala yake maendeleo binafsi. Kuna vingi vya kuthibitisha hilo.

Wakati akifafanua katika makala yake, eti Rage alijisifia kufanya biashara ya kumuuza Emmanuel Okwi katika Klabu ya Etoile Du Sahel kwa dola 300,000 (Sh milioni 480) ambazo ameifanya kwamba yeye ni mtu makini na ana uzoefu na biashara ya wachezaji! Nilijiuliza huyu Rage ni mzima kweli? Naamini atakuwa ana tatizo.

Mimi niliita biashara kichaa kwa kuwa hakuna fedha iliyoingia Simba hadi sasa huku Okwi akianza kurushwa kama mpira, sasa atacheza SC Villa kwa miezi sita. Kwa kipindi hiki Simba inafaidika nini, kama si biashara kichaa ni nini? Yeye anashangaa akitoa mfano wa kitu kilichonunuliwa kwa Sh 1,000 kikiuzwa Sh 1,500 kama inaweza kuwa biashara kichaa. Kweli haiwezi kuwa, sasa Simba wamemuuza Okwi au wamemgawa?

Kuonyesha Rage ni mbabaishaji kama ambavyo nimekuwa nikisema siku zote, alijisahau na kudanganya kwamba eti Okwi kama asingeuzwa kipindi hicho, angeondoka na kujiunga na timu nyingine kama Yanga au Azam FC kwa kuwa mkataba wake umebakiza siku chache.

“Ukiwa muongo, usiwe mwepesi kusahau”. Naona amesahau kwamba alipewa fedha dola 40,000 (Sh milioni 64) na kwenda Kampala, Uganda kumsainisha Okwi mkataba wa miaka miwili, kama kawaida yake yeye akachukua ujiko kama muhusika mkuu.
Bado nasisitiza kuwa ile ni biashara kichaa na ninaweza kufafanua hivi, kwamba hakuna ambacho Simba inafaidika katika mauzo ya Okwi zaidi ya ‘stress’ za kuendelea kudai, huku ikipata hasara ya kupiga simu au kusafirisha watu kwenda kudai fedha zao Tunisia.

Hakuna mfanyabishara mwenye malengo anaweza kufanya ujinga wanaofanya Simba katika kipindi hiki kwa kuwa wanaendelea kupoteza muda na hii yote inatokana na Rage, kama angekuwa makini siku husika ya biashara, basi leo Simba isingekuwa ikihagaika na kupoteza fedha kama ilivyo sasa.

Wakati Simba inamuuza Okwi ilikuwa inashiriki michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, Mganda huyo alikuwa tegemeo katika kuanzisha mashambulizi. Ikamuuza, halafu haikupata hata shilingi, hilo likachangia timu kuzorota na mwisho kuambulia vipigo vya aibu kutoka kwa FC Liboro ya Angola ikiwa nyumbani ikalala 1-0 na ugenini 4-0. Bado Rage anaona hiyo ni biashara safi sana.

Kama faida, basi Simba ingepata fedha kipindi kile kwa kuwa ilikuwa inazihitaji sana kujiimarisha, ikashindikana. Hadi leo haijazipata, lakini Rage anaiita biashara na tena anajisifia, kweli duniani, kila mmoja ana uwezo wake tofauti wa kufikiri!

Kilichomuuma ni mimi kusisitiza kwamba fedha za Okwi ziondoke na kichwa cha mtu, ndiyo maana kwa kiongozi makini anaweza kujipima kwa kosa kubwa moja na kuona kweli anastahili kujiuzulu kwa maslahi ya anachokiongoza, najua Rage hawezi na ndiyo maana anasifia madudu aliyoyafanya akilazimisha kioo kiwe almasi, kitu kisichowezekana hata iwe vipi.

Anasema Simba wamekuwa na mafanikio sana, wamechukua makombe tena alivyo msahaulifu anakumbushia hadi Kombe la BancABC ambalo timu ya vijana ya Simba ambao aliwazungusha kuwapa fedha zao za ubingwa walizoahidiwa na hadi leo bado kuna fedha ambazo hawajalipwa. Huyu jamaa mzima kweli?

Lakini ajabu, katika makala hayo, Rage alijisifia eti si wao Simba tu ambao wanaidai Etoile du Sahel akitolea mfano wa timu nyingine, akiwemo wakala Msenegali. Sasa Simba linawahusu nini! 
Hao Wasenegal wanapaswa kuangalia yao na Simba yake, unajisifia kuingia kwenye matatizo eti kwa kuwa na wengine pia wamo humo, ehh! Huyo ndiyo Rage bana!

Rage amekuwa ni mtu wa kufeli karibu kila anachohusika kama lile suala la kumsainisha Mbuyu Twite jijini Kigali, Rwanda, mwisho akaishia kutumia picha aliyopiga naye akiisambaza kwenye mkutano wa wanachama wa Simba, kuonyesha alivyofanikiwa. 

Haikutosha hapo, akaibandika kwenye mtandao wa kijamii wa Facebook, halafu siku chache baadaye beki huyo akatua Yanga, huku akisema alipiga picha na Rage kama shabiki wa kawaida! Kumbuka Simba ilipata hasara, tiketi ya ndege na baadhi ya fedha, lakini aibu kwa kuonekana mwenyekiti wake anafanya mambo ya kubahatisha, kwake si tatizo, maana amezoea kubahatisha.

Leo kamuuza Okwi, hadi hapa unaposoma makala haya, Simba haijapata hata senti tano ya malipo ya fedha hizo, yeye anajisifia na kuona amefanya biashara kwa uzoefu mkubwa! Tena kwa tambo huku akisema eti ninapaswa kufanya utafiki kwanza, la sivyo nitakuwa kasuku!

Ametoa mfano wa kauli hiyo ya Mwenyekiti Mao, bila ya kujua aliitumia katika sehemu isiyo sahihi, karukia maneno kutokana na umasikini wake wa maneno ya Kiswahili (sababu anaijua).

Ukweli suala hilo wala halihitaji uchunguzi, ukweli ni kwamba Simba imefanya biashara ya dola 300,000 hadi sasa haijapata kitu na hakukuwa na haja ya haraka kwa kuwa Okwi tayari aliongeza mkataba na Simba na kama Waarabu hao walisema hawana fedha, basi Okwi angebaki na kuendelea kuitumikia timu yake hadi miezi michache baadaye katika dirisha litakapofunguliwa tena wangekuja kumnunua wakati wana fedha. Sasa nini cha kuchunguza hapa?

Siku moja niliwahi kumpigia simu Rage na kumuuliza hivi, kwamba nina taarifa kuwa akiwa Tunisia alifanya mambo mawili ya kijinga. Kwanza, Etoile walitangaza kumnunua Okwi kwa dola 500,000 (Sh milioni 800), akiwa huko yeye akawataarifu baadhi ya wajumbe wa kamati ya utendaji kwamba bei imepungua hadi kufikia dola 300,000.

Lakini taarifa zikaeleza katika dola 200,000 iliyopunguzwa, Rage ‘alikatiwa’ asilimia 10, yaani dola 20,000 (Sh 32m) kama shukurani ya kukubali kupunguza hiyo bei. Pili, kukawa na taarifa kwamba alikuwa akimuomba fedha Okwi mara tu baada ya mchezaji huyo kulipwa mamilioni kama fedha zake za kukubali kuingia mkataba na Etoile. Rage akaniambia maneno yote hayo ni uzushi, sikuridhika kwa dhati, ila nikaachana nayo.

Lakini bado nikabaki na hofu kwa kuwa mwenendo wake na hasa maneno yake ya kubabaisha, yakazidi kunibabaisha. Huyu mtu ni tatizo katika mchezo wa soka nchini na si Simba tu.
Ingekuwa ni kutumia neno kasuku, basi yeye ndiye angeendana na kila kitu, kwamba ana maneno mengi mazuri lakini katika utekelezaji ni tatizo kubwa na ana uwezo mkubwa wa kusema maneno kwa mbwembwe, utekelezaji wake ni sifuri.
Angalia mambo ya ujenzi wa uwanja, kuna mengi tu ambayo yanaweza kuwa sehemu ya kuonyesha madudu wakati wa uongozi wa Rage.
Makocha wawili Wazungu katika msimu mmoja, mmoja akalazimika kupata msaada wa kulipa, mwingine hadi sasa yuko jijini Dar akihaha kulipwa. Nitaishia hapa, nitampa nafasi Rage aendelee kutoa anazoziita hoja zake, halafu nitahamia katika upande huo wa makocha, ujenzi wa uwanja, namna anavyong’ang’ania fedha za tiketi ili apate ‘pasu’ na mengine mengi ambayo kabla sikuwahi kuyagusa ili kuwaonyesha kiasi gani kuwa mtu huyu mheshimiwa ni chui mwenye ngozi ya kondoo, mwenye maneno matamu kama chiriku lakini mwenye hamu kubwa ya kuitumikia nafsi yake tu.

Post a Comment

Previous Post Next Post