Logarusic aibomoa Mbeya City

Kocha Mkuu wa Simba, Zdravko Logarusic.

IMEFAHAMIKA kuwa, Simba imepanga kuibomoa Mbeya City katika usajili wa msimu ujao kwa kuwasajili wachezaji watano kwenye kikosi cha timu hiyo kinachofundishwa na Juma Mwambusi.
Timu mbalimbali za Ligi Kuu Bara hivi sasa zipo kwenye usajili kwa ajili ya kuviimarisha vikosi vyao kuelekea msimu ujao uliopangwa kuanza Agosti, mwaka huu.
Baadhi ya wachezaji wanaotajwa kuwaniwa na klabu hiyo ni mshambuliaji Saad Kipanga na kiungo mkabaji Anthony Matogolo ‘Mmasai’ aliyewasumbua viungo wa Simba, Yanga na Azam FC ndani ya msimu uliopita.
Kwa mujibu wa chanzo cha habari kutoka ndani ya uongozi wa Simba, wachezaji hao wanaotaka kuwasajili ni mapendekezo katika sehemu ya ripoti ya Kocha Mkuu, Mcroatia, Zdravko Logarusic.
Chanzo hicho kilisema, wakati wakiwawania wachezaji hao, uongozi wa Simba umekata tamaa ya kuwapata nyota hao kutokana na urefu wa mikataba yao.
“Hivi sasa tumelisimamisha zoezi la usajili hadi pale tutakapowapata viongozi wapya katika uchaguzi wetu watakaoiongoza Simba.
“Wakati tukisubiria uchaguzi huo kupita, baadhi ya viongozi wa Kamati ya Utendaji ya Simba wanaendelea kupitia mapendekezo ya ripoti ya kocha ambayo inatupa ugumu katika usajili kwa kuwa inahitaji wachezaji watano katika kikosi cha Mbeya City na wote wana mikataba mirefu,” kilisema chanzo hicho.
Alipotafutwa Mwenyekiti wa Mbeya City, Mussa Mapunda, alisema: “Sasa hao Simba wakiwachukua wachezaji hao watano si wataiua timu yenyewe yote, lakini acha tuangalie, wao waje tufanye mazungumzo.”

Post a Comment

أحدث أقدم