Hali bado si shwari katika Jamhuri ya Afrika ya Kati

Licha ya wito wa Rais mpya wa Jamhuri ya Afrika ya Kati wa kutaka kufanya mazungumzo na makundi ya wanamgambo na wito wake wa kurejeshwa amani katika nchi hiyo, habari kutoka mji mkuu Bangui zinasema kuwa, hali bado si shwari kutokana na kuendelea kushuhudiwa machafuko. 

Jana mapigano makali yalishuhudiwa katika mji mkuu Bangui ambapo watu wasiopungua 9 walipoteza maisha yao na makumi ya wengine kujeruhiwa. 

Mapigano hayo yalijiri huku Rais Catherine Samba-Panza akianza maisha mapya katika Ikulu ya Rais baada ya kuapishwa kuwa Rais wa muda wa nchi hiyo. 

Taarifa zaidi zinasema kuwa, hali ya ukosefu wa amani ingali inashuhudiwa katika mji mkuu Bangui. 

Hayo yanajiri katika hali ambayo, Shirika la Kimataifa la Kutetea Haki za Binadamu la Amnesty International limeripoti kwamba, kwa akali Waislamu 50 wameuawa baada ya wanamgambo wa Anti Balaka kushambulia vijiji viwili kaskazini magharibi mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati. 

Wiki iliyopita pia, wanamgambo wa Kikristo wa Anti-Balaka waliwaua Waislamu 22, wakiwemo watoto watatu na kuwajeruhi makumi ya wengine. 

Mapigano ya ndani katika Jamhuri ya Afrika ya Kati yalianza mwezi Machi mwaka jana baada ya kung'olewa madarakani serikali ya aliyekuwa Rais wa nchi hiyo François Bozizé.

Post a Comment

Previous Post Next Post