Mbeya City Vs Simba leo

Wachezaji wa timu ya Mbeya City wakipasha kabla ya mechi. Leo wanatupa karata yao katika Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya, wakiwakabili wekundu wa Msimbazi Simba ya Jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Wakati vinara wa Ligi Kuu, Azam na Yanga wakiwa katika michezo ya kimataifa nje ya nchi, macho na masikio ya mashabiki wa soka  leo yatakuwa jijini Mbeya wakati Mbeya City watakapoikaribisha Simba kwenye Uwanja wa Sokoine.
Vinara wa ligi Azam wenye pointi 36, wapo Maputo wakiikabili Ferroviano katika Kombe la Shirikisho kesho, mabingwa watetezi Yanga (35) leo watashuka uwanjani Comoro kuikabili Komorozine katika Ligi ya Mabingwa.
Mbeya City, ipo katika nafasi ya tatu katika msimamo  ikiwa na pointi 34, wanajua ushindi wa leo dhidi ya Simba inayoshika nafasi nne na pointi 31 utawapeleka kileleni kwa kwa mara ya kwanza mwaka huu.
Simba wanashuka kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya wakiwa na kumbukumbu ya kunyukwa bao 1-0 na Mgambo Shooting katika mechi yao iliyopita, hivyo wanautazama mchezo dhidi ya Mbeya City kama fursa ya kurekebisha makosa yao.
Kocha wa Simba, Zdravko Logarusic ambaye tayari ametangaza kunawa mikono katika vita ya kusaka ubingwa amekiri kwamba shughuli itakuwa pevu leo.
“Tukutana na timu yenye rekodi nzuri katika ligi kwani imepoteza mchezo mmoja tu hivyo ni dhahiri tunatakiwa kupambana kufa na kupona ili kupata ushindi,”alisema Logarusic.
Kocha wa Mbeya City Juma Mwambusi akizungumzia mchezo huo alisema, utakuwa mkali na wenye upinzani wa ajabu, lakini kikosi chake kimejiandaa kuitoa machozi Simba.
“Simba ni timu kubwa na tunaiheshimu, lakini mwisho wa siku soka inachezwa sehemu ya wazi na idadi ya wachezaji ni 11 kwa kila  timu hivyo sina shaka kwamba kikosi changu kipo tayari kuvuna pointi tatu,” alisema kocha huyo wa zamani wa Prisons.
Pia, utamu wa ligi  hiyo utashuhudiwa katika  viwanja vingine vitano Kwenye Uwanja wa Manungu, Mtibwa Sugar  itapepetana na Prisons, Mgambo Shooting itakung’utana na  Rhino Rangers kwenye Uwanja wa Ali Hasani Mwinyi, Ruvu Shooting itapimana ubavu na Coastal Union kwenye Uwanja wa  Mabatini.
Wakati JKT  Oljoro itavutana mashati na JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid kadhalika Ashanti United itakuwa kwenye Uwanja wa Azam Complex kumenyana na Kagera Sugar

Post a Comment

أحدث أقدم