News: Barcelona sasa kuuza na kununua wachezaji baada ya Fifa kuitupilia mbali adhabu yake

Klabu ya Barcelona sasa inaweza kununua na kuuza wachezaji katika kipindi hiki cha usajili baada ya Fifa kutupilia mbali adhabu yake iliyotoa kwa klabu hiyo ya kutosajili.
Miamba hiyo ya Uhispania ilipewa adhabu ya miezi 14 kutonunua wamchezaji baada ya kuthibitika kuvunja sheria kwa kuwasajili wachezaji wa kimataifa walio na umri wa chini ya miaka 18 ingawa sasa adhabu hiyo imetupwa kapuni.
Barca ilihusishwa na kutaka kumsanisha mlinda mlango kinda wa Borussia Monchengladbach Marc-Andre ter Stegen na kuwa na dili la kutaka kumsainisha kiungo wa Croatia Alen Halilovic.
Nahodha wa klabu hiyo Carles Puyol na mlinda mlango wa muda mrefu Victor Valdes wametangaza kuitema klabu hiyo mwishoni mwa msimu huu.
Mabingwa hao wa Uhispania walikutana na rungu la Kamati ya Nidhamu ya Fifa 2 April mwaka huu kwa kuvunja sheria ambapo waliadhibiwa kutosajili kwa kipindi cha miezi 14 ingawa waliruhusiwa kuuza wachezaji pekee na kutozwa faini ya franga za Uswis 450,000.
Baada ya Barcelona kufuata ahadi ya kukata rufani, Fifa iliamua kwamba kutokana na uzito wa kesi yenyewe na uwezekano wa kukata rufani katika Court of Arbitration for Sport (Cas), ikataka kuimaliza kabla ya ufunguzi wa dirisha la usajili ambalo litafunguliwa rasmi 1 July na kwa hiyo ikatupa kapuni adhabu hiyo.
Sheria za Fifa zinaeleza  kwamba uhamisho wa kimataifa unaruhusiwa tu kwa wachezaji waliokuwa na umri wa zaidi ya miaka 18 - au mchezaji husika awe na sababu kuu tatu.
Mchezaji wa chini ya umri wa miaka 18 anaweza kuhamia kwenye klabu ya nchi nyingine kama wazazi wake watakwenda nchini humo kwa sababu zisizokuwa na kimpira, au kama wanatoka katika nchi nyingine ambayo ni mwanachama wa Umoja wa Ulaya au Jumuia ya Uchumi ya Ulaya na awe na umri kati ya miaka 16 na 18, au wanaishi ndani ya 100km za klabu.

Post a Comment

Previous Post Next Post